Mtandao #1 kwa Afya ya Mama na Mtoto

Address:

P. O. Box 38995, Dar es Salaam, Tanzania

Maumivu ya Mgongo Wakati wa Ujauzito

Habari njema ni kuwa mtoto wako anaendelea kukua. Maumivu makali katika mgongo kipindi hichi yanasababishwa na ukuaji wa mtoto tumboni.

Kumbuka sio wewe tu unayepitia hali hii,wajawazito wengi wanaanza kupatwa na hali hii mara nyingi kuanzia kipindi cha pili cha miezi mitatu ya ujauzito.

Makala hii itakupa nafasi ya kufahamu vidokezo vitakavyokusaidia kupunguza maumivu ya mgongo kipindi cha ujauzito.

Chanzo cha maumivu ya mgongo kwa mama wajawazito

Kawaida maumivu ya mgongo wakati wa ujauzito yanatokea sehemu ambayo nyonga na uti wa mgongo vinakutana (sacroiliac joint)

Maumivu ya mgongo yanachangiwa na mambo mengi.  Zifuatazo ni sababu zinazoongeza nafasi ya maumivu ya mgongo kutokea kwa wajawazito:

  • Kuongezeka uzito. Wakati wa ujauzito ambao ni salama, kawaida wanawake huongezeka uzito (kilo 11-16). Kazi ya kuhimili uzito huu inafanywa na uti wa mgongo. Hii inaweza kusababisha maumivu ya sehemu ya chini ya mgongo. Uzito wa mtoto anayekua na uterasi vinasababisha mgandamizo kwenye mishipa na mirija ya damu inayopatikana katika nyonga na mgongo.
  • Mabadiliko ya mkao. Uzani wa mtoto, uterasi na kiowevu cha amnioni hubadili mkao wak na kuweka mkazo kwenye mifupa na misuli ya mgongo wa mama mjamzito.Taratibu bila hata kujua utaanza kubadilisha mkao wako na jinsi unavyotembea,hali hii inaweza kusababisha maumivu ya mgongo.
  • Mabadiliko ya homoni. Wakati wa ujauzito, mwili unatengeneza homoni iitwayo “relaxin” ambayo inaruhusu ligamenti katika nyonga kupumzika na viungo kulegea kwaajili ya maandalizi ya kujifungua. Homoni hii inasababisha ligamenti zinazosaidia uti wa mgongo kufanya kazi vizuri kulegea pia, hali hii inasababisha maumivu.
  • Msongo wa mawazo. Msongo wa mawazo unaweza kusababisha mvutano wa misuli inayopatikana kwenye mgongo,hali hii inaweza kusababisha maumivu ya mgongo kwa mama mjamzito.

Matibabu kwaajili ya maumivu ya mgongo kwa mama mjamzito

Habari njema zaidi: maumivu ya mgongo yanaweza kupungua taratibu kabla ya kujifungua isipokuwa kama ulikuwa na matatizo ya kudumu ya mgongo kabla ya kubeba ujauzito.

Wakati huohuo, yapo mambo mengi unaweza kufanya kutibu sehemu ya chini ya mgongo wako au kupunguza maumivu haya:

  • Kufanya mazoezi kila mara, mazoezi salama kwa mjamzito kama kutembea, kuogelea yanaweza kunyoosha misuli na kupunguza mvutano katika uti wa mgongo. Mkunga wako anaweza kukushauri mazoezi ya kunyoosha mgongo na fumbatio ambayo ni salama kwako na ujauzito wako.
  • Tumia vitu vya baridi au joto kutuliza maumivu ya mgongo. Zungumza na mkunga au daktarin wako anayesimamia maendeleo ya ujauzito wako kama ni salama kutumia njia hii. Unaweza kuanza kwa kuweka kitu cha baridi (mfuko wenye barafu au njegere zilizoganda) kwa dakika 20 eneo lenye maumivu. Baada ya siku mbili au tatu ukabadilisha na kuweka chupa ya plastiki au mpira maalumu wa maji ya moto eneo lenye maumivu. Kuwa makini usisababisha maumivu kwenye fumbatio wakati wa ujauzito.
  • Imarisha mkao wako. Kuchechema kunaumiza uti wako wa mgongo. Hivyo basi, mkao mzuri wakati unafanya kazi, kaa kitako au kulala ni hatua nzuri. Kwa mfano, wakati wa kulala-lala kwa upande kwa msaada wa mto katikati ya magoti ili kutoa mkazo mgongoni. Ukiwa umekaa kwenye dawati ofisini, weka mto au taulo iliyoviringishwa vizuri nyuma ya mgongo wako kuupa msaada mgongo. Vilevile pumzisha miguu yako juu ya vitabu kadhaa ulivyovipanga au kigoda kisha kaa kwa kunyooka, mabega yako yakirudi nyuma. Ikiwezekana vaa mkanda maalumu unasaidia.
  • Ushauri nasaha. Ikiwa maumivu yako ya mgongo yanahusiana na msongo wa mawazo, kuongea na rafiki yako unayemwamini au mshauri nasaha inaweza kukusaidia.
  • Matibabu ya kutumia sindano(acupuncture) hii ni aina ya dawa kutoka China ambapo sindano nyembamba zinatumika kuchomwa kwenye ngozi katika maeneo fulani. Utafiti unaonyesha aina hii ya matibabu inaweza kutuliza maumivu ya mgongo wakati wa ujauzito. Ongea na daktari wako kama ni salama kwako na upatikanaje wake.

Vidokezo zaidi:

  • Ikiwa unataka kuokota kitu chini, tumia miguu yako kuchuchumaa kuliko kuinama.
  • Usivae viatu vyenye kisigino kirefu.
  • Usilale kwa mgongo

Ikiwa maumivu yako yatazidi, ni busara zaidi kumuona dakatari, ili kuona kama kuna hatua nyingine inaweza kuchukuliwa. Hakikisha unapata maelekezo au ushauri kutoka kwa daktari anayesimamia maendeleo ya ujauzito wako kabla ya kutumia dawa yeyote kutumiza maumivu. Acetaminophen (Tylenol) ni salama kwa mama mjamzito. Dawa kama Asprin na dawa nyinginezo za maumivu kama ibuprofen (Advil,Motrin) au naproxen(Aleve) hazishauriwi kutumika kwa mama mjamzito.

Kwa baadhi ya wanawake, maumivu ya mgongo sio sababu pekee ya kuwasiliana au kumuona daktari. Lakini inakubidi umuone daktari haraka iwezekanavyo ikiwa utapata dalili zifuatazo:

  • Maumivu makali sana
  • Ongezeko la maumivu haya makali au maumivu yanayoanza ghafla.
  • Shida kukojoa au kuhisi hali ya kuchomwa na pini au sindano kwenye mikono na miguu.
  • Maumivu yanayofuatana katika fumbatio.

KUMBUKA

Katika hali nadra, maumivu makali ya mgongo yanaweza kuhusishwa na shida kama vile ugonjwa wa mifupa “osteoporosis”-hali ambayo mifupa inakua dhaifu na yenye kuvunjika kwa urahisi. Maumivu yanayofuatana inaweza kuwa ishara ya uchungu wa kujifungua kabla ya muda. Kwa hivyo ikiwa unapata shida hizi, ni muhimu kuchunguzwa na daktari wako hospitalini.

IMEPITIWA: APRILI, 2021.

Maumivu ya Tumbo na Kukakamaa kwa Fumbatio Wakati wa Ujauzito

Ujauzito unakuja na baadhi ya hali ambazo zinaweza kumkosesha utulivu mama mjamzito kama vile matiti kuongezeka ukubwa au maumivu ya mgongo na kiuno.  Maumivu ya tumbo na kukakamaa kwa fumbatio (abdominal cramping) kunaweza kukufanya upate wasiwasi haswa kama wewe ni mjamzito.

Baadhi ya maumivu haya wakati wa ujauzito ni kawaida, lakini wakati mwingine yanaweza ashiria tatizo linalohitaji matibabu haraka iwezekanavyo. Maumivu haya yanaweza kutokea wakati wowote katika ujauzito. Kupitia makala hii utaweza kufahamu kama maumivu ya tumbo na kukakamaa kwa fumbatio wakati wa ujauzito ni kawaida au ni ishara unahitaji matibabu na ushauri wa daktari haraka.

Je, mikakamao hii wakati wa ujauzito ni kawaida?

Baadhi ya maumivu ya tumbo na kukakamaa kwa fumbatio wakati wa ujauzito ni kawaida na hayana madhara kipindi cha ujauzito. Maumivu yanayosababishwa na ukuaji wa uterasi,maumivu ya ligameti zinazoshikilia uterasi,kukosa choo au kuvimbiwa na mikazo ya leba ya uwongo (Braxton Hicks contractions).

Maumivu ya tumbo yanayosababishwa na ujauzito kutungwa nje ya uterasi,kutoka au kuharibika kwa mimba changa (miscarriage), uchungu wa kujifungua kabla ya wiki 37 za ujauzito (preterm labor),tatizo la kondo la nyuma kuachia kabla mtoto hajazaliwa (placenta abruption), kifafa cha mimba (preeclampsia), maambukizi katika njia ya mkojo (UTI) na ugonjwa wa kidole tumbo(appendicitis) wakati wa ujauzito ni hatari. Siku zote ni salama kuwasiliana na mtaalamu wa afya anayesimamia maendeleo ya ujauzito wako ikiwa utapata dalili zinazokupa wasiwasi.

Chanzo cha maumivu ya tumbo na mikakamao ya fumbatio wakati wa ujauzito

Zifuatazo ni sababu za kawaida za maumivu na mikakamao ya fumbatio wakati wa ujauzito ambayo inaweza kutokea kipindi chochote cha miezi mitatu ya ujauzito:

Tumbo kujaa gesi

Gesi na kuvimbiwa ni malalamiko ya kawaida kipindi cha ujauzito yanasababishwa na ongezeko la viwango vya homoni ya projesteroni, homoni inayohusika na kutuliza misuli laini ndani ya njia ya mmeng’enyo.

Matokeo yake ni kuvimbiwa ikiambatana na kukosa choo kwasababu mmeng’enyo wa chakula unafanyika taratibu- hali zote hizi zinaweza kusababisha kuhisi fumbatio lako kukakama.

Tatizo lako la kiafya linahusishwa na mmeng’enyo wa chakula iwapo utakuwa unatoa hewa nje ya mwili kwa kujamba au baada ya kujisaidia haja kubwa unapata unafuu. Unaweza kuzuia kupata shida hizi zinazohusiana na mfumo wa umeng’enyaji wa chakula kwa kula vyakula vya nyuzinyuzi (fiber), kula milo midogo midogo badala ya kula milo mitatu mikubwa, chukua muda wako kutafuna vizuri na taratibu chakula. Ikiwa mabadiliko haya madogo hayatasaidia, wasiliana na daktari au mhudumu wa afya anayesimamia maendeleo ya ujauzito wako kila miadi kwa ushauri na matibabu zaidi.

Mikakamao ya fumbatio inayotokea baada ya kufika kileleni(orgasm) wakati wa tendo la ndoa

Wakati mwingine mikakamao hii inafuatwa na maumivu ya sehemu ya chini ya mgongo, ambayo ni kawaida na una hatari ndo kwa ujauzito ulio salama. Sababu ya maumivu haya baada na wakati mama anapofika kileleni ni ongezeko la mtiririko wa damu kwenye nyonga na mikazo ya kawaida ya uterasi inayotokea kila mama anapofika kileleni.

Usiwe na hofu ya mtoto wako kuumia kila unapofika kileleni, yuko salama. Jaribu kufurahia tendo hili ikiwa daktari au mtoa huduma wako atakuruhusu kufanya tendo la ndoa wakati wa ujauzito. Kutuliza mikakamao na maumivu haya, jaribu kujilaza kitandani au kulala kidogo baada ya tendo.

Mtiririko wa damu kwenye uterasi

Wakati wa ujauzito, mwili wako unatuma damu nyingi zaidi ya kawaida kwenye uterasi. Hii inapelekea kuhisi mgandamizo eneo hilo. Jilaze kitandani upate kupumzika au oga kwa maji ya moto inaweza kusaidia kutuliza maumivu haya.

Maambukizi katika njia ya mkojo (UTI)

UTI inaweza isiwe na dalili, lakini mara nyingi inasababisha maumivu au mgandamizo eneo la nyonga. Dalili nyingine ni kama harufu mbaya, rangi tofauti au damu kwenye mkojo, maumivu na kuungua wakati wa kukojoa, homa au kutaka kukojoa kila mara. UTI ni hatari isipo tibiwa vizuri na mapema. Bahati nzuri matumizi mazuri mpaka mwisho ya antibiotiki yanatibu maambukizi haya.

Ukosefu wa maji mwilini

Ukosefu wa maji ya kutosha mwili unaweza kusababisha leba ya uwongo au mikazo ya uterasi katikati ya ujauzito ambayo ni kawaida. Kunywa maji ya kutosha kila unaposikia kiu, baadhi ya tafiti zinaonyesha ukosefu wa maji uliokithiri unaweza ongeza hatari za kupata uchungu na kujifungua kabla ya muda.

Lenga kunywa angalau glasi 8 mpaka 10 za maji kwa siku. Mkojo kuwa na rangi ya njano iliyopauka ni moja ya ishara una maji ya kutosha mwilini.

Maumivu tumbo na mikakamao kwenye fumbatio miezi mitatu ya kwanza ya ujauzito

Upandikizaji

Mapema baada ya kujua una ujauzito, unaweza kupatwa maumivu ya tumbo la uzazi kama yale ya siku za hedhi. Maumivu haya hutokea siku ambayo hedhi yako ilitarajiwa kutokea, kabla hata hujapata uhakika umepata ujauzito.

Vichomi vya mbali na kuona damu kidogo kwenye nguo zako za ndani ni matokeo ya yai lililorutubishwa kujipandikiza kwenye ukuta wa mfuko wa uzazi (uterasi), hali hii inatokea siku ya 6 mpaka 12 baada ya urutubishaji wa yai na inadumu kwa siku moja.

Mimba kutungwa nje ya mfuko wa uzazi (Ectopic pregnancy)

Wakati yai lililorutubishwa linajipandikiza sehemu tofauti, mara nyingi katika mirija ya falopia-inaweza kusababisha maumivu na mikakamao sehemu ya chini ya fumbatio.

Maumivu haya yanaweza anza taratibu na kuongezeka kadiri muda unavyoenda. Mara nyingi ujauzito wa aina hii unasababisha maumivu ya mabega, kutoka damu ukeni,kizunguzungu na kuzimia.

Ikiwa unahisi una dalili za ujauzito huu, tafadhali onana na daktari mapema. Uchunguzi wa aina hii ya ujauzito unafanywa kwa kipimo cha ultrasound na vipimo vya damu wiki ya 5 mpaka 6 ya ujauzito.

Kutoka au kuharibika kwa mimba changa (miscarriage)

Kukakamaa kwa fumbatio na maumivu ya tumbo miezi ya kwanza ya ujauzito inahusishwa na mimba kutoka au kuharibika, maumivu haya yanaweza fananishwa na yale ya kipindi cha hedhi. Mara nyingi hutokea kwenye fumbatio, sehemu ya chini ya mgongo na eneo la nyonga, huambatana na kutoka damu ukeni.

Inaweza kuwa ngumu kugundua kama maumivu unayoyapata mwanzoni wa ujauzito ni dalili ya mimba kutoka, upandikizwaji wa yai lililorutubishwa au kupanuka kwa uterasi. Njia pekee itakayokusiaidia ni kuangalia kwa makini damu inayotoka ukeni. Mimba kutoka au kuharibika inaambatana na utokwaji wa damu ukeni kwa siku kadhaa na mara nyingi inaongezeka uzito kadiri siku zinavyoongezeka ukilinganisha na upandikizwaji wa yai. Ikiwa una wasiwasi wasiliana na mtoa huduma za afya, ikiwezekana tembelea kituo cha afya kilicho karibu na wewe.

Maumivu tumbo na mikakamao kwenye fumbatio miezi mitatu ya pili ya ujauzito

Maumivu ya ligamenti zinazoshikilia uterasi

Ujauzito unavyoendelea kukua, ligamenti hizi huvutika na kusababisha maumivu ya ghafla ambayo hutokea upande mmoja au pande zote za eneo la chini la fumbatio.

Mara nyingi maumivu haya huanza kipindi cha pili cha miezi mitatu ya ujauzito, hutokea wakati wa mazoezi, baada ya kuamka kitandani, ukipiga chafya, ukikohoa/ukicheka au ukiasogea ghafla. Maumivu haya hukoma baada ya dakika chache. Kusugua kwa taratibu au kuweka kitambaa chenye joto kwenye fumbatio kunaweza kusaidia. Jaribu pia kupumzika na kugeuka taratibu kila unapobadili mkao wako.

Leba ya uwongo (Braxton Hicks contractions)

Zinaweza kutokea kuanzia wiki ya 20 ya ujazuito, ni njia za mwili wako kukutaarifu ujio wa siku ya kweli ya kujifungua. Mikazo hii hudumu kwa sekunde chache na haina mpangilio.

Kama utapatwa na mikakamao hii kipindi cha pili cha miezi mitatu ya ujauzito na kuendelea, jaribu kubadili mkao wako. Lala au kaa kitako kama ulikua umesimama mpaka maumivu yatakapotoweka.

Kumbuka: tatizo la kondo la nyuma kuachia kabla ya mtoto kuzaliwa (placenta abruption), kifafa cha mimba na mama kujifungua kabla ya wiki ya 37 vinaweza kutokea katika kipindi cha pili cha miezi mitatu ya ujauzito.

Maumivu tumbo na mikakamao kwenye fumbatio miezi mitatu ya mwisho ya ujauzito

Tatizo la kondo la nyuma kuachia kabla mtoto kuzaliwa (placenta abruption)

Ikiwa kondo la nyuma litatengana (kidogo au lote) na ukuta wa uterasi kabla mtoto kuzaliwa, inaweza kusababisha maumivu makali na yanayo jirudiarudia, vilevile maumivu ya mgongo na kutokwa damu ukeni.

Tatizo hili linatokea sana miezi mitatu ya mwisho ya ujauzito, lakini pia linaweza tokea miezi mitatu ya pili ya ujauzito. Ikiwa unapatwa na mikakamao ya fumbatio inayoambatana na kutokwa damu ukeni, wasiliana na daktari au mkunga anayesimamia maendeleo ya ujauzito wako haraka kupata huduma za kitabibu.

 Kifafa cha mimba

Mara nyingi hali hii hutokea kipindi cha mwisho cha ujauzito na inajulikana kupitia dalili kama shinikizo la ghafla la damu na uwepo wa protini katika mkojo.

Inaweza sababisha maumivu ya sehemu ya juu ya fumbatio yanayoambatana na kuumwa kichwa sana ambacho hakitulizwi kwa dawa, mikono na uso kuvimba sana, mabadiliko ya uwezo wa kuona, ongezeko la uzito ambao hauhusiani na ulaji wako, kichefuchefu au kutapika na kupumua kwa shida.

Ni muhimu kumuona daktari au mkunga wako ikiwa unapitia dalili zilizotajwa hapo awali. Kumbuka kifafa cha mimba ambacho hakitatibiwa vizuri ni hatari kwako na mtoto wako, kwasababu kinapunguza kiasi cha oksijeni na lishe inakwenda kwa kijusi tumboni. Pia inaongeza nafasi ya kupata tatizo la kondo la nyuma kuachia kabla mtoto kuzaliwa. Ikigundulika mapema na kutibiwa una uwezekano mzuri wa kuwa na ujauzi wenye afya.

Kubana na kuachia kwa misuli wakati wa kujifungua (Labor contractions)

Uchungu wa uzazi hutokana na kubana na kuachia (tena kwa kurudiarudia) kwa misuli katika tumbo la uzazi. Misuli hii inavyobana na kuachia taratibu husababisha kufunguka kwa mlango wa tumbo la uzazi. Kubana na kuachia kwa misuli hutokea taratibu na yenye mpangilio maalumu,idadi ya marudio ya mikazo ya uterasi ni mara 3-4 kila dakika 10 na kila mkazo huchukua sekunde 40-60

Mkazo au mbano wa tumbo la uzazi mwanzoni hauchukui muda mrefu. Huachia mama anapopumzika. Unapokaribia kujifungua hapo ndipo uchungu wa uzazi wa kweli huja kwa nguvu, haupungui hata ukibadili mkao wako. Dalili nyingine za kujifungua ni pamoja na mgandamizo eneo la nyonga (kama mtoto anasukuma kushuka chini) na mabadiliko ya uchafu unaotoka ukeni (damu nyepesi au uvujaji wa majimaji ya ukeni).

Katika miadi yako daktari au mkunga wako alikutaarifu kuwasiliana nae ikiwa utapatwa dalili za mikakamao ya fumbatio kipindi hiki cha mwisho cha ujauzito ikiwa utahisi ni uchungu wa uzazi. Ukipatwa na dalili kama kupasuka kwa chupa ya uzazi, kutokwa damu ukeni au kama una dalili zozote za ghafla za kifafa cha mimba ghafla wasiliana na daktari au mkunga anayesimamia maendeleo ya ujauzito wako.

Ikiwa unapata dalili hizi kabla ya wiki ya 37 ina maanisha utajifungua kabla ya muda, wasiliana pia na mkunga wako hata kama hauna uhakika au tembelea hospitali unayotarajia kujifungulia mara moja.

Jinsi ya kupunguza maumivu ya ujauzito

Utulizaji wa maumivu ya tumbo na mikakamao kwenye fumbatio wakati wa ujauzito hutegemea sababu ya maumivu unayoyapata. Vidokezo hivi vinaweza kusaidia kutuliza sababu za kawaida zinazopelekea maumivu ya tumbo na mikakamao ya fumbatio wakati wa ujauzito:

  • Laza mwili wako na pumzika kwa muda, itasaidia kutuliza maumivu yanayohusiana na upandikizaji, kufika kilele wakati wa ujauzito, ongezeko la mtiririko wa damu kwenye uterasi na maumivu ya ligameti zinazoshikilia uterasi.
  • Kunywa maji ya kutosha, itasaidia kutuliza maumivu yanayohusiana na ukosefu wa maji ya kutosha mwilini, kukosa choo au kuvimbiwa.
  • Oga kwa maji ya moto kutuliza maumivu yanayohusiana na ongezeko la mtiririko wa damu kwenye uterasi.
  • Badilisha mkao kama unapatwa na mikazo ya leba ya uwongo
  • Tumia mikanda maalum kusaidia kupunguza maumivu ya tumbo wakati wa ujauzito yanayohuisana na ligameti zinazoshikilia uterasi.

Lini niwasiliane na daktari au mkunga wangu

Wakati gani inakupasa upate wasiwasi kuhusu maumivu na mikakamo kama wewe ni mjamzito?

Hakikisha unawasiliana na daktari au mkunga wako anayesimamia maendeleo ya ujauzito ikiwa utapatwa na dalili zifuatazo:

  • Maumivu makali ya sehemu ya chini ya fumbatio katikati au pande zote, maumivu ambayo hayapungui (hata kama hayaambatani na kutoka damu)
  • Ongezeko la ghafla la kiu, inayoambatana na kupungua kwa kukojoa au kutokojoa kabisa siku nzima.
  • Maumivu makali ya kichwa yasiyoisha, mabadiliko katika kuona, kuvimba au ongezeko la uzito usioelezeka
  • Homa au kutetemeka
  • Kutokwa damu nzito au kutoka damu kunakoambatana na maumivu au maumivu makali chini ya fumbatio.
  • Kuharisha damu
  • Maumivu au kuungua wakati wa kukojoa, au kukojoa kwa shida au damu kwenye mkojo
  • Kubanana kuachia misuli ya uterasi zaidi ya mara nne ndani ya saa moja (haswa kama inatokea kabla ya wiki ya 37 ya ujauzito).

UJUMBE

Kumbuka kuna nafasi nzuri kwamba maumivu ya tumbo wakati wa ujauzito ni kawaida kabisa. Lakini ni busara kujua sababu kubwa zaidi ya mibano ya fumbatio na maumivu ya tumbo wakati wa ujauzito ili uweze kupata huduma ya matibabu ambayo unaweza kuhitaji.

IMEPITIWA: APRIL,2021.

Maambukizi ya Njia ya Mkojo (UTI) Wakati wa Ujauzito

UTI ni kifupi cha urinary tract infection au kwa lugha rahisi maambukizi katika njia ya mkojo, ambayo inajumuisha figo, ureta (mirija ya figo inayobeba mkojo kutoka kwenye figo mpaka kwenye kibofu), kibofu cha mkojo na urethra (mrija mfupi unaobeba mkojo kutoka kwenye kibofu mpaka nje ya mwili). Ogani zote hufanya kazi pamoja ili kuondoa uchafu kutoka kwenye damu. Kwanza figo husafisha damu na kugeuza uchafu kuwa mkojo. Halafu mkojo huteremka kwenda kwenye kibofu kwa msaada wa mirija ya figo-ureta ambapo hapo hutunzwa na baadaye kutolewa nje ya mwili kupitia mrija wa urethra.

Maambukizi haya yanasababishwa na bakteria. Mtu yeyote anaweza kuyapata. Mwanamke anaweza kupata maambukizi kwenye njia ya mkojo wakati wa ujauzito kuliko nyakati zingine zote. Ikiwa utahisi una UTI,ongea na daktari wako mapema. Kwa huduma na matibabu mazuri wewe na mtoto wako mtakuwa salama.

Mara nyingi maambukizi haya ushambulia zaidi kibofu cha mkojo na urethra. Lakini wakati mwingine yanaweza kupelekea maambukizi ya figo, maambukizi haya kwenye figo yanaweza pelekea mama kujifungua kabla ya muda au kujifungua mtoto mwenye uzito duni. Ndio maana ni muhimu kuchunguza dalili na ishara za maambukizi katika kila miadi ya kliniki kwa mjamzito.

Aina za Maambukizi Katika Njia ya Mkojo (UTI)

Cystitis or Bladder infection: Aina hii hutokea pale bakteria wanakusanyika kwenye kibofu cha mkojo na kusababisha uvimbe.

Maambukizi ya figo: bakteria wanaweza kupita kutoka kwenye kibofu cha mkojo kupitia mirija ya mkojo (ureter) na kuathiri figo moja au zote mbili, ugonjwa unaojulikana kama ‘pyelonephritis’. Ugonjwa huu unawaathiri sana wajawazito na huweza kusambaa kwenye damu. Madhara huwa makubwa kwa mama mjamzito na huweza kusababisha mtoto kuzaliwa njiti.

Asymptomatic bacteriuria: Mara nyingine bakteria katika njia ya mkojo hawaonyeshi dalili zozote.

Dalili za Maambukizi Katika Njia ya Mkojo (UTI)

Ikiwa una UTI, unaweza kuwa na dalili kama:

  • Kubanwa na mkojo haraka au kwenda kujisaidia haja ndogo kila mara
  • Shida wakati wa kukojoa
  • Kujisikia hali ya kuungua au maumivu sehemu ya chini ya misuli ya mgongo au tumbo la chini
  • Kujisikia hali ya kuungua kila unapojisaidia haja ndogo.
  • Mkojo kubadilika rangi au kuwa na harufu kali.
  • Maumivu wakati wa tendo la ndoa.
  • Damu kwenye mkojo, ambayo itaubadikisha rangi na kuwa pinki inayong’aa au rangi ya cocacola

Ikiwa una maambukizi ya figo unaweza ukawa na dalili kama:

  • Homa kali
  • Kichefuchefu
  • Kutapika
  • Maumivu ya sehemu ya juu ya mgongo, mara nyingi upande mmoja.

Kama una dalili za maambukizi ya figo, muone daktarin haraka katika kituo cha afya kilicho karibu na wewe. Bila matibabu sahihi, maambukizi haya yanaweza kuenea ndani ya mfumo wako wa damu na kusababisha hali za kutishia maisha.

Kwanini UTI Inatokea Mara kwa Mara Wakati wa Ujauzito

Homoni ni moja ya sababu. Kipindi cha ujauzito, homoni zinasababisha mabadiliko katika njia ya mkojo na kumfanya mwanamke awe katika hatari ya kupata maambukizi. Mabadiliko ya homoni yanapelekea hali ambayo mkojo unarudi kwenye kibofu cha mkojo kisha kwenye figo (vesicoureteral reflux), hali hii inaweza kusababisha UTI.

Ukiwa na ujauzito, mkojo wako una sukari zaidi, protini na homoni ndani yake. Mabadiliko haya pia yana kuweka katika hatari kubwa ya kupata UTI.

Kwasababu ya ujauzito, ukuaji wa uterasi unaoendelea kadiri ujauzito unavyokua hugandamiza kibofu cha mkojo. Hali hii inazuia mkojo wote ulio kwenye kibofu kutoka, mkojo unaobaki unaweza kuwa chanzo cha maambukizi.

Sababu/Chanzo cha UTI ni pamoja na:

“Escherichia coli” ni bakteria wanaotoka kwenye kinyesi chako: E.Coli ni chanzo kikubwa cha UTI na anaweza kuhama kutoka kwenye sehemu ya haja kubwa (mkundu) mpaka kwenye urethra ikiwa baada ya kujisaidia unajisafisha kuanzia nyuma kwenda mbele.

Shughuli zinazohusiana na tendo la ndoa. Vidole, uume wa mwenza wako, au vifaa vinavyotumika wakati wa tendo la ndoa vinaweza kusogeza bakteria karibu na urethra yako ku

“Group B streptococcus” baktari huyu anapatikana katika uke na utumbo mkubwa wa chakula, anaweza kusababisha UTI. Maambukizi haya yanaweza kupatiwa kwa watoto wachanga pia kutoka kwa mama zao. Katika wiki kati ya 36 mpaka 37 ya ujauzito daktarin atafanya kipimo kwa mama mjamzito kuchunguza aina hii ya bakteria. Ikiwa utapatikana na bakteria huyu, daktarin wako atakupatia dawa wakati wa kujifungua.

Jinsi Gani Maambukizi Katika Njia ya Mkojo Yanachunguzwa?

  • Kipimo cha mkojo kitachukuliwa. Inapendekezwa kupima mkojo wa kwanza wa asubuhi, ikiwa mkojo una chembechembe nyeupe za damu nyingi huashiria maambukizi.
  • Kipimo cha damu
  • Kipimo cha “urine culture” ni kipimo cha kugundua vijidudu vinavyoleta maambukizi kama vile bakteri kwenye mkojo. Sampuli ya mkojo huongezwa kwenye dutu ambayo inasababisa vijidudu kukua. Ikiwa hakuna vijidudu vinavyokua, basi kipimo ni (-ve), ikimaanisha hakuna bateria ndani ya mkojo. Uchunguzi huu ndio bora zaidi na unafaa kufanywa kabla ya kutumia dawa za antibayotiki.
  • Wakati mwingine kipimo cha Ultrasound hutumika kwa mgonjwa anayepata ugonjwa huu mara kwa mara.

Matibabu ya UTI Wakati wa Ujauzito

Utatumia dawa alizokuandika daktari kwa siku 3 mpaka 7. Ikiwa maambukizi yako yatakufanya ujisikie vibaya daktari wako anaweza kukuanzishia matibabu hata kabla majibu ya mkojo kutoka.

Dalili za UTI zinazokusumbua zitaanza kupotea siku ya tatu baada ya kuanza dozi. Tumia dawa zote ulizoandikiwa kwa wakati. Usiache kutumia dawa mapema hata kama dalili zimepotea.

Baadhi ya antibiotiki zinazotumika kutibu maambukizi ya njia mkojo ni pamoja na: amoxicillin, erythromycin na penicillin, dawa hizi ni salama kwa wanawake wajawazito. Daktari ataepuka kukuandikia dawa ambazo zinaweza kuathiri ukuaji wa mtoto ambazo ni pamoja na ciprofloxacin (Cipro), sulfamethoxazole, na tetracycline.

Matatizo Yanayoweza Kusababishwa na UTI Wakati wa Ujauzito

Maambukiz ya njia ya mkojo yanayoathiri figo yanajulikana kama “pyelonephritis”. Ikiwa wewe ni mjamzito aina hii ya maambukizi inaweza sababisha mambo yafuatayo:

  • Kujifungua kabla ya muda
  • Maambukizi makali
  • Anemia
  • Maambukizi ya mda mrefu ya njia ya mkojo (UTI sugu)

Nitajikingaje Dhidi ya Maambukizi Katika Njia ya Mkojo Wakati wa Ujauzito?

Ili kujaribu kuepuka UTI mambo yafuatayo hayana budi kufuatwa:

  • Kunywa maji ya kutosha angalau glasi 8 kwa siku. Maji huzimua mkojo na kusaidia kutoa bakteria kwenye kibofu cha mkojo kwa njia ya mkojo.
  • Ukimaliza kujisaidia jifute kuanzia mbele kurudi nyuma
  • Jisaidie haja ndogo kabla na baada ya kufanya tendo la ndoa na usisahau kujifuta sehemu za siri baada ya tendo la ndoa, ukianzia mbele kurudi nyuma. Pia inashauriwa kunywa glasi moja ya maji.
  • Epuka sabuni zenye marashi makali zinazoweza sababisha muwasho katika kusafisha sehemu zako za siri.
  • Kula vyakula vyenye vitamini C kama vile matunda(ubuyu, machungwa, machenza,nk)mkojo wenye asidi hupunguza bakteria
  • Vaa nguo za ndani zilizotengenezwa na pamba ili kuruhusu mzunguko wa hewa.
  • Usivae nguo za ndani zinazokubana
  • Jisaidie haja ndogo kila mara, angalau baada ya saa mbili au tatu. Usibane mkojo kwa muda mrefu, hali hii huwapa bakteria nafasi ya kukua
  • Epuka pombe, vyakula vyenye pilipili, kahawa na vyakula vyote vinavyoweza sababisa muwasho katika kibofu chako.

IMEPITIWA: APRIL 2021

Ninawezaje Kuongeza Nafasi ya Kupata Mtoto wa Kike au Kiume?

Je, moyo wako unafarijika kila uonapo nguo ya mtoto wa kike au kiume dukani au sokoni?

Hakika unapata furaha ndani ya moyo wako ndio maana upo kusoma makala yetu hii. Makala hii itakujuza vidokezo mbalimbali vinavyoweza kuongeza nafasi ya kupata ujauzito wa mtoto wa kike au kiume. Jambo la kwanza unalotakiwa kujua ni kwamba njia hizi za kujaribu kupata mtoto wa kike au kiume hazihakikishi kufanikiwa na pia hazithibitishwi na ushaidi wa kisayansi.  Njia pekee ya kukuhakikishia kupata mtoto wa jinsia unayotaka ni kutumia utaratibu maalumu unaohusisha kupandikiza kiinitete (kike au kiume) ndani ya uterasi ya mama, njia hii inajulikana kama “IVF- in vitro fertilization”. Njia hii ni gharama sana na sio halali kwa baadhi ya nchi.  Hivyo basi sio mbaya kujaribu baadhi ya mbinu hizi hata kama hazikupati uhakika asilimia 100 wa kupata mtoto wa jinsia unayotaka.

Ni muhimu kujua kuwa mbegu ya mwanaume ndiyo inayotoa uamuzi wa jinsia ya mtoto. Ijapokuwa mbinu mbalimbali zinashauri vitu ambavyo wanandoa wanaweza kufanya ili kupata mtoto wa kike au kiume,mwisho wa siku uteuzi wa jinsia ya mtoto una amuliwa na mbegu ya kiume itakayolifikia yai la mwanamke. Mara baada ya urutubishaji kutokea, jinsia ya mtoto huamuliwa.

Vifuatavyo ni vidokezo vitakavyokusaidia kuongeza nafasi ya kupata mtoto wa kike au kiume:

Matumizi ya njia ya “Shettles”

Ingawa hakuna data zinazoweza kuthibitisha ufanisi wa njia hii inayoitwa “the shettles” baadhi ya wanandoa wamekiri imewasaidia na wengine wameamua kujaribu njia hii. Nadharia inayotumika hapa ni kwamba mbegu ya kiume inayobeba jinsia ya kike (X) inasafiri taratibu lakini pia ina nguvu na inaishi mda mrefu ukilinganisha na mbegu ya kiume iliyobeba jinsia ya kiume (Y) ambazo zinasafiri haraka sana lakini zinaishi kwa muda mfupi. Hii inamaanisha kwa wanandoa wanaofanya tendo la ndoa siku mbili mpaka tatu kabla ya siku yai linapevuka ndani ya mwili wa mwanamke, wanaweza kuongeza nafasi ya kupata mtoto wa kike. Hii ni kwasababu mbegu za kiume zenye jinsia ya kike zinaweza kuishi mda mrefu hadi kipindi yai linapevuka, siku chache baadae zitakuwa bado zinaishi ndani ya mirija ya uzazi.

Lakini kama unataka kupata ujauzito wa mtoto wa kiume, wanandoa wanashuriwa kufanya tendo la ndoa siku moja kabla ya “ovulation” au siku yai linapevuka kujishindia nafasi ya mwanamke kubeba ujauzito wa mtoto wa kiume, kwasababu mbegu hizi zina kasi zaidi hivyo ni rahisi kulifikia yai haraka zaidi. Utafiti unaonyesha njia hii inaweza kuongeza nafasi ya kupata mtoto wa kike kwa asilimia 75, ijapokuwa hakuna utafiti wa kisayansi unaothi itisha iwapo njia hii inafanya au haifanyi kazi.

Matumizi ya njia ya “Whelan”

Njia hii ilianzishwa na Elizabeth Whelan. Njia hii inafanana na “shettles” kwani zote mbili zinaamini muda ni kitu muhimu katika kutafuta mtoto wa jinsia fulani. Nadharia inayotumika hapa inashauri ikiwa unataka kupata mtoto wa kike fanya tendo la ndoa siku 2 au tatu kabla ya yai kupevuka au siku ya ovulation kabisa. Wazo linatumika hapa kuunga mkono nadharia hii ni kwamba mbegu zenye kubeba jinsia ya kike na kiume zinafanya kazi tofauti katika kipindi tofauti ndani ya mzunguko wa hedhi wa mwanamke. Mbegu za kiume zenye kromosomu X zinaweza kurutubisha yai zaidi katika kipindi hichi cha mzunguko. Hivyo basi ikiwa utakutana kimwili na mwenza wako siku chache kabla ya “ovulation” au siku ya “ovulation” mbegu hizi zina nafasi kubwa ya kuishi. Kulingana na mvumbuzi wa nadharia hii- Elizabeth, kiwango cha kufanikiwa kupata mtoto wa kike kwa kutumia njia hii ni asilimia 57.

Njia hii ya Whelan inategemea wazo la kwamba mabadiliko ya dutu za kemikali ndani ya mwili wa mwanamke katika kipindi fulani ndani ya mzunguko wake yanafanya mbegu zilizobeba jinsia ya kiume “Y”kurutubisha yai, na wakati mwingine dutu za kikemikali kuruhusu mbegu zilizobeba jinsia ya kike “X” kurutubisha yai. Hivyo basi, ikiwa unatamani kupata mtoto wa kiume, dhana inasema, wanandoa wajitahidi kukutana kimwili siku nne mpaka sita kabla ya ovulation. Mbali na kuwa na rekodi za kuonyesha njia hii inafanya kazi, wakosoaji wanasema kufanya tendo la ndoa siku nne mpaka sita kabla ya yai kupevuka ni mbali sana na mara nyingi mbegu zilizobeba jinsia ya kiume haziishi mda mrefu.

Mikao wakati wa kujamiana

Zipo dhana nyingi kuhusu aina fulani ya mikao itakusaidia kupata mtoto wa kike au kiume, lakini ijulikane kwamba hakuna ushahidi wa kisayansi unaoonyesha hivyo, lakini pia hakuna madhara ikiwa wewe na mwenza wako mkajaribu. Mikao inayoruhusu uume kupenya kwa kina ndani ya uke (deep penetration),itasaidia kupata mtoto wa kiume wakati mikao ile isiyoruhusu upenyo wa kina inasaidia kupata ujauzito wa mtoto wa kike (shallow penetration). Kukusaidia kujua zaidi kuhusu mikao hii, soma makala yetu ya “mikao mizuri ya kujamiana ili kupata ujauzito haraka”.

Kufika kileleni “Orgasm”

Wataalamu wa mambo ya uchaguzi wa jinsia wanashauri ili kupata ujauzito wa mtoto wa kike mwanamke anatakiwa asifike kileleni. Mwanamke akifika kileleni anatoa alkali ambayo inasaidia mbegu zilizbeba jinsia ya kiume kuishi zaidi kwa kutengeneza mazingira yasiyohatarishi. Bila alkali hii inayotolewa pindi mwanamke amefika kileleni, mbegu zilizobeba jinsia ya kiume hushindwa kuishi na zina nafasi ndogo ya kufika kwenye yai lililotolewa na ovari tayari kwa kurutubishwa. Mwanamke akifika kileleni inaongeza nafasi ya kupata mtoto wa kiume.

Vidokezo vinginevyo ikiwa unajaribu kupata mtoto wa kike ni pamoja na:

  • Kutana na mwenza wako kimwili mara kwa mara
  • Punguza chumvi katika milo yako
  • Kula vyakula vyenye asidi nyingi (machungwa, machenza,n.k)na epuka vyakula vyenye alkali kama vile tango, tofaa, parachichi na almond. Mbegu za kiume zilizobeba jinsia ya kiume haziwezi kuishi katika mazingira yenye aside, hivyo kuongeza wingi wa aside mwili kupitia chakula kunasaidia kubadilisha kiwango cha Ph ya uke wako. Vilevile ikiwa mnatafuta mtoto wa kiume ulaji wa vyakula vyenye alkali ya kutosha utasaidia kuishi vizuri kwa mbegu zilizobeba jinsia ya kiiume.

Je, Vyakula Gani Vitaongeza Nafasi ya Kupata Mtoto wa Kike?

Vyakula vinavyofikiriwa kuongeza nafasi ya kupata mtoto wa kike ni pamoja na:

  • Maharagwe
  • Mboga za majani zenye kijani kilichokolea
  • Almond
  • Vyakula vya baharini hasa dagaa
  • Bidhaa za maziwa kama vile jibini, maziwa na mtindi
  • Bamia
  • Matunda jamii ya machungwa
  • Mayai
  • Karanga ya kusaga
  • Korosho
  • Mbegu kama mbegu za maboga na chia
  • Spinachi
  • Shayiri
  • Apple
  • Matunda kama strawberi,zabibu

Je, Vyakula Gani Vitaongeza Nafasi ya Kupata mtoto wa Kiume?

Vyakula vinavyofikiriwa kuongeza nafasi ya kupata mtoto wa kiume ni pamoja na:

  • Vyakula vyenye potasiamu ya kutosha kama vile ndizi, parachichi,uyoga,apple,almond, samaki aina ya salmon
  • Vyakula vyenye alkali ya kutosha kama vile machungwa, machenza,
  • Matunda freshi na mbogamboga
  • Nafaka ambazo hazijakobolewa
  • Epuka bidhaa za maziwa

Kumbuka

Kwa kadri unavyotamani kupata mtoto wa kike au kiume, ukweli ni kwamba hakuna njia inayoweza kuahidi matokeo unayotaka. Na ukweli ni kwamba, hakuna madhara katika kujaribu njia hizi – lakini utafiti zaidi unahitajika ili kujua ufanisi wa mapendekezo haya. Bila kujali kama utapata mtoto wa kike au kiume, jambo muhimu ni kuwa na ujauzito salama na kujifungua mtoto mwenye afya.

IMEPITIWA: APRILI 2021

Kutoka Kwa Mimba Changa (Miscarriage)

Kutoka kwa mimba changa ni nini?

Miscarriage au kutoka kwa mimba changa ni kupoteza ujauzito kabla haujafikia wiki ya 20. Jina la kitaalamu kwa upotevu huu wa ujamzito mchanga ni “Spontaneous abortion” ikimaanisha “upotevu mimba wa ghafla”.

Zaidi ya asilimia 80 ya upotevu mimba changa hutokea katika miezi mitatu ya mwanzo ya ujauzito. Upotevu wa mimba ni vigumu kutokea baada ya wiki 20 za mwanzo za ujauzito kupita. Na kama ikitokea madaktari huita hali hii kama upotevu mimba uliochelewa “Late miscarriage”.

Dalili za upotevu mimba changa

Dalili za “miscarriage” ni pamoja na:

  • Kutoka kwa damu inayoanza kutoka kidogo kidogo na kuendelea mpaka kuanza kutoka kwa wingi
  • Maumivu makali ya tumbo la kukata (cramps)
  • Maumivu ya tumbo
  • Uchovu
  • Maumivu ya mgongo yanayoongezeka
  • Homa inayoambatana na dalili zozote kati ya hizo hapo juu
  • Kupungua uzito
  • Kutoka uchafu mweupe wenye upinki ukeni
  • Kukaza kwa misuli ya nyonga (contractions)
  • Kutoka kwa vinyama nyama kama damu iliyoganda kutoka ukeni
  • Dalili dhoofu za ujauzito

Kama una dalili kati ya hizo hapo juu ni vyema kuhudhuria kituo cha afya kwa ushauri Zaidi. Watakuambia kama ni dalili za dharura au kufanyiwa vipimo kuchunguza ujauzito wako kwa ujumla.

Nini husababisha upotevu wa mimba changa kutokea?

Mara kwa mara kutoka kwa mimba changa hutokea pale mtoto anaekua tumboni akiwa na matatizo ya kigenetiki. Matatizo haya hayana uhusiano na mama.

Matatizo mengine yanayoweza kusababisha uwezekano wa kutoka kwa mimba changa ni kama:

  • Maambukizi
  • Matatizo ya kiafya kwa mama kama ugonjwa wa kisukari au matatizo ya thairoidi
  • Matatizo ya mfumo wa homoni
  • Matatizo katika uitikiaji kinga mwili (Immune response)
  • Matatizo ya kimaumbile kwa mama
  • Matatizo katika umbo la mfuko wa kizazi
  • Uvutaji wa sigara
  • Unywaji wa pombe
  • Matumizi ya madawa ya kulevya
  • Kuwa kwenye uwepo wa ukaribu na mionzi au viambata sumu

Mwanamke anakuwa kwenye uwezekano mkubwa wa kupoteza mimba ikiwa changa kama:

  1. Ana umri zaidi ya miaka 35
  2. Ana matatito mengine ya kiafya kama kisukari na matatizo ya kithairoidi
  3. Ameshawahi kupata kupoteza mimba changa mara tatu au zaidi

Udhoofu au kulegea kwa mlango wa mfuko wa uzazi (Cervical Insufficiency)

Kutoka kwa mimba ikiwa changa mara nyingine hutokea pale mama mjamzito anapokuwa na udhoofu au ulegevu wa mlango wa kizazi. Hii inamaanisha mlango wa kizazi hauwezi kuhimili ujauzito kikamilifu na hivyo kufunguka na ujauzito kutoka kabla ya muda wake. Mara nyingi aina hii ya upotevu wa ujauzito mchanga hutokea katika hatua ya pili ya ujauzito. Huwa kuna dalili chache sana kabla ya upotevu wa aina hii kutokea. Unaweza ukahisi mkandamizo wa ghafla, unaweza ukavunja chupa (maji mengi kutoka ukeni), na nyama nyama pamoja na kondo la nyuma la ujauzito kutoka ukeni bila ya kupata maumivu makali.

Madaktari kwenye nchi zilizoendelea hutibu aina hii ya upotevu mimba changa kwa kushona nyuzi kwenye mlango wa kizazi kwenye ujauzito wako utakaofuata. Hufanya hivi kwenye walau wiki ya 12 ya ujauzito. Nyuzi hizi zitasaidia kuufanya mlango wa kizazi uendelee kufungwa mpaka utakapokaribia kujifungua ndipo nyuzi hizi hutolewa na utajifungua kawaida.

Aina za kutoka kwa mimba changa

Kuna aina mbalimbali za upotevu mimba changa, kama:

Upotevu mimba changa hatarishi. Hii hutokea pale unapokuwa unatokwa na damu na kuna hali ya hatari kwa mama kupoteza ujauzito wake lakini mlango wa kizazi haujafunguka. Katika hali hii kama sababu za kutokwa kwa damu zitatatuliwa basi ujauzito huendelea bila matatizo.

Upotevu mimba changa usioepukika. Hapa mama mjamzito hutokwa na damu na pia anakuwa na maumivu ya tumbo mkazo (crampings), na pia mfuko wa kizazi umefunguka. Uwezekano wa kutoka kwa mimba changa kwenye hali hii ni wa hali ya juu sana.

Upotevu mimba changa usiokamilika. Baadhi ya nyama nyama kutoka kwa mtoto wako na sehemu ya kondo la nyuma na mfuko wa mimba vinatoka nje ya uke na baadhi vinabaki ndani ya uke.

Upotevu mimba changa uliokamilika. Ujauzito wote unatoka nje ya mwili wako. Kila kitu kinatoka, yaani, mtoto, mfuko wa mimba na kondo la nyuma. Aina hii mara nyingi hutokea kabla ya wiki ya 12 ya ujauzito kufika.

Upotevu mimba ulionusurika. Aina hii inahusisha kifo cha kiini cha mimba lakini nyama nyama za ujauzito husika zinabaki kwenye mfuko wa uzazi bila kutoka nje.

Upotevu mimba changa unaojirudia rudia. Aina hii inatambulika pale unapopoteza mimba zaidi ya tatu mfululizo ambazo hazikufikia umri wa zaidi ya wiki 12. Aina hii ya upotevu mimba changa hutokea kwa asilimia moja tu (1%) ya wenza wanaojaribu kupata mtoto.

Daktari atatambuaje kwamba una tatizo la upotevu mimba changa?

Kuhakikisha kwamba umepata upotevu mimba changa, daktari wako atafanya yafuatayo:

  • Uchunguzi wa mlango wako wa kizazi kuangalia kama umefunguka
  • Kipimo cha “ultrasound” Hapa atajaribu kuangalia maendeleo ya mtoto tumboni na kutafuta mapigo ya moyo ya mtoto. Kama itashindikana kupata jibu la moja kwa moja kipimo hiki kinaweza kurudiwa baada ya wiki moja.
  • Vipimo vya damu. Hapa daktari ataangalia uwepo wa homoni za ujauzito kwenye damu yako na kulinganisha kiwango cha homoni hizi na vipimo vilivyofanywa hapo awali. Pia ataangalia wingi wa damu kama umekuwa ukitokwa na damu nyingi ukeni.
  • Vipimo vya vinyama vinyama vilivyotoka ukeni pia huweza kufanyika kama vilikuwa vinatoka. Hii husaidia kuwa na uhakika kwamba umepata upotevu mimba changa na pia kuweza kutambua kama kuna matatizo mengine yanayosababisha kupatwa na tatizo hili.
  • Kipimo cha kromosomu (chromosome test). Kipimo hiki kinaweza kufanyika kama wewe na mwenza wako mmepoteza zaidi ya mimba changa mbili mfululizo. Daktari atachunguza kama mfumo wenu wa genetiki ndio unaosababisha upotevu huu.

Matibabu ya upotevu mimba changa

Asilimia 85% ya wanawake wanaopata upotevu mimba changa hufanikiwa kupata ujauzito salama na kujifungua salama baadae. Kupata upotevu mimba changa haimaanishi una tatizo la uwezo wa kupata watoto. Kwa upande mwingine, karibia asilimia 1 mpaka 2 ya wanawake hupata upotevu mimba changa unaojirudia rudia. Yani mara tatu au zaidi. Baadhi ya watafiti wanaihusisha hali hii na magonjwa ya ukinzani wa kinga mwili binafsi (autoimmune diseases)

Kama umepata upotevu mimba changa mara mbili mfululizo, ni vyema kuacha kujaribu kupata ujauzito, tumia uzazi wa mpango na wasiliana na mtaalamu wa afya ili waweze kutambua sababu ya upotevu wako wa mimba changa mfululizo.

Kama upotevu wako wa mimba changa ni uliokamilika na mfuko wa uzazi ni mtupu, inawezekana hautahitaji matibabu zaidi.

Wakati mwingine sio tishu zote na nyama nyama hutoka nje ya mfuko wa uzazi. Kama hili litatokea, daktari wako atafanya “Dilation and Curretage”. Haya ni matibabu ambayo itambidi daktari aupanue mlango wa uzazi na kutoa kila kitu kilichabaki kwenye mfuko wa uzazi kwa umakini. Pia kuna madawa ambayo ukitumia husaidia kutoa tishu zilizobaki kwenye mwili ziweze kutoka nje.

Baada ya utokaji wa damu kuisha unaweza ukaendelea na shughuli zako za kila siku. Kama mlango wako wa uzazi umefunguka lakini ujauzito bado upo salama daktari wako ataweza kufunga mlango wa kizazi kwa kuushona ili kuepusha ujauzito kutoka mpaka pale wakati wa kujifungua utakapofika.

Kama kundi la damu yako ni lile lenye Rh hasi (Rh-), daktari wako anaweza akakupa chembechembe tiba za damu ziitwazo (Rh Immune Globulin). Hizi husaidia kuepusha wewe kutengeneza kinga mwili (antibodies) ambazo zinaweza zikamdhuru mwanao au mimba zijazo.

Unaweza ukafanyiwa vipimo vya damu, vipimo vya genetiki au madawa kama umeshapata upotevu mimba changa mara mbili mfululizo. Kuweza kuhakikisha kwamba una upotevu mimba changa mfululizo (recurrent miscarriages) daktari wako atafanya vipimo vifuatavyo:

  • “Ultrasound” ya nyonga
  • Hysterosalpingogram (Hii ni X-ray ya mfuko wa uzazi na mirija ya uzazi kwa pamoja)
  • Hysteroscopy (Daktari wako atatumia mrija mrefu mwembaba wenye mwanga na kamera kuingia kwenye mfuko wako wa uzazi kuweza kuona kama una matatizo yoyote)

Dalili mbalimbali baada ya kupata upotevu mimba changa

Kutoka kwa damu na hali ya kujisikia vibaya ni dalili mojawapo baada ya kupata upotevu mimba changa. Kama utakuwa na kutoka kwa damu nyingi ikiambatana na homa, mwili kutetemeka na maumivu makali, hudhuria kituo cha afya haraka kwani hizi ni dalili za maambukizi.

Pamoja na dalili za kimwili unaweza pia ukawa unajihisi kuwa na hisia za huzuni, kujilaumu na pia kuwa na wasiwasi kuhusu mimba zitakazofuata. Unachojisikia ni kawaida na ni vyema kupitia hatua hii ya huzuni kuliko kuipotezea mbali na kuiacha ikusononeshe ndani kwa ndani.

Kama unaweza na hautajali, ni vyema kuliongelea swala hili na watu wako wa karibu kama mwenza wako, rafiki au mwanafamilia uliyemzoea. Vikundi vya wamama waliopoteza mimba kwenye jamii vinaweza kuwa na manufaa makubwa kwako na kwa mwenza wako. Pia muulize daktari wako kama kuna taarifa au ushauri wa ziada ambao anaweza kukupatia. Kumbuka kila mtu anapona na kuhuzunika na kurudia hali yake ya kawaida tofauti. Hivyo usikate tamaa.

Kupata mimba tena baada ya upotevu wa mimba changa

Unaweza ukapata ujauzito tena baada ya upotevu wa mimba changa. Zaidi ya 85% ya wanawake waliojaribu mara moja baada ya kupoteza mimba changa walipata ujauzito na kuendelea na kuja kujifungua salama. Kuwa na upotevu wa mimba changa haimaanishi kwamba una tatizo kwenye uwezo wako wa kupata mtoto. Hivyo hivyo asilimia 1 mpaka 2 ya wanawake wanaweza wakapata upotevu mimba changa unaojirudia rudia (mara tatu au zaidi).

Kama umepata upotevu mimba changa mara mbili mfululizo, ni vyema kuacha kujaribu kupata ujauzito, tumia uzazi wa mpango na wasiliana na mtaalamu wa afya ili waweze kutambua sababu ya upotevu wako wa mimba changa mfululizo.

Ni wakati gani ujaribu kupata ujauzito tena baada ya kupoteza mimba changa

Ni vyema kufanya mazungumzo haya na daktari wako. Wataalamu wengine wa afya wanasema ni vyema kusubiria kwa muda fulani kabla ya kupata ujauzito mwingine. Muda kati ya mzungumko mmoja wa hedhi mpaka miezi mitatu kabla ya kufikiri kujaribu tena kupata ujauzito. Kuzuia upotevu mwingine wa mimba changa daktari wako anaweza kukupa matibabu kutumia “Progesterone”, homoni inayosaidia kiini mimba kujishika kwenye mfuko wa uzazi na kusaidia maendeleo yake kwenye hatua za mwanzo za ujauzito.

Kuchukua muda kupona kimwili na kiakili ni muhimu pia baada ya kupoteza mimba changa. Ni vyema kutokujilaumu na kujiona mwenye makosa. Hakikisha unapata msaada wa kimawazo na ushauri kujitayarisha na kuwa tayari pale utakapoweza kujaribu tena.

Je, utazuiaje kutokea kwa upotevu mimba changa?

Upotevu mimba changa mara nyingi hutokea kwa sababu kuna tatizo kwenye ujauzito husika. Huwezi kuzuia hili. Kama daktari wako atakupima na kuona tatizo, aina mbalimbali za matibabu zinapatikana.

Kama una ugonjwa, kuutibu ugonjwa husika kutaongeza uwezekano wa kupata ujauzito ulio salama na kujifungua bila matatizo. Njia bora unayoweza kuchukua mwenyewe ni kuhakikisha unakuwa mwenye afya kadiri uwezavyo kabla ya kujaribu kupata ujauzito:

  • Fanya mazoezi ya mara kwa mara
  • Kula mlo kamili na wenye afya
  • Zingatia kuwa kwenye uzito wako kiafya
  • Epuka maambukizi
  • Usivute, kunywa pombe au kutumia madawa ya kulevya
  • Punguza utumiaji mkubwa wa “caffeine” kama kahawa.

IMEPITIWA: MARCH 2021

Vidokezo vya Urembo Kipindi cha Ujauzito

Ni vipi nitaonekana mrembo kipindi cha ujauzito ni swali wanalokuja nalo wakina mama wengi. Kuna njia kumi sahihi za kukusaidia kufurahia urembo wako hasa katika kipindi maalumu maishani mwako.

  1. Kunywa maji

Kipindi cha ujauzito unahitajika kupata maji mengi kwa siku. Yatakusaidia kusafisha na kutoa taka na sumu mwilini mwako. Zaidi maji yanasaidia kutunza kiasi cha kimiminika kinachotakiwa mwilini mwako. Maji ni muhimu zaidi kwa afya yako na mwanao. Kunywa angalau lita 2 za maji kwa siku.

  1. Mlo sahihi

Unahitaji uangalizi na umakini wa ziada katika chakula unachokula wakati wa ujauzito na afya yako. Inashauriwa kumuhusisha daktari wako kukuandalia ratiba ya aina ya chakula unachotakiwa kula. Fuatilia ratiba hii kwa umakini, kula kwa afya, ikiwa pia ni muhimu kwa ajili ya mtoto wako.

  1. Pata muda wa kulala

Uchovu ni dalili moja wapo anazopata mama mjamzito hasa katika kipindi cha mwanzo. Kupumzika vizuri ni muhimu kwa ajili ya mwili na akili yako mwenyewe. Hakikisha unapata muda mzuri na wa kutosha kupumzika kiasi kwamba mwili wako uwe unahisi uchovu kidogo. Jiweke huru wakati wa kulala. Pumzika kwa usahihi, unaweza kutaka kutumia mito au kitu kingine cha kukuweka huru unapolala.

  1. Uzito sahihi

Unahitajika kuangalia uzito wako kipindi cha ujauzito. Baadhi ya wakina mama wanakula chochote na kila kitu pasipo kuhofia kuhusu uzito. Ikiwa ni kawaida kuongezeka uzito wakati wa ujauzito, si vema kiafya kuongezeka katika njia tofauti. Uzito unaongezeka kwa kula vyakula ambavyo havina msaada mwilini, mara kwa mara kula mlo sahihi, unaweza kumuhusisha daktari wako kwa machaguo bora.

  1. Mazoezi

Ndio, ni muhimu! Kuna mazoezi maalumu kwa ajili ya wajawazito. Hudhuria darasa la mazoezi ya yoga yaliyoandaliwa kwa ajili ya wajawazito, pata muda wa kukutana na wajawazito wengine na kujifunza na kupata uzoefu. Unaweza pia kumuomba ushauri daktari ni michezo gani unaweza kushiriki.

  1. Epuka michirizi

Wakina mama wengi wanalalamika kupata michirizi baada ya kujifungua. Unahitaji kuchukulia uangalizi hili wakati wa ujauzito.  Tumia cream uliyoshauriwa au zinazouzwa kwa ajili ya kuondoa michirizi. Tumia kila siku kuukanda mwili wako. Unaweza pia kutaka kuepuka kukimbia, kuruka au kugonga kama njia ya kuepuka michirizi.

  1. Thamini umbo lako

Pindi unatoka katika matembezi vaa nguo ya kuonyesha umbo lako, umbo la mwanamke ni zuri wakati wa ujauzito, ujauzito unamuongezea hipsi mwanamke. Tumia nafasi hii kuvaa nguo za kushika mwili wako vizuri ili kuonyesha vema hipsi zako.

  1. Uangalizi wa ngozi

Pamoja na yote wakati wa ujauzito, usisahau ngozi yako. Urembo katika kipindi cha ujauzito ikiwemo urembo wa ngozi, kwa kupendelea mimea tiba katika kipindi sahihi. Kutokana na mabadiliko ya homoni kunaweza kuwa na athari kidogo katika ngozi yako. Unaeza kutumia bidhaa za kulinda ngozi kwa kuzingatia aina ya ngozi yako lakini hakikisha hutumii kemikali hatarishi.

  1. Make-Up

Mwanamke hachukizwi na make up! kutokana na mabadiliko ya homoni unaweza kupata madoa usoni hivyo poda ni mkombozi. Make up ndio mkombozi, tena angalia zile ambazo hazitumii kemikali kali.

  1. Pumzika

Mwisho na muhimu zaidi ni kukumbuka kupumzika, weka mapumziko katika ratiba yako. Lala chini kwa muda unapopata nafasi. Pumzisha mwili wako. Ujauzito unaweza kuja na stress sana lakini hakikisha hazikushindi, jinsi unavozidi kupumzika ndivo jinsi unaonekana mrembo.

IMEPITIWA: JUNI 2020

Zifahamu chanjo sahihi. Je, Mtoto wako anazipata kwa wakati?

Chanjo ni nini?

Chanjo huokoa maisha ya hadi watoto milioni 3 kila mwaka. Chanjo hukinga maradhi, ulemavu na vifo vitokanavyo na magonjwa yanayozuilika kwa chanjo ikiwa ni pamoja na surua, homa ya ini (hepatitisi B), dondakoo, kifaduro, nimonia, polio, kuhara kunakosababishwa na virusi vya rota, rubela na pepopunda.
Kisayansi chanjo ni kitendo cha kupewa kinga mwili kwa njia ya kuamsha vitoa kinga viwe tayari kupambana na adui ambaye wanamjua tayari.

Umuhimu wa chanjo

Watoto waliopata chanjo huwa wamekingwa dhidi ya magonjwa hatari, ambayo kwa kawaida huweza kusababisha ulemavu au kifo. Watoto wote wana haki ya kupata kinga hii. Kinga ya utotoni ni muhimu sana hasa kwa ukuaji wa baadae. Hivyo basi, chanjo kwa mtoto katika mwaka wake wa kwanza na katika mwaka wa pili ni muhimu sana.
Ni muhimu pia, kina mama wajawazito kupata chanjo ya pepopunda ili kujikinga wao wenyewe na watoto wao wanaozaliwa. Wazazi na walezi wengine wanapaswa kufahamu sababu za umuhimu wa chanjo, ratiba ya chanjo inayotumika na mahali chanjo inakotolewa kwa watoto.
Wazazi na walezi wengine wanapaswa kufahamu kuwa kutoa chanjo kwa mtoto mgonjwa kidogo au mwenye ulemavu au mwenye upungufu wa lishe ni salama.

Ukweli kwa ajili ya familia na jamii kuhusu chanjo

1. Chanjo ni jambo la lazima. Kila mtoto ni lazima apate chanjo zote zilizopendekezwa. Kinga ya utotoni ni muhimu sana; chanjo katika mwaka wa kwanza na wa pili zina umuhimu wa pekee. Wazazi wote au walezi wengine wanapaswa kuzingatia ushauri wa mtaalamu wa afya kuhusu muda wa kukamilisha chanjo zinazohitajika.

2. Chanjo hutoa kinga dhidi ya magonjwa mengi hatarishi. Mtoto ambaye hajapata chanjo yuko katika hatari kubwa ya kupatwa na maradhi, ulemavu wa kudumu au hata kupoteza maisha.

3. Mama wote wajawazito pamoja na watoto wao wanapaswa kukingwa dhidi ya pepopunda. Hata kama mama aliwahi kupata chanjo kabla , anapaswa kupata ushauri wa mtaalamu wa afya kuhusu kama bado anahitaji kupewa chanjo ya pepopunda.

4. Sindano mpya hazina budi kutumika kwa kila mtu anayepata chanjo. Kila mtu anapaswa kudai sindano mpya kwa kila chanjo anayopewa.

5. Ugonjwa huweza kuenea haraka watu wengi wanapokuwa wamekusanyika pamoja. Watoto wote wanaoishi katika maeneo yenye mkusanyiko mkubwa , hasa katika mazingira ya wakimbizi au ya watu waliojikusanya kutokana na janga fulani, wanapaswa kupewa chanjo haraka.

6. Kadi ya chanjo ya mtoto (au ya mtu mzima) haina budi kuwasilishwa kwa mtoa chanjo kabla ya kutolewa kwa chanjo.

Aina za chanjo

BCG (Bacile Calmette-Guérin)
Watoto wote wanastahili kupokea chanjo itwayo BCG (Bacile Calmette-Guérin) vaccine. Hii huumpa mtoto kinga dhidi ya aina zingine za kifua kikuu na ukoma.

DTP au DPT (Dondakoo, Pepopunda na Kifaduro)
Watoto wote wanastahili chanjo dhidi ya dondakoo, pepopunda na kifaduro kupitia aina ya chanjo iitwayo DTP au DPT vaccine. Viini vya dondakoo husababisha maambukizi ya njia ya kuingizia hewa na huenda ikasababisha shida za kupumua na hata kifo. Pepopunda nayo husababisha kukauka kwa misuli na maumivu makali yanayo sababishwa na mkazo wa misuli. Mkazo huo wa misuli unaweza sababisha kifo. Kifaduro huathiri njia ya kuigizia hewa na kusababisha kikohozi kinachoweza dumu wiki nne hadi nane na ni hatari sana kwa watoto wachanga.

Wanawake wote waja wazito na watoto wachanga wanahitaji chanjo ya pepopunda.

Surua
Watoto wote wanastahili kupokea chanjo dhidi ya surua. Maradhi ya surua husababisha utapiamlo, udhaifu wa maendeleo ya ubongo na huweza kufanya mtoto kiziwi au kipofu. Ishara zinazoelekeza kuwa mtoto anaweza kuwa anaugua surua ni pamoja na kuongezeka kwa joto mwilini, upele, kikohozi, kumwaga kamasi na macho kubadilika na kuwa mekundu. Tahadhari, mtoto anaweza kufa kutokana na surua.

Polio
Watoto wote wanastahili chanjo dhidi ya polio. Dalili za polio ni utepe kwenye mguu au mkono na udhaifu wa kukitumia kiungo kilicho athirika. Kwa kila watoto mia mbili wanaoambukizwa maradhi ya polio, mmoja atapata ulemavu wa maisha.

Ratiba za chanjo hutofautiana kulingana na nchi au sehemu ya nchi unayoishi. Ni muhimu kufuatilia ratiba ya chanjo kwa mujibu wa mwongozo wa taifa. Watoto wanastahili kupokea chanjo kwa umri unaostahili na kwa muda unaostahili.
Pamoja na kutofautiana huku kwa ratiba za chanjo kati ya nchi na nchi, unaweza kufuatilia utaratibu uliopendekezwa na CDC (Centre for Disease Control) hapa chini.

Ufuatao ni mtiririko wa chanjo husika na wakati muafaka ambao mtoto wako anatakiwa awe ameshapatiwa.

UMRIAINA YA CHANJOINATOLEWAJEMUHIMU KUJUA
0 – AnapozaliwaKifua Kikuu (BCG)  Sindano bega la kulia  Ni lazima kovu lotokee kwenye bega la kulia baada ya muda  
 Polio (OPV 0)Matone mdomoniChanjo ya ugonjwa wa kupooza ya kuanzia
    
Wiki ya 6Polio (OPV 1)Matone mdomoniChanjo ya kwanza ya ugonjwa wa kupooza
 DTB-HepB-Hib1 (Dondakoo, Kifaduro, Pepopunda na Hepatiti B)Sindano paja la kushotoChanjo ya kwanza ya Dondakoo, Kifaduro, Pepopunda na Hepatiti B kwa pamoja.
 PCV 1Sindano paja la kuliaChanjo ya Nimonia ya kwanza
 Rota 1Matone mdomoniChanjo ya Kuhara ya kwanza
    
Wiki ya 10Polio (OPV 2)Matone mdomoniChanjo ya pili ya ugonjwa wa kupooza
 DTB-HepB-Hib2 (Dondakoo, Kifaduro, Pepopunda na Hepatiti B)Sindano paja la kushotoChanjo ya pili ya Dondakoo, Kifaduro, Pepopunda na Hepatiti B kwa pamoja.
 PCV 2Sindano paja la kuliaChanjo ya Nimonia ya pili
 Rota 2Matone mdomoniChanjo ya kuhara ya pili
    
Wiki ya 14Polio (OPV 3)Matone mdomoniChanjo ya mwisho ya ugonjwa wa kupooza
 DTB-HepB-Hib3 (Dondakoo, Kifaduro, Pepopunda na Hepatiti B)Sindano paja la kushotoChanjo ya tatu ya Dondakoo, Kifaduro, Pepopunda na Hepatiti B kwa pamoja.
 PCV 3Sindano paja la kuliaChanjo ya Nimonia ya tatu
    
Miezi 9Measles (MR 1)Sindano bega la kushotoChanjo ya kwanza ya surua
    
Miezi 15Measles (MR 2)Sindano bega la kushotoChanjo ya pili ya surua

IMEPITIWA: 26 MAY 2020

Kipimo cha Ultrasound Kipindi cha Ujauzito

Kipimo cha Ultrasound ni Nini?

Kipimo cha ultrasound ni uchunguzi unaotolewa kwa wajawazito wengi kabla ya kujifungua. Kinatumia mawimbi ya sauti kuonyesha picha ya mtoto aliyeko tumboni. Kipimo hichi kinamsaidia mtoa huduma kuangalia afya na ukuaji wa mtoto aliye tumboni.

Kipimo cha ultrasound kinamsaidia daktari kuona kama kuna tatizo katika ogani, mishipa na tishu bila kufanya upasuaji. Tofauti na tekinolojia nyingine, ultrasound haitumi mionzi, ndio maana ni njia inayopendekezwa kwaajili ya kuangalia ukuaji wa kijusi kipindi cha ujauzito. Wakati wa kufanya kipimo cha ultrasound ni muhimu sana kwa wajawazito wengi- ni mara ya kwanza unapoweza kumuona mtoto wako. Unaweza kuona mikono, miguu na sehemu nyingine za mwili kulingana na lini kipimo kitachukuliwa na mkao wa mtoto wako tumboni. Utaweza pia kujua jinsia ya mtoto wako.

Wanawake wemgi wanafanya kipimo cha ultrasound katika kipindi cha pili cha miezi mitatu ya ujauzito (second trimester) wiki 18-20 ya ujauzito. Baadhi wanafanya katika kipindi cha kwanza cha miezi mitatu ya ujauzito (kabla ya wiki ya 14 ya ujauzito). Idadi ya vipimo vya utrasound na muda unaweza tofautiana kwa wanawake wenye aina fulani ya matatizo ya kiafya kama asthma na kisukari.

Kuna Tofauti Gani Kati ya Kipimo cha Ultrasound na X-ray?

Ultrasound inatumia mawimbi ya sauti na mwangwi kutoa picha hai, kama video.

X-rays ni njia rahisi na haraka kwa mtaalamu wa afya kutumia kuona viungo vya ndani ya mwili na hali ya mifupa. X-rays zinatumia mionzi kupiga picha ya ogani za ndani ya mwili, na mionzi hiyo ina madhara makubwa kwa afya ya binadamu. Picha zinazopigwa zinafanana na kivuli cha mwili wa ndani wa binadamu.

Kwanini kipimo cha Ultrsound Kinafanyika?

Vipimo hivi vitampatia mama mtarajiwa nafasi ya kumuona mtoto wake ambaye hajazaliwa. Lakini pia kipimo hichi kina kazi nyingine.

Daktari wako atakutaka ufanye kipimo hich kama utakua na maumivu, kuvimba au dalili nyingine itakayo hitaji uchunguzi wa ogani za ndani ya mwili. Ultrasound inaweza kuangalia sehemu za mwili kama vile: kibofu cha mkojo, ubongo (wa mtoto), macho, figo, ini, ovari, bandama, uterasi, korodani, na mishipa ya damu.

Je, Kuna Aina Tofauti za Vipimo vya Ultrasound?

Ndio. Aina ya kipimo inategemea na uchunguzi anaoufanya daktari na ujauzito wako una umri gani. Ultrasound zote zinatumia kifaa kinachoitwa ‘transducer’ kinachotumia mawimbi ya sauti kutengeneza picha ya mtoto wako kwenye kompyuta. Aina kuu mbili za ultrasound ni:

‘Transabdominal ultrasound’: aina hii inafanyika sana kipindi cha ujauzito, mama mjamzito hulala juu ya kitanda kwa mgongo kisha mhudumu wa afya atapaka kimiminika maalumu ‘gel’ juu ya tumbo lako kusaidia mawimbi ya sauti kutembea kwa urahisi na kupata picha nzuri. Baada ya kukupa ‘gel’ atatumia ‘transducer’ kupapasa juu ya tumbo lako. Masaa mawili kabla ya kufanya kipimo hichi ni vizuri kunywa maji glasi kadhaa ili kibofu kiwe kimejaa wakati wa zoezi hili. Kibofu kilichojaa kinasaidia mawimbi ya sauti kutembea kwa urahisi zaidi na kupata picha nzuri. Aina hii ya ultrasound itachukua dakika 20.

‘Trasvaginal ultrasound’: aina hii inafanyika kupitia ukeni (njia ya uzazi). Utalala juu ya kitanda kwa mgongo na kupanua miguu yako. Mtoa huduma ataingiza kwenye uke wako ‘transduce’ nyembemba yenye muonekano kama kijifimbo cha kiongozi wa muziki. Utasikia msuguano kutoka kwenye ‘transducer’ bila maumivu. Katika aina hii ya ultrasound kibofu chako si lazima kijae, itachukua dakika 20.

Mtoa huduma anaweza kutumia aina nyingine za ultrasound kupata taarifa zaidi lakini mara nyingi ni kwa jambo muhimu:

‘Doppler ultrasound’: aina hii inatumika kuangalia usambazaji wa damu kwa mtoto wako ikiwa sio mzuri. ‘Transducer’ itatumika kusikiliza mapigo ya moyo ya mtoto wako na kupima usambaaji wa damu kwenye kitovu cha kichanga na baadhi ya mishipa ya damu ya mtoto wako. Matumizi ya aina hii ya ultrasound yanatumika kuangalia kama una aina fulani ya ugonjwa wa damu (Rh disease) ambao unaleta matatizo makubwa kwa mtoto kama hautatibiwa. Kipimo hichi kinaweza kufanyika miezi mitatu ya mwisho ya ujauzito, lakini kinaweza kufanyika mapema zaidi.

‘3-D ultrasound’: kinachukua picha elfu moja kwa wakati mmoja, inaweza chukua picha ya kuonekana vizuri kama picha za kawaida. Kipimo hichi kinatumika kuhakikisha ogani za mtoto zinakua na kuendelea vizuri. Kinaangalia kasoro katika uso wa mtoto na matatizo katika mfuko wa uzazi.

‘4-D ultasound’: ni sawa na 3-D, ila hiki kinaonyesha mwondoko wa mtoto wako katika video.

Maandalizi ya Kufanya Kipimo cha Ultrasound Kipindi cha Ujauzito

Kabla ya kufanya kipimo hichi, utaambiwa unywe maji mengi na kubana mkojo wako kwa kipindi fulani ili kibofu chako kiwe kimejaa mda wa uchunguzi. Hii ni muhimu kwa vipimo vya ujauzito mchanga, kibofu kilichojaa kinasukuma mfuko wa uzazi juu ili picha za mtoto zipatikane kwa urahisi zaidi.

Mtoa huduma au daktari atakayeshughulikia suala zima la kufanya kipimo cha ultrasound atakupa maelekezo ya mda gani kabla ya kipimo unywe maji na kiasi gani cha maji unywe.

Kwa kawaida ultrasound hazina maumivu. Unaweza kuona usumbufu wakati kibofu chako kimejaa au wakati wanafanya ‘transvaginal ultrasound’.

Nini Kinatokea Wakati wa Ultrasound?

Wakati wa ultrasound utapakwa kimiminika maalumu ‘gel’ kwenye tumbo lako na kifaa maalumu kinachotoa na kupokea mawimbi ya sauti ‘transducer’ kitapitishwa juu ya Ngozi yako. Mawimbi ya sauti yanatua juu yam too na maeneo mengine ndani ya mwili, kutengeneza picha kwenye skrini ya TV.

Ultrasound zinazofanyika mimba ikiwa change zinatakiwa kufanyika kwa njia ya uke ‘transvaginally’. Hii ina maanisha badala ya kutumia ‘transducer’ juu ya ngozi ya tumbo la chini, kifaa chembamba kitaingizwa taratibu ukeni na kuchuka picha za mtoto.

Mtaalamu wa huduma hii anaweza kukuonyesha baadhi ya picha za mtoto wako kwenye skrini na kutoa kopi baadhi kwaajili yako. Picha hizi zitaangaliwa pia na mkunga wako.

Je, Unahitaji Kufanya Kipimo cha Ultrasound Mara Ngapi Kipindi cha Ujauzito?

Ikumbukwe kuwa itakuwa ngumu kuona chochote katika wiki chache za kwanza za ujauzito, ila kijusi kitaanza kuonekana zaidi wiki ya 13.

Wanawake wengi wanajiuliza mara ngapi anatakiwa kufanya kipimo cha ultrasound? Inatofautiana kulingana na mama na ujauzito wake, zifuatazo ni baadhi ya vipimo vya ultrasound unavyoweza kutarajia:

Miezi mitatu ya kwanza ya ujauzito

Kipimo cha kwanza kinaweza kufanyika kati ya wiki ya 6 mpaka ya 8. Lakini baadhi ya madaktari wanafanya kipimo hichi kama uko katika hali hatari ya ujauzito. Hali hizi ni pamoja na maumivu ya tumbo la chini, kutoka damu na historia yoyote ya kasoro baada ya kuzaliwa mtoto au mimba kuharibika.

Kipimo kingine (dating scan) kinashauriwa kufanyika kwa wanawake wajawazito wasio na uhakika wa umri wa ujauzito wao na lini wanatarajiwa kujifungua, hii inasababishwa na uwepo wa mzunguko wa hedhi usio wa kawaida. Majibu ya kipimo cha ultrasound yatasaidia kuthibitisha umri wa ujauzito na kumpatia mama rekodi za uhakika. Vilevile matokeo ya kipimo hichi yanaweza kumuonyesha kama mama ana ujauzito wa mtoto mmoja au mapacha. Kipimo hichi kinaweza kufanyika kuanzia wiki ya 10-13 ya ujauzito.

Ndani ya kipindi hichi cha miezi mitatu ya kwanza ya ujauzito kipimo kingine cha ultrasound (nuchal translucency scan) kinafanyika kwa wajawazito kati ya wiki 14-20 ya ujauzito. Kipimo hiki kinafanyika pamoja na kipimo cha damu kwa nia ya kutambua kama mtoto yuko na hatari ya kuwa kasoro za maumbile (down syndrome). Kama majibu yataonyesha kuna hatari zaidi vipimo vingine vitafanyika zaidi.

Miezi mitatu ya pili ya ujauzito

Wiki ya 18 mpaka 20 kipimo cha ultrasound kinashauriwa kufanyika ili kuangalia ukuaji wa mtoto. Vipimo tofauti vitafanyika kuangalia ukuaji na maendeleo yam toto. Kijusi kitatathminiwa kama kina aina yeyote ya kasoro katika kichwa, miguu, moyo na ogani nyingine ndani ya mwili.

Katika hatua hii ya ujauzito jinsia ya mtoto inaweza kugunduliwa. Inaweza kuwa vigumu kuona sehemu za siri za mtoto ikiwa mtoto amekaa vibaya tumboni.

Uchunguzi wa mlango wa uzazi, kiasi cha uoevu wa amnion (amniotic fluid) na nafasi ya placenta katika mfuko wa uzazi utafanyika .

Miezi mitatu ya mwisho ya ujauzito

Kipimo cha ultrasound baada ya wiki ya 35 ni salama zaidi na cha uhakika zaidi kukuhakikishia kuwa mtoto wako anakua kawaida.

Lakini pia, ikiwa ujauzito wako uko katika hatari kubwa kwa mfano kama una shinikizo kubwa la damu, kisukari, unatoka damu, kiasi kidogo cha uoevu wa amnion, una dalili za kujifungua kabla ya wakati, umri zaidi ya miaka 35, daktari anaweza kufanya kipimo cha ultrasound ili kuhakikisha afya ya mama na mtoto ni nzuri. Kipimo cha ultrasound wakati huu kitasaidia kutathmini kama mtoto amekaa mkao unaotakiwa tumboni au amegeuka. Na njia gani ya kujifungua itumike kama mtoto amegeuka.

Licha ya hayo, kipimo cha ultrasound katika kipindi hiki hakiwezi onyesha siku ya uhakika ya kujifungua na uzito wa mtoto.

Kumbuka:

Inapendekezwa kwa wanawake wenye ujauzito wa mtoto zaidi ya mmoja au wanapatwa na kutoka damu ukeni mara kadhaa kufanya kipimo cha ultrasound mara kwa mara.

Sababu / Faida za Kufanya vipimo vya Ultrasound Kipindi cha Ujauzito

  • Kuthibitisha ujauzito.
  • Kuangalia kama una mtoto zaidi ya mmoja.
  • Kuweka tarehe ya kujifungua kwa kuangalia umri na ukuaji wa mtoto.
  • Kuangalia mapigo ya moyo ya mtoto, hali ya misuli, mwondoko na ukuaji kwa ujumla.
  • Kupima ovari na mfuko wa ujauzito.
  • Kufuatilia ujauzito uliotungika nje ya mfuko wa uzazi.
  • Kutathmini hatari za mtoto aliyepatikana na kasoro za maumbile kama ugonjwa wa ‘down sydrome’
  • Kuangalia ukuaji wa kimwili wa mtoto na kuangalia kama anakua ipasavyo.
  • Kuangalia kiasi cha uoevu wa amioni (amniotic fluid) kinachomzunguka mtoto katika mfuko wa uzazi.
  • Kutambua nafasi ya plasenta.
  • Kuangalia mkao wa mtoto kabla ya kujifungua.

Hasara za kufanya kipimo cha ultrasound

Ultrasound ni salama kwako na kwa mtoto ikiwa itafanywa vizuri na mtoa huduma mwenye ujuzi nayo. Ultrasound ni kipimo salama zaidi kuliko X-rays kwasababu kinatumia mawimbi ya sauti badala ya mionzi.

Kama ilivyo kama vipimo vingine, kipimo cha ultrasound hakiwezi kuona kila tatizo. Wakati mwingine kinakosea kugundua baadhi ya kasoro.

IMEPITIWA: 28 APRILI 2020.

Vidokezo Vitakavyomsaidia Mama Kupona Haraka Baada ya Kujifungua kwa Njia ya Upasuaji.

Kujifungua salama ni muda wa furaha sana. Ni wakati unaofanikiwa kukutana na mtoto aliyekuwa anakua ndani yako kwa kipindi cha miezi tisa. Lakini pia kujifungua inaweza kukugharimu, hususa kama umejifungua kwa njia ya upasuaji. Itakuchukua mda mrefu kupona kuliko aliyejifungua kwa njia ya kawaida.

Ufuatao ni ushauri utakao kumsaidia mama aliyejifungua kwa njia ya upasuaji kupona haraka, ili upate muda wa kutosha kumjua na kumlea mtoto wako mchanga.

Pata Mapumziko ya Kutosha.

Kujifungua kwa njia ya upasuaji ni upasuaji mkubwa. Kama ilivyo upasuaji mwingine, mwili wako unahitaji mda wa kupona baada ya hapo. Tegemea kubaki hospitali kwa siku tatu mpaka nne baada ya kujifungua (au zaidi ya hapo kama kulitokea tatizo lingine la kiafya), kisha upe mwili wako wiki sita kupona kabisa.

Ni rahisi kusema zaidi ya kutenda. Ni vigumu kwenda kulala kwa masaa kadhaa huku una mtoto anayehitaji uangalifu mwingi kutoka kwako.

Huenda umesikia ushauri huu wa “lala kila mtoto wako akilala” kwa marafiki na ndugu zako wa karibu. Wako sahihi. Jaribu kulala kila mtoto anapolala. Omba msaada wa kubadilisha nepi na kazi mbalimbali za nyumbani kwa rafiki na ndugu zako wa karibu ili upate muda wa kupumzika kidogo pale inapowezekana. Dakika chache za kupumzika hapa na pale katikati ya siku zinasaidia.

Uangalie Mwili Wako

Kuwa makini zaidi kila unachofanya huku ukiendelea kupona. Epuka kupanda na kushuka ngazi kadiri uwezavyo. Weka mahitaji muhimu ya mtoto na wewe (chakula, nepi, kanga,nguo zako na mtoto) karibu na wewe ili usiamke kila mara.

Usinyanyue kitu chochote kizito zaidi ya mtoto wako. Omba msaada kwa mpenzi/mme wako au rafiki au ndugu yako.

Ni vizuri ukashika sehemu ya kidonda kila unapokohoa au kupiga chafya.

Inaweza kukuchukua mpaka wiki nane kurudia ratiba zako za kwaida. Ni vizuri kumuuliza daktarin wako lini inafaa wewe kufanya mazoezi tena, kurudi kazini na kuendesha gari. Pia subiria mpaka daktari atakapo kuruhusu kujamiana tena.

Epuka mazoezi mazito, ila unaweza kufanya mazoezi mepesi kama kutembea taratibu kila unapoweza. Mzunguko huu utasaidia mwili wako kupona na kuzuia tatizo la kukosa choo na damu kuganda. Pia kutembea ni moja ya njia ya kumtambulisha mtoto katika ulimwengu.

Kama unavyoangalia afya yako ya mwili usisahau hali ya hisia zako. Kuwa na mtoto inaleta hisia ambazo hujawahi kutarajia. Kama ukisikia kuchoka,huzuni au kuvunjika moyo usizipuuzie hisia hizo. Ongea na rafiki yako wa karibu,mwenzi wako, daktari yako au hata mshauri nasaa.

Punguza Maumivu Yako ya Mwili

Katika wakati huu unaonyonyesha, ni vema kumuuliza daktari au mkunga wako dawa gani ya maumivu unaweza tumia.

Kulingana na kiwango cha maumivu, daktari atakuandikia dawa ya kupunguza maumivu au kukushauri utumie dawa za kutuliza maumivu kama ibuprofen (Advil,Motrin)

Unaweza kutumia mpira wa maji ya moto kupunguza maumivu katika eneo la mshono na tumbo la chini kwa ujumla, hakikisha unatumia maji ya uvuguvugu.

Lenga katika Ulaji wa Lishe Bora.

Lishe bora ni muhimu katika miezi baada ya kujifungua kama ilivyokuwa kipindi ukiwa mjamzito. Bado wewe ni chanzo kikuu cha virutubisho kwa mwanao kama unanyonyesha. Kula vyakula vya kila aina itasaidia mtoto kukua katika afya na nguvu.

Utafiti unaonyesha ulaji wa mbogamboga za majani wakati unanyonyesha unasaidia kuyapa maziwa ladha ambayo inaongeza kasi ya mtoto kunyonya na kufurahia maziwa ya mama kadiri anavyokua.

Pia kunywa vimiminika vingi, hususani maji. Unahitaji vimiminika vya ziada kuongeza upatikanaji wa maziwa na kuzuia kukosa choo.

Wasiliana na Daktari Endapo:

Bado utapata maumivu katika eneo la mshono, unaweza kutoka damu au kutoka usaha mpaka wiki ya sita baada ya upasuaji. Hii ni kawaida.

Lakini dalili zifuatazo zinakupa  haki ya kuwasiliana na daktari wako, kwasababu zinaweza kuwa ishara za maambukizo:

  • Kuvimba, uwekundu, au usaha kutungika katika mshono
  • Maumivu kuzunguka mshono
  • Homa kali zaidi ya 38⁰C (100.4⁰F)
  • Usaha wenye harufu mbaya kutoka ukeni
  • Kutoka damu nyingi ukeni
  • Kuvimba au uwekundu katika ngozi ya miguuni
  • Kupumua kwa shida
  • Maumivu ya kifua
  • Maumivu ya matiti

Pia wasiliana na daktari wako kama unasikia huzuni na unyonge.

Mwisho kabisa, kama una rafiki au ndugu ambaye alipitia hali hii ya kujifungua kwa njia ya upasuaji, usijilinganishe nao. Kila mwanamke ana uzoefu wa tofauti katika njia hii ya kujifungua. Lenga katika kupona na upatie muda mwili wako kurudia hali yake ya awali.

IMEPITIWA:02 APRIL 2020

Virusi Vya Corona COVID19 na Ujauzito

 

Je, wajawazito na kina mama wanaonyonyesha wanahitaji kujua nini kuhusu virusi vya corona?

Kuna mengi yasiyofahamika kuhusu madhara ya virusi vya corona kwa wajawazito na kina mama wanaonyonyesha. Lakini uelewa wa madhara ya virusi hivi utaongezeka kadiri muda unavyoenda.

Kuwa mjamzito huleta wasiwasi na hali ya sintofahamu kwa wamama wengi watarajiwa, hata kama kila kitu kinaenda sawa.

Wanahitaji kuepuka aina fulani ya vyakula mfano samaki wasiopikwa vizuri na jibini laini. Hii ni kwasababu miili yao inabadilika kwa kiasi kikubwa kila siku na utaratibu wake wa kawaida unaweza kuvurugika.

Taifa la Uingereza ni moja ya nchi ambazo hivi karibuni zimewahusisha wanawake wajawazito katika kundi la watu walio katika hatari za kupata maambukizi haya. Inashauriwa wanawake wajawazito kukaa mbali na mikusanyiko ya watu ili kupunguza nafasi za kushika virusi vya Corona. Inaeleweka, wajawazito wengi na familia zao wana wasiwasi na wamechaganyikiwa kwasababu ya ujio huu wa Virusi vya Corona.

Pamoja yote hayo, ukweli unabaki kuwa hatuna ufahamu wa kutosha kuhusu madhara ya virusi hivi vya Corona COVID-19 kwa wajauzito. Kuwepo kwa ufahamu wa kutosha husaidia kuchukua hatua za uhakika. Uwepo mdogo wa wanawake wajawazito waliopata maambukizi haya pamoja na ufahamu wa kutosha wa Virusi hivi vya Corona kwa ujumla utatusaidia kutoa ushauri wa ziada kwa wanawake wajawazito kuchukua tahadhari mapema.

Mfumo Dhaifu wa Kinga ya Mwili

Mwanzoni ilidhaniwa kipindi cha ujauzito kinga ya mwili ya mwanamke inadhoofika na kumfanya kuwa katika hatari ya kupata maambukizo. Hata hivyo, kama ilivyo vitu vingi vinavyohusiana na mwili wa binadamu ushahidi mpya unaonesha kuwa kinga mwili ya mjamzito hupanda kipindi cha ujauzito, na wakati mwingine huwa ni ya kubadilika badilika.

Mabadiliko haya ya kinga ya mwili kipindi cha ujauzito ni muhimu kwa ajili ya kumpa nafasi mtoto anayeendelea kukua katika hatua tofauti za ujauzito. Kwa mfano katika hatua za kwanza za ujauzito kinga ya mwili inabadilika ili kuruhusu upandikizaji katika mwili. Wakati mwingine mfumo wa kinga unahitaji kujirekebisha katika njia tofauti, mfano mzuri ni wakati mwili wa mwanamke unajiandaa kupata uchungu wa kujifungua.

Jambo la muhimu katika maelezo yote haya ni kwamba kuwa na mfumo wa kinga wenye kubadilika badilika inakuweka katika hatari kubwa ya matatizo ya Virusi vya Corona kama vile shida katika upumuaji na hata homa ya mapafu (pneumonia).

Kitu cha kwanza cha kutiliwa mkazo ni wanawake wajawazito waendelee kuhudhuria miadi yao ya kliniki katika hospitali isipokuwa kama wameambiwa vinginevyo na mkunga au daktari wao.

Kwa sasa hakuna sababu ya kubadilisha mpango wako wa kujifungua, kama uliandaa hapo awali. Mpango wa kujifungua unahusisha mahali unapotarajia kujifungulia (hospitali, zahanati, kituo cha afya, au nyumbani) na aina gani ya dawa za maumivu unatarajia kupata.

Walakini, ikiwa umeonekana na dalili zinazoashiria maambukizi ya Virusi vya Corona, kama kikohozi kikavu au joto kubwa la mwili, kubanwa kifua na kupumua kwa shida,  ni lazima ujitenge (self-isolation) na wasiliana na daktari au mkunga wako haraka.

Vilevile, kwa wanawake wajawazito wenye matatizo mengine ya kiafya wanahitaji kuwa makini zaidi na kukaa mbali na mikusanyiko ya watu ikiwezekana kufikiria kujitenga (self-isolation) kipindi cha ujauzito. Wanawake waliopata ugonjwa wa kisukari, aina ya ugonjwa wa kisukari ambayo ni matokeo ya ujauzito ijulikanayo “Ugonjwa wa Kisukari kipindi cha Ujauzito” (gestational diabetes), wanatakiwa kuchukua tahadhari na kupunguza migusano na watu.

Kuwa mgonjwa wa kisukari wakati wa ujauzito ni kundi la hatari hata bila kupata Virusi vya Corona, kwasababu ugonjwa huu wa kisukari unaongeza ugumu wakati wa ujauzito na kujifungua. Zaidi ya hapo, viwango vikubwa vya sukari katika damu kwa mda mrefu bila kutibiwa na kuangaliwa vizuri vinaweza kudhoofisha mfumo wa kinga zaidi.

Kutokana na mfumo wa kinga unaobadilika kila hatua wakati wa ujauzito ni vizuri wanawake wasio na matatizo ya kiafya kuchukua tahadhari na kukaa mbali na watu pale inapobidi.

Kama ilivyo wajawazito wengi wanaishi na wenzi wao au mara nyingine mtoto/watoto wao wengine, ushauri huu ni vizuri kufuatwa ili kupunguza nafasi ya kuweka afya ya mama mjamzito katika hatari ya kupata maambukizi ya Virusi vya Corona.

Tahadhari hizo ni pamoja na kufanya kazi ukiwa nyumbani kwa wale wanaoweza, kataa mgusano wa aina yeyote na watu na epuka sehemu za mikusanyiko.

Mwisho kabisa, ili kuwasaidia wajawazito kuwa na ujauzito wenye afya na kinga ya mwili nzuri katika kipindi hiki, ni vizuri kuzingatia mlo bora wenye madini chuma kwa wingi (kama mboga za majani zenye kijani kilichokolea, samaki na mayai) na madini ya foliki ambayo yanapatikana kwenye maharage, kunde, maharage ya kijani n.k. Bila kusahau vidonge vya vitamini vya kila siku ulivyoandikiwa na daktari wako vinasaidia pia.

Je, ninaweza kumpatia mtoto wangu Virusi vya Corona?

Je, kuna uwezekano wa mama mjamzito aliyepata maambukizi ya Virusi vya Corona kumpatia mtoto anayeendelea kukua ndani ya mwili wake?  Hili ni moja ya swali linalowaumiza wajawazito wengi na familia zao.

Ukweli ni kwamba kuna maambukizi mengi ya virusi, bakteria na fangasi ambayo yanaweza kupatiwa mtoto kipindi cha ujauzito, kama vile Virusi vya Ukimwi, Homa ya Manjano, Tetekuwanga, Rubela na Toxoplasmosis (maambukizi yanayosababishwa kwa kula nyama isiyopikwa vizuri na iliyogusana na kinyesi cha paka).

Hakuna ushahidi unaoonyesha Virusi vya Corona vinaweza kumpata mtoto aliye tumboni kama mama mjamzito anayo maambukizi. Ila kwa sababu virusi hivi ni vipya wanasayansi wanaendelea kuusoma ugonjwa huu taratibu na tutegemee taarifa zaidi hapo mbeleni.

Utafiti uliochapishwa katika jarida la kujitegemea la Kidaktari liitwalo “The Lancet” ambalo liliwafuatilia wanawake 9 waliopatikana na maambukizi ya virusi hivi baada ya kufanyiwa vipimo nchini China, waligundua hakuna mtoto hata mmoja aliyezaliwa na maambukizi haya (ikumbukwe wanawake hawa wote walijifungua kwa njia ya upasuaji). Ijapokuwa idadi ni ndogo ila inatia matumaini.

Pia hakuna ushahidi ulioonyesha kulikuwa na virusi ndani ya kimiminika cha amnion “Amniotic fluid” hichi ni kimiminika kinachomzunguka na kumlinda mtoto wakati wa ujauzito. Pia hakuna ushaidi uliopatikana ndani ya sampuli za damu zilizochukuliwa kutoka katika kitovu cha kila mtoto. Hali hii inaweza kupendekeza kujifungua kwa njia ya kawaida kwa mjamzito aliye na maambukizi ni njia salama, lakini hatuna majibu ya uhakika kuhusu hili kwasababu idadi ya tafiti zilizofanywa ni ndogo sana.

Kwa tafiti zote hizi inaonyesha kuna ushahidi kidogo kuwa watoto wanaweza kupata maambukizi ya virusi hivi kutoka kwa mama zao wakati wa ujauzito.

Je, ninaweza kumpatia mtoto wangu maambukizi kwa njia ya kunyonyesha?

Hakuna uwazi wa kutosha katika suala la maziwa ya mama, hata hivyo hatuwezi fanya hitimisho kama maziwa ya mama yanabeba virusi au la!

Baadhi ya virusi, kama virusi vya UKIMWI vinajulikana kuenezwa kwa njia ya maziwa ya mama, lakini mpaka tulipofikia hakuna ushahidi kuwa Virusi vya Corona COVID-19 vinaweza kuenezwa kwa njia hii pia.

Ushauri uliopo ni kuwa wamama ambao hawana maambukizi haya waendelee kuwanyonyesha watoto wao ila wakumbuke kunawa mikono yao vizuri kabla na baada ya kuwanyonyesha.

Ikiwa mama ataonekana na dalili za kukohoa au joto kubwa la mwili, ni vizuri atumie njia mbadala ya kunyonyesha (mf: vifaa maalumu vya kukamua maziwa) na kumpatia mtu mwingine asiye na maambukizi kumlisha mtoto mpaka atakapo pona.

Kuna ushahidi wa kutosha kuwa maziwa ya mama ni mazuri kwa kuongeza kinga mwili ya mtoto, hivyo kusitisha moja kwa moja kumnyonyesha mtoto wako kunaweza kumuweka katika  hatari ya kupata maambukizi kwa urahisi.

Kadiri muda unavyokwenda, haitaepukika na tutarajie kushuhudia wanawake wengi wajawazito wakipata virusi vya corona COVID-19, hii itapelekea wanasayansi kuweza kutambua zaidi jinsi kirusi hiki kinafanya kazi na ni kwa namna gani kinamuathiri mjamzito. Kwa sasa kuchukua hatua za kujikinga ni muhimu – kuosha mikono kwa maji tiririka, kuepuka kukaa karibu karibu sana ikiwemo kuepuka maeneo yenye mikusanyiko ya watoto, kukaa nyumbani, kuepuka wageni ni njia zinazohitaji kufuatwa kuweza kuwa salama.

 

IMEPITIWA: 19 MARCH 2020