Mtandao #1 kwa Afya ya Mama na Mtoto

Address:

P. O. Box 38995, Dar es Salaam, Tanzania

Kunyonyesha au kutumia maziwa ya formula?

Kunyonyesha au kutumia maziwa ya formula, njia ipi ni bora kwa mtoto?

Unyonyeshaji wa maziwa ya mama ni njia mojawapo ya mafanikio makubwa kabisa ya kufanikisha na kuhakikisha afya ya mtoto. Kama kila mtoto akinyonyeshwa maziwa ya mama kwa ndani ya saa moja toka azaliwe, upewaji pekee maziwa ya mama kwa miezi ya sita ya kwanza katika uhai wa mtoto, na kuendelea kumnyonyesha hadi umri wa miaka miwili kutahakikisha mtoto anakua na afya bora. Huu ndio msingi wa kuimarika kiafya ya mwili na akili kwa watoto wote. Kitakwimu duniani, chini ya asilimia 40 ya watoto wachanga chini ya umri wa miezi sita hawapewi maziwa ya mama.

Ushauri nasaha wa kutosha kuhusu kunyonyesha na huduma ni vitu muhimu kwa ajili ya akina mama na familia katika kuanzisha na kudumisha zoezi hili la kunyonyesha.
Shirika la afya duniani lipo kikamilifu katika kukuza hali ya unyonyeshaji kama chanzo bora cha chakula kwa ajili ya watoto wachanga na watoto wadogo.

Shirika la Afya Duniani (WHO) linapendekeza:

Kunyonyesha maziwa ya mama pekee kwa miezi sita ya kwanza katika maisha ya mtoto. Katika miezi sita, vyakula, kama vile matunda kama parachichi, ndizi na mboga, lazima aanze kuwekewa ili kumsaidia katika kipindi anachokuwa akinyonya kwa muda wa miaka miwili au zaidi.

Aidha:
1. Kunyonyesha kunapaswa kuanza ndani ya saa moja baada ya kujifungua.
2. Kunyonyesha lazima kuwe “kwenye mahitaji”, kama mara kwa mara kama mtoto anavyohitaji iwe mchana ama usiku
3. Unyonyeshaji wa chupa hauna budi kuepukwa kadiri iwezekanavyo

Faida za Kunyonyesha

Kwa watoto wachanga
Maziwa ya mama ni chakula bora kwa watoto wachanga na watoto wakuao. Pia huwapa watoto wachanga virutubisho vyote wanavyohitaji kwa ajili ya maendeleo ya afya zao.
Maziwa haya ni salama na yana kinga ambayo husaidia kuwalinda watoto wachanga dhidi ya magonjwa ya kawaida katika utoto kama vile kuhara na homa ya mapafu (pneumonia), ambayo kimsingi ndio sababu kuu mbili za vifo vya watoto wachanga duniani kote.

Maziwa ya mama hupatikana kwa urahisi na kwa bei nafuu (bure), ambayo husaidia kuhakikisha kwamba watoto wachanga hupata lishe ya kutosha.

Faida za muda mrefu kwa watoto
Kwa zaidi kuna manufaa kwa ajili ya watoto, kwani kunyonyesha maziwa ya mama inachangia kuwa na maisha yenye afya njema.

Vijana na watu wazima ambao walikuwa wananyonya maziwa ya mama walipokuwa watoto wana uwezekano mdogo sana wa kuwa na tatizo la unene na uzito uliopitiliza.
Pia huwa wako katika hali nzuri ya kutokupata uwezekano wa kuwa na aina ya 2 ya ugonjwa wa kisukari na vile vile katika kipimo cha akili huwa wako vizuri.

Faida kwa akina mama
Kunyonyesha pia kuna faida kwa mama. Kunyonyesha maziwa ya mama inahusishwa na njia ya asili kama njia ya uzazi wa mpango (Asilimia 98 huwasaidia katika miezi sita ya kwanza baada ya kujifungua katika kuzuia mimba).

Pia inapunguza hatari ya kupata saratani ya matiti na na saratani ya mifuko ya mayai (ovary) baadaye katika maisha, husaidia wanawake kurudi katika maumbile yao kama kabla ya ujauzito, na husaidia kupunguza viwango vya unene uliopitiliza.

Vipi kuhusu maziwa ya kopo au maziwa ya formula?

Maziwa ya kopo/formula kwa watoto wachanga huwa hayana kingamwili /antibodies ambayo hupatikana katika maziwa ya mama tu. Wakati ambapo maziwa ya kopo/formula hayakutayarishwa vizuri, kuna hatari inayotokana na matumizi ya maji yasiyokuwa safi na salama na pia kutokuwa na vifaa vya kutakasia/kuondoa vijidudu. Hivyo kuwepo uwezo wa bakteria katika maziwa haya.

Utapiamlo pia unaweza kutokea ukisababishwa na uchanganyaji wa maziwa ya unga na maji mengi kuliko kipimo. Kama utaweka mazingira ya kumpa maziwa ya unga kila siku mara kwa mara siku zote, na ikitokia siku hayapo maziwa hayo, na ukawa huna budi kurudi katika kumnyonyesha maziwa ya mama, basi changua hilo halitakuwa sahihi kwa sababu kutakuwa na upungufu wa uzalishaji wa maziwa katika matiti ya mama kwa siku hiyo.

Kwa ushauri wa kisayansi ni vyema kukuchukua maamuzi ya kumnyonyesha mtoto maziwa ya mama. Maziwa ya kopo/formula yatumike pale tuu kutakapokuwa na ushauri toka kwa mkunga au daktari kufanya hivyo.

Taratibu za kusimamia maziwa mbadala

Kanuni za kimataifa za kudhibiti masoko ya maziwa mbadala ilipitishwa mwaka 1981 ilikuwa na wito huu:

• Maandiko yote katika maziwa ya kopo/ formula na habari za kuelezea hali ya faida ya kunyonyesha maziwa ya mama na hatari ya afya ya maziwa mbadala/ yakopo au unga lazima zielezwe
• Si ruhusa kufanya matangazo ya maziwa mbadala /maziwa ya kopo ama unga kibiashara
• Si ruhusa sampuli yeyote ya maziwa mbadala kutolewa kwa wanawake wajawazito, mama au familia zao; na
• Si ruhusa kusambaza maziwa mbadala/maziwa ya kopo ama unga kwa bure au ruzuku kwa wafanyakazi wa afya au na vituo vya afya.

Unyonyeshaji sahihi

Unyonyeshaji una hitaji kujifunza na wanawake wengi wanapambana na magumu mengi sana mwanzoni wanapoanza hatua hii. Maumivu ya chuchu, na hofu kwamba hakuna maziwa ya kumtosheleza mtoto ni kawaida.

Vituo vya afya ambayo vinaunga mkono kunyonyesha hufanya mafunzo juu ya kunyonyesha sambamba na upatikana wa ushauri kwa mama wapya katika kunyonyesha. Hii huhamasisha viwango vya juu na uzoefu katika kunyonyesha.

Kutoa msaada huu na kuboresha huduma kwa akina mama na watoto wachanga, kuna hatua kadhaa zimetolewa kama”mama na mtoto” katika kliniki nchini kwetu. Katika mpango huu wa “mama na mtoto” ushauri na taratibu za unyonyeshaji hutolewa bure.

Kufanya kazi na kunyonyesha

Akina mama wengi ambao hurudi kufanya kazi makazini kwao wengi wao huacha kwa muda au kabisa kunyonyesha watoto wao. Sababu kuu ikiwa ni hawana muda wa kutosha, au mahali pa kukaa na kunyonyesha, hujieleza kwa kukosa kuhifadhi ya kusitiri maziwa yao.

Akina mama wanahitaji usalama, hali ya usafi na sehemu ya kujisitiri au sehemu ya karibu na mahali pa kazi yao ili waweze kuendelea kunyonyesha. Pia ili kumwezesha kuendelea na kazi zake, wengi wao hulazimika kuomba likizo ya kulipwa ya uzazi, pamoja na upatikanaji wa vifaa vya kwa ajili ya kutoa na kuhifadhi maziwa kutoka kwenye matiti.

Kumuanzishia mtoto chakula kigumu

Ili kukidhi mahitaji ya kuongezeka kwa watoto katika umri wa miezi sita, chakula kigumu lazima kiazishwe ili kusaidia ukuaji wake wa haraka kipindi hiki. Kwa wakati huu mtoto huyu anatakiwa aendelee kunyonya pia maziwa ya mama. Vyakula vya mtoto vinaweza kuwa vimetengenezwa mahsusi kwa ajili ya mtoto au inashauriwa viwe vinachukuliwa kutoka kwenye milo ya familia za watu wazima kwa kadiri inavyowezekana.

Wataalamu wa afya na vyakula wanasema ya kwamba:

• Kunyonyesha hakupaswi kupungua wakati unaanza kumpatia chakula kingine kigumu
• Mtoto apatiwe chakula akilishwa kwa kutumia kijiko, kikombe na sahani na sio kwatika chupa ya kunyonya.
• Chakula lazima kiwe safi, salama na mtoto alishwe katika mazingira safi.
• Muda wa zaidi na wa kutosha unahitajika kwa ajili ya watoto wadogo kujifunza kula vyakula vingine vigumu.

Imepitiwa: July 2017

Huduma ya Kwanza: Mtu aliyekabwa kwenye koo la hewa – choking

Huduma ya kwanza: Mtu aliyekabwa kwenye koo la hewa – Choking

Kukabwa kwenye koo la hewa hutokea pale kitu kinapokwenda na kubana koo la hewa kwenye koromelo na kuzuia kupita kwa hewa kuelekea na kutoka kwenye mapafu. Kwa watu wazima mara nyingi vipande vya chakula ndio husababisha. Kwa watoto wadogo mara nyingi huwa ni vitu vidogo vidogo wanavyochezea na kuvimeza kwa bahati mbaya. Kwa sababu kukabwa kwa koo huzuia oksijeni kuelekea kwenye ubongo ni vyema kupata huduma ya kwanza mara moja.

Alama ya kimataifa ya mtu aliyekabwa koo la hewa ni mikono kuonekana imeishikilia shingo kwa nguvu. Kama mtu aliyekabwa koo la hewa hatoi ishara hii, ziangalie pia ishara zifuatazo:

Kushindwa kuongea
Kupumua kwa tabu au kwa kelele
Kushindwa kukohoa kwa nguvu
Midomo na kucha kuwa za bluu
Kupoteza fahamu

Mtu aliyekabwa koo la hewa:

Shirika la huduma ya kwanza – Red Cross linaelekeza kutumia mufumo wa “tano – kwa – tano” kuweza kutoa huduma ya kwanza:
Toa mapigo matano 5 mgongoni: kwa kutumia upande wa mkono ambao ungetumia kupiga kofi ila kwa nguvu zaidi piga mara tano mgongoni. Sehemu sahihi ya kupiga ni katikati ya mabawa mebega kwa nyuma mgongoni.
Toa mapigo matano 5 kwenye tumbo: Toa mapigo matano ya tumboni ambayo kwa jina lingine ni kufaitilia mfumo wa Heimlich “Heimlich maneuver”
Pishana kati ya mapigo matano mgongoni na matano tumboni: mpaka kilichokaba kimetoka na kuachia koo la hewa.

Kuutumia mfumo wa Heimlich “Heimlich Maneuver”

Kwa mtu mwingine:

Simama nyuma ya mtu husika. Zungusha mikono yako kukizunguka kiuno chake. Msogeze mutu mhusika aegemee mbele zaidi kidogo.
Tengeneza ngumi kwa mkono mmoja. Iweke ngumi hii juu kidogo ya kitovu chake.
Ikamate ngumi hii kwa mkono mwingine. Bonyeza kwa nguvu tumboni kwa mpigo wa haraka kuelekea juu – Kana kwamba unataka kumnyanyua mtu huyu juu.
Toa mapigo haya ya tumboni mara 5, kama itahitajika. Kama kilichomkaba bado hakitoki, rudioa mzunguko wote wa tano-kwa-tano kama uluvyoelezewa awali.

Kama upo peke yako fanya kwanza mzunguko wa mapigo ya mgongo na tumbo kabla ya kupika simu ya dharura kuomba msaada. Kama kuna mtu mwingine karibu, muelekeze mtu huyu kupiga simu kuomba msaada wakati wewe unatoa huduma ya kwanza.
Kama mhusika ataonekana anapoteza fahamu, inashauriwa kumfanyia huduma ya kwanza ya CPR inayojumuisha kukisukuma kifua na kutoa pumzi mdomoni. (Makala nyingine inayohusu huduma hii ya kwanza itafuata baadae)

Kwako mwenyewe:

Kwanza kama upo mwenyewe na umekabwa koo la hewa, piga 112 au namba ya dharura ya sehemu ulipo haraka iwezekanavyo. Halafu, ijapokuwa unaweza ukashindwa kujipiga mgongoni ila bado una uwezo wa kutumia mfumo wa kupiga tumboni na kukiondoka kinachokukaba.
Weka ngumi juu kidogo ya kitovu
Ishike ngumi hii kwa mkono mwingine na egemea sehemu ngumu – upande wa meza au egemeo la kiti itafaa.
Iingize ngumi yako ndani ya tumbo kuelekea juu

Kwa mwanamke mjamzito au mwenye umbile kubwa
Iweke mikono yako juu zaidi kuliko mfumo wa Heimlich wa kawaida, chini kidogo ya chembe cha moyo, pale mbavu za chini kabisa zinapokutana kufuani.
Endelea kutumia mfumo wa Heimlich kwa kubonyeza kwa nguvu kuelekea kifuani, kwa mapigo ya haraka.
Rudia mpaka chakula au kilichokuwa kimekaba kimetoka au mhusika anapoteza fahamu

Namna ya kuifungua njia ya hewa kwa mtu aliyepoteza fahamu:

Mlaze mtu kwa mgongo kwenye sakafu
Fungua njia ya hewa. Kama unakiona kilichomkaba nyuma kabisa ya koo la mhusika, ingiza kidole mdomoni na ukisafishe kinachomkaba kitoke nje. Kuwa muangalifu usikisukume chakula au chochote kinachomkaba ndani zaidi, kwani inaweza kutokea kwa urahisi zaidi kwa watoto.
Anza mapigo ya uhai (Cardiopulmonary Resescitation – CPR) kama kinachomkaba kinaendelea kumkaba na mtu haoneshi dalili ya kupata nafuu. Mapigo ya uhai ya CPR yanaweza yakasababisha kinachomkaba kikatoka. Kumbuka kuangalia mdomo mara kwa mara.

Mtoto mdogo chini ya mwaka mmoja:

Chuchumaa kama upo kwenye mkao wa kukaa. Mbebe mtoto kicha kikiwa kinaangalia chini kwenye mkono wako, ambao umelala juu ya paja lako.
Mbonyeze kwa kiganja chako kichanga huyu mara tano katikati ya mgongo wake. Kwa mkao huu na mapigo haya ya mgongoni yatatosha kukiondoa kitu kinachomkaba.
Mshike mtoto uso ukiwa unaangalia juu kwenye mkono wako, katika mkao ambao kichwa kipo chini kuliko kiwiliwili kama njia hapo juu haikusaidia. Kwa kutumia vidole viwili vilivyowekwa kwenye chembe cha moyo cha mtoto, toa mapigo matano ya kukibonyeza kifua.
Rudia mapigo ya mgongoni na msukumo wa kifua. Kama kupumua hakutarudi. Piga simu kuomba msaada wa matibabu ya haraka.
Anza kufanya mapigo ya uhai (CPR). Kama moja ya njia hizi zimefungua njia ya hewa lakini mtoto huyu bado hajaanza kupumua

Mtoto mdogo juu ya mwaka mmoja:

• Toa mapigo ya tumbo pekee

Kujiweka tayari kwa tatizo kama hili au kwa matatizo mengine ambayo huduma ya kwanza inaweza ikawa ndio msaada pekee utakaosaidia kuokoa maisha ya mtu wako wa karibu. Ni vyema ukajifunza au kujisomea kuhusu namna mbali mbali za kutoa huduma ya kwanza. AFYAPLUS itakuwa inatoa makala moja kila wiki inayohusiana na huduma ya kwanza.

Imepitiwa: July 2017

Vifahamu vyakula bora na vile vinavyokatazwa kipindi cha ujauzito

Ni vyakula gani vya kuepuka kutumiwa na wajawazito?

Ili mtoto azaliwe akiwa na afya njema pamoja na akili timamu, akiwa tumboni lazima alishwe lishe bora na mlo sahihi. Mwenye jukumu la kutoa lishe bora na sahihi kwa kiumbe kilichomo tumboni ni mama. Anatakiwa kujua aina ya vyakula anavyopaswa kula. Vivyo hivyo, anatakiwa kujua aina ya vyakula vya kuviepuka.

Katika makala ya leo, tunaangalia orodha ya vyakula vilivyokatazwa. Mama mja mzito haruhusiwi kuvila vyakula vifuatavyo kwa faida ya kiumbe kilichomo tumboni na kwa faida yake mwenyewe:

Nyama mbichi

Epuka kula samaki au nyama mbichi au iliyopikwa lakini haikuiva vizuri. Utajiepusha na uwezekano wa kula bakteria na vijidudu vingine hatari kwa afya ya mtoto tumboni. Mjamzito anapokula nyama, anatakiwa kuhakikisha imeiva sawasawa.

‘Soseji” na “Sandwich”
Mjamzito haruhusiwi kula ‘soseji’, ‘sandwichi’ za nyama na vyakula vingine vilivyotengenezwa kwa nyama. Inaaminika kuwa nyama zinazoandaliwa kwa ajili ya kutengenezea vyakula kama hivyo, huwa vimewekewa vihifadhi vyakula (preservatives) ambavyo vinaweza visiwe vizuri kwa afya ya mtoto.

Samaki wenye zebaki (Mercury)
Wajawazito wamekatazwa kula samaki wenye kiasi kingi cha madini ya zebaki. Ulaji wa zebaji kwa wajawazito umehusishwa na uzaaji wa watoto taahira. Mfano wa samaki hao ni pamoja na Papa, Chuchunge na dagaa wakubwa.

Mayai Mabichi
Ulaji wa mayai mabichi au vyakula vilivyochanganywa na mayai mabichi, mjamzito haruhusiwi kuvila. Kuna baadhi ya ‘Ice Cream’ na ‘mayonaizi’ hutengenezwa kwa kuchanganywa na mayai mabichi. Mjamzito amekatazwa kuvila vyakula hivyo.

Maini
Maini yana kiwango kikubwa cha madini aina ya chuma. Hata hivyo, yana kiasi kikubwa cha Vitamin A ambacho huweza kuwa na madhara kwa mtoto kikizidi.

Maziwa mabichi
Maziwa mabichi huweza kuwa na bakteria ajulikanae kama ‘Listeria’, ambaye huweza kusababisha kuharibika kwa mimba. Unapokunywa maziwa, hakikisha yamechemshwa au kama ni ya paketi hakikisha ni yale yaliyoandikwa‘Pasteurized’ na siyo ‘Unpasteurized’.

Kafeini (Caffeine)
Ingawa baadhi ya utafiti unaonesha kuwa unywaji wa kiasi kidogo cha kafeini hauna madhara, lakini kuna utafiti mwingine unaonesha kuwa unywaji wa kafeini una uhusiano na kuharibika kwa mimba. Kafeini ni aina ya kirutubisho kinachopatikana ndani ya kahawa.

Iwapo mjamzito atakunywa kahawa, basi anywe kiasi kidogo sana kisichozidi kikombe kimoja kwa siku. Kwa kawaida kahawa hukausha maji mwilini, hivyo unywaji wake husaidia kukauka maji mwilini ambayo ni muhimu sana kwa mjamzito.

Utafiti mwingine unaonesha kuwa kafeini inahusishwa pia na uharibikaji wa mimba, uzaaji wa watoto ‘njiti’ na watoto wenye uzito mdogo. Ni vizuri kunywa maji ya kutosha, maziwa na juisi na kuepuka kunywa vinywaji vyenye kahawa.

Pombe
Hakuna ushahidi unaothibitisha kuwa unywaji wa pombe kiasi kidogo wakati wa ujauzito hauna madhara, kwa maana hiyo matumizi ya pombe hayaruhusiwi kabisa wakati wa ujauzito, hata kama ni kidogo.
Unywaji wa pombe wakati wa ujauzito huweza kuathiri ukuaji mzuri wa mtoto. Kutegemeana na kiasi atakachokunywa mjamzito, pombe inaweza kumsababishia mtoto ugonjwa hatari utokanao na pombe (Fetal Alcohol Syndrome).

Vyakula gani ni muhimu sana kutumiwa na wajawazito?

Lishe bora wakati wa ujauzito ni muhimu sana, kwani lishe hii hutumika kwa mama na mtoto anaendelea kukua tumboni. kwa kawaida mahitaji ya chakula na virutubisho mwilini mwa mwanamke huongezeka wakati wa ujauzito na kadri ujauzito unavyoendelea kukua, virutubisho hivyo hutumika kujenga mwili wa mama na mtoto. hivyo maamuzi ya lishe au lishe mama anayopata huathiri pia maendeleo ya mtoto anayekua mwilini mwake. tutaona vyakula muhimu vya kuzingatia lishe bora wakati wa ujauzito na baadhi ya vitu vya kukwepa.

Mlo kamili (balanced diet), ni muhimu kwa ajili ya maendeleo mazuri ya afya ya mjamzito na mtoto tumboni. Pamoja na mlo kamili mjamzito hupewa virutubisho ziada (supplements) kwa ajili ya kuongeza madini kama ya chuma na Foliki. Mlo kamili unajumuisha vyakula vya wanga, protini, mafuta, vitamini, madini na maji kama inavyochambuliwa hapa chini:

Nafaka na vyakula vya wanga
Vyakula hivi huupa mwili nguvu za kufanya kazi ikiwemo ukuaji wa mtoto tumboni. Vyanzo vya wanga ni kama nafaka mbalimbali(mahindi,mtama,ulezi n.k), viazi, ndizi, mihogo. Ni vizuri mjamzito awe anapata nafaka kamili(whole grains) kama mahindi, ngano na mchele usiokobolewa; cereals n.k.

Nyama, samaki na vyakula vya protini
Hivi ni muhimu kwenye kuujenga mwili, hasa kipindi cha miwezi wa 4 mpaka wa 9 ambacho viungo mbalimbali vya mtoto vinajengwa. Ni muhimu mama apate vyakula vya protini vya kutosha ili kuhakikisha ukuaji wa mtoto unaenda vizuri. Nyama za kuku, ng’ombe, mbuzi, senene, panzi na wanyama wengine ; vyanzo vya protini za mimea kama maharage, soya, njugu, njegere, karanga,korosho n.k . Samaki, maziwa, mayai ni vyanzo vingine vya protini muhimu

Vyakula vya mafuta
Hutumika kwenye kuupatia mwili nguvu pamoja na ujengaji wa seli za mwili. Mara nyingi vyakula kama nyama, karanga, ufuta, alizeti,senene, panzi, samaki na matunnda kama maparachichi huwa na mafuta. Ni vizuri kutumia mafuta yatokanayo na mimea ili kupunguza mafuta yenye lehemu(cholesterol) nyingi.

Mboga za majani na matunda
Matunda na mboga za majani ni sehemu muhimu sana ya mlo wakati wa ujauzito, kwani huupatia mwili vitamini, madini na kambakamba kwa ajili ya kulainisha chakula. Vitamini husaidia kuimarisha kinga ya mwili sambamba na ufanyaji kazi wa mwili. Madini kama ya chuma, kalsiamu, zinki, madini joto(Iodine) na magneziamu ni muhimu kwa ukuaji salama wa mtoto tumboni mwa mama.Vitamini B9 (Foliki asidi) na madini ya chuma hutolewa kama virutubisho ziada kliniki wakati wa ujauzito ili kutosheleza mahitaji ya mwili na kuzuia hatari ya upungufu wa damu kutokea.

Maji
Maji ni muhimu kwenye mmenyenyo na unyonywaji wa chakula, pia husaidia kuzuia choo kigumu, mwili kuvimba na maambukizi ya mfumo wa mkojo (UTI). Inashauriwa mjamzito anywe maji si chini ya lita 2.3 kwa siku, yanaweza kuwa katika chai, juisi, soda, au maji yenyewe. Ni vema zaidi kama akinywa maji kama maji zaidi na kupunguza vinywaji kama soda.

Mfano wa mpangilio wa mlo

Ili kuhakikisha mlo kamili mjamzito anaweza kufuata mfano wa mpangilio wa mlo ufuatao. Katika mpangilio huu inashauriwa kuchagua aina moja ya chakula kutoka katika kila herufi A mpaka E ili kuweza kuupata mlo kamili.

Mfano:

Mlo wa Asubuhi:
A – Chungwa/ Embe/ Ndizi mbivu/ Parachichi
B – Mkate/ Maandazi/ Chapati/ Vitumbua/ Uji
C – Karoti
D – Mayai
E – Maziwa/ Mtindi/ Siagi/ Maziwa ya Soya

Mlo wa Mchana:
A – Parachichi/ Papai/ Ndizi/ Embe na chungwa
B – Ugali/ Wali/ Ndizi/ Makande/ Tambi
C – Mchicha/ matembele/ Mnavu/ Kisamvu/ Spinach/ Kabeji
D – Maharage/ Samaki/ Kuku/ Njugu/ Nyama/ Dagaa
E – Maziwa/ Mtindi/ Siagi/ Maziwa ya Soya.

Mlo wa Usiku:
A – Parachichi/ Papai/ Ndizi/ Embe na Chungwa
B – Wali/ Ndizi/ Viazi/ Tambi/ Chapati
C – Mchicha/ Matembele/ Mnavu/ Kisamvu/ Spinach/ Kabeji,
D – Maharage/ Samaki/ Kuku/ Njugu/ Nyama/ Dagaa
E – Maziwa/Mtindi/Siagi/Maziwa ya Soya.

Imepitiwa: July 2017

Ugonjwa wa Malaria

Ufahamu ugonjwa wa Malaria

Malaria ni ugonjwa unaosababishwa na vimelea vinavyojulikana kama Plasmodium.Vimelea hivi huenezwa na mbu jike aina ya anofelesi (anopheles). Lakini watu wengi huelewa kwamba malaria husababishwa na mbu. Mbu huyu husaidia katika usambazaji tuu wa vimelea husika.

Aina ya vimelea ambavyo humdhuru binadamu kati ya vimelea vingi vya Plasmodium ni:
• Plasmodium Vivax
• Plasmodium Falciparum
• Plasmodium Malariae
• Plasmodium Oval

Plasmodium Vivax: Vimelea hivi havina madhara makubwa ingawa vimesambaa sana kuliko vile vya Plasmodium Falciparum.
Plasmodium Falciparum: husababisha vifo vingi na kwa haraka zaidi.
Vimelea vingine kama Plasmodium Malariae na Plasmodium Oval husababisha pia malaria lakini sio kwa ukali na yenye uharibifu kama vile vya Plasmodium Falciparum. Ukurasa huu umejizatiti zaidi kuzungumzia malaria inayosababishwa na Plasmodium Falciparum, kwani ndio inayotushambulia zaidi ukanda huu wa Afrika Mashariki.

Jinsi mtu anavyopata maambukizi ya malaria

Vimelea (parasites) huingia kwenye mwili wa binadamu baada ya mbu jike aliyeathirika na vimelea hivyo vya malaria wakati akinyonya damu ya binadamu kama mlo wake, atamng`ata na kunyonya damu binadamu mwingine. Ni katika kipindi hiki ambapo mbu huweza kuviacha vimelea alivyovitoa kwa mtu mwingine na kumuathiri mtu huyu. Mbu huyu ana kawaida ya kumdhuru binadamu kwa kumng`ata kuanzia saa kumi na mbili jioni hadi saa kumi na mbili asubuhi.
Vimelea huzaliana ndani ya utumbo wa mbu na baadae husafiri hadi kwenye tezi za mate yake. Wakati mbu anamng’ata binadamu hutoa mate kama ganzi ili binadamu asigundue kama anang’atwa na hapo ndipo vimelea vya malaria humuingia binadamu.
Baada ya kuingia kwenye mwili wa binadamu vimelea hivi husafiri hadi kwenye ini ambapo huzaliana kwa wingi na hatimaye kuingia kwenye mzunguko wa damu na kusababisha uharibifu wa seli nyekundu za damu. Hapa ndipo mtu huanza kujihisi homa, kutetemeka na dalili nyinginezo za malaria.

Dalili za malaria

Dalili za malaria zinategemea mtu na mtu kutokana na nguvu ya kinga yake. Hata hivyo dalili zinazowapata wagonjwa wa malaria zinatokana na hatua ya ugonjwa aliyonayo mtu aliyeambukizwa.

Kuna aina mbili za malaria:
1. Malaria ya kawaida, isiyokuwa kali au sugu kitaalamu inaitwa “Uncomplicated Malaria”. Hii inakuwa haijasababisha madhara makuwa katika mwili.
2. Malaria sugu, kitaalamu “Complicated Malaria”. Hii imeishasababisha madhara kama kuharibu viungo muhimu mwilini kama, ubongo (kupoteza fahamu – cerebral coma), figo (figo kufeli-renal failure), ini (ini kufeli -liver failure), moyo (moyo kufeli – heart failure), mapafu (mapafu kufeli – pulmonary failure), upungufu wa sukari mwilini (hypoglycaemia). Na pia kuwa na vimelea vingi (hyperparasitaemia).

Dalili za malaria isiyo kali

1. Homa ikiambatana na maumivu ya kichwa
2. Maumivu ya mwili
3. Tumbo kuuma na kuharisha
4. Kichefuchefu na kutapika
5. Kizunguzungu
6. Kutokwa jasho
7. Kutetemeka
8. Kifua kuuma
9. Kukosa hamu ya kula

Dalili za malaria kali

1. Mabadiliko katika mwenendo na tabia (kuchanganyikiwa)
2. Uchovu mkubwa kupita kiasi (mgonjwa hawezi kukaa au kusimama)
3. Upungufu mkubwa wa damu (mgonjwa husikia kizunguzungu sana)
4. Kupoteza fahamu
5. Kupumua kwa shida
6. Degedege/mtukutiko mwili (Kwa watoto wadogo)
7. Kutapika kila kitu, kushindwa kunywa au kunyonya kwa watoto
8. Mzunguko hafifu wa damu, kutokwa damu isiyo ganda kwa urahisi
9. Figo kushindwa kufanya kazi na kukojoa mkojo wenye rangi nyeusi/kahawia.

Kumbuka:

Malaria hushambulia zaidi watoto wenye umri chini ya miaka mitano (5), wanawake wajawazito na watu wanaoishi na virusi vya ukimwi. Hii ni kutokana na kinga zao za mwili huwa chini.

Hizi dalili pia hutokea katika magonjwa yanayoambukizwa na bakteria, kwa mfano:
Homa inaweza kuwa dalili ya UTI, Pneumonia, Typhoid, n.k
Kukohoa kunaweza kuwa sababu ya maambukizi katika mapafu mfano pneumonia, kifua kikuu n.k
Kutapika na kuharisha inaweza kuwa dalili za magonjwa ya maambukizi ya tumbo pia.

Hivyo ni vema ukipata dalili hizi usichukue dawa bila kupata uchunguzi wa kitaalamu na pia ushauri kutoka kwa madaktari. Unapopata dalili hizi wahi hospitali ili wataalamu wakuchunguze na kujua ni ugonjwa gani ulionao.

Matibabu ya Malaria

Kwa malaria isiyosugu/isiyokali, dawa inayopendekezwa kwa sasa kama tiba ya kwanza ni dawa ya Mseto (ALU), pia gonjwa anatumia dawa akiwa nyumbani kwake. Kutokana na dalili za mgonjwa huyu, inawezekana anaweza kula na kunywa vizuri na dalili nyingine pia sio za kushtua sana ndio maana mgonjwa hupewa vidonge na ushauri wa mlo na vitu vya kuepuka akiwa anatumia dawa za malaria, hususani bidhaa za pombe.

Kwa malaria sugu, matibabu yanayopendekezwa kama tiba kwa mgonjwa ni dawa ya Quinine kwa njia ya dripu. Pia mgonjwa anapatiwa matibabu chini ya uangalizi wa wataalamu wa afya. Mgonjwa analazwa hospitalini hadi anapopata nafuu na kuweza kula mwenyewe. Wagonjwa wengi wenye malaria kali au sugu, kutokana na hali yao ya kupoteza fahamu, kutapika kila kitu na kushindwa kula, pamoja na dalili zingine kama zilivyoorodheshwa hapo juu, ni vyema walazwe ili wapewe huduma stahiki.

Jinsi ya kujikinga na Malaria

Malaria ni moja ya magonjwa yanayoongoza kwa vifo nchini Tanzania. Ila ni ugonjwa ambao vilevile kwa maamuzi na bidii za binadamu ugonjwa huu unaweza kukwepeka. Hivyo basi, zifuatazo ni namna mbalimbali za kujikinga na malaria:

1. Kutumia chandarua kilicho wekwa dawa ya kuua mbu. Kutumia tu chandarua haitoshi. Ni muhimu kulala kwenye chandarua kilicho na dawa. Chandarua nyingi zinazouzwa madukani kwa muda huu zimeshawekwa dawa tayari, lakini unashauriwa kuuliza na kuwa na uhakika kuwa chandarua unachonunua kimewekwa dawa.

2. Kuweka mazingira safi kwa kufukia madimbwi na mashimo yasababishayo maji kutuama. Maji yanayotuwama huzalisha sana mbu. Mayai ya mbu hupendelea maeneo yenye majimaji lakini yasiyokuwa na kusogea (yaliyotuama), mfano madimbwi ya maji ya mvua yaliyokaa muda mrefu bila kukauka, unyevunyevu vichakani na kwenye nyasi ndefu, makopo yenye uwazi yaliyotelekezwa na kujaa maji ndani yake, magari mabovu yaliyonyeshewa mvua na kukusanya maji ndani, mabwawa madogomadogo kama ya kufugia samaki n.k. Hivyo ni vyema kufukia madimbwi, kufyeka nyasi, kuchoma au kusafisha makopokopo na magaloni na pia kuondoa magari mabovu na chochote kinachoweza kukusanya maji kwa muda mrefu kwa eneo lote linalozunguka nyumba yako. Ukifanya hivi utakuwa umesababisha hatua muhimu ya kisababishi cha malaria (mbu) asizaliwe.

3. Kuteketeza mazalia ya mbu kwa kunyunyuzia dawa ya DDT. Baada ya kufanikisha namba mbili hapo juu, na kuna sehemu ambazo mazalia ya mbu yanaweza kutokea na hakuna jinsi ya kuepuka maji haya yaliyotuama inashauriwa kunyunyuzia dawa ya DDT. Dawa hii ni sumu ambayo pia inaweza ikamdhuru binadamu. Hivyo shughuli ya kunyunyizia dawa hii hufanywa na wataalamu wa afya na mazingira.

4. Kufukuza na kuzuia kung`atwa na mbu. Ni ukweli kwamba pamoja na juhudi zote hapo juu bado kuna uwezekano wa kung`atwa nambu kwani tupo kwenye eneo la tropiki ambalo ndio makazi yao. Hivyo basi njia nyingine za ziada zinahitajika kujikinga using`atwe na mbu waliofanikiwa kuzaliwa.

Kuua mbu – Kutumia dawa za kupuliza au kufukiza ndani na nje ya nyumba. Kuna baadhi ya kampuni wanafanya kazi ya kuua vimelea (fumigation) maeneo mbalimbali.
Kufukuza mbu – Kutumia dawa za kupuliza au kufukiza ndani na nje ya nyumba (Ifahamike kuwa kuna dawa ambazo zina uwezo wa kufukuza pekee na kuna ambazo zinaua kabisa hivyo unavyonunua dawa dukani elewa unanunua dawa ya aina gani ili uitumie kama inavyoelekezwa)
Kuzuia mbu – Dawa za kupaka. Kwa wakati ambao haupo nyumbani inawezekana ukawepo kwenye sehemu yenye mbu, mfano baa, mpirani au hata kazini katika ule muda ambao mbu hung`ata, ni vyema ukajikinga nao kwa kujipaka dawa mbalimbali za kuwafukuza au kuwaua mbu pale wanapokukaribia au kuanza kukung`ata. Dawa hizi zinatoa harufu ambayosio rafiki kwa mbu hawa au zina uwezo wa kuwaua pindi wanapoanza kukuchoma.

5. Kujikinga na ugonjwa wa malaria kwa kina mama wajawazito ni muhimu. Wajawazito wana hatari kubwa zaidi ya kung`atwa na mbu kutokana na mabadiliko yao ya kimwili, mfano joto la mwili kuongezeka, hivyo mbu huweza kuwafikia kwa urahisi zaidi. Inapendekezwa na wizara ya afya kwamba wanawake wajawazito watumie dawa ya malaria aina ya “SP” kabla ya kujifungua. Hii itawasaidia kama kinga dhidi ya malaria kwao na kwa watoto wao tumboni. Dozi ya dawa hizi hutolewa katika vituo vya afya vinavyo toa huduma kwa mama na mtoto.

6. Ni muhimu kuzingatia matumizi sahihi ya dawa za malaria kwa wagonjwa. Kuzingatia dozi sahihi inaweza ikawa kinga kwa maambukizi mengine yanayokuja. Vilevile kutokumaliza dozi kunamaanisha kuviacha baadhi ya vimelea mwilini ambavyo havikufa tayari mpaka kipindi ulipoacha dozi.

7. Usitumie dawa bila kumuona daktari kwani kwa kufanya hivyo utakuwa unaongeza usugu wa dawa mwilini mwako bila sababu ya msingi na pia unahatarisha maisha yako. Usugu wa dawa za malaria ni hatari na inamaanisha ukipata malaria na vimelea ulivyonavyo vimeshakuwa sugu kwa dawa zilizopo za malaria, maisha yako yanakuwa hatarini kwani madaktari watashindwa kukutibu.

Wito

Malaria ni ugonjwa hatari unaoua kwa haraka hivyo pindi unapohisi una dalili za malaria kama zilivyoorodheshwa hapo awali, wahi katika kituo cha kutoa huduma za afya kilichokaribu na wewe ili upatiwe uchunguzi na kupata tiba sahihi.

Imepitiwa: July 2017

Teknolojia: Matumizi ya “drones” kusafirisha dawa vijijini

Matumizi ya “drone” kusafirisha dawa

Katika karne hii ya ishirini na moja, maendeleo ya kiteknolojia ni makubwa sana kuliko baadhi yetu tunavyoweza kuamini. Dunia imefikia kwenye muongo wa mabadiliko makubwa ya kisayansi na teknolojia. Katika sekta ya usafiri, teknolojia pia imekua kwa haraka sana hivi punde.

“Drone” ni nini?

Kifaa kinachoitwa “drone” ni mfano wa ndege ndogo inayoweza kupaa na kusafiri bila kuwa na rubani ndani yake. Drones zinaweza kuwa na ukubwa tofauti tofauti kulingana na uwezo wake wa kufanya kazi. Vindege hivi vidogo huwa vinaendeshwa na muongozaji au rubani ambaye huwa anatumia kompyuta au simu ya mkononi iliyounganishwa na mtandao na GPS ya drone husika.

Matumizi mbalimbali ya “drones”

Matumizi ya drones yapo ya aina mbalimbali. Kwa muda mrefu drone zimekuwa zikitumika kuchukua picha au video za maeneo husika kwa kupiga picha zikiwa angani. Ila pia zimekuwa zikitumiwa na wataalamu wa ardhi kuweza kupima na kutengeneza ramani za mashamba, ranchi na pia hifadhi za mali asili. Kwa baadhi ya nchi zilizoendelea matumizi ya drone yamekua na hutumika pia na majeshi ya ulinzi na usalama kwa matumizi mbalimbali.

Matumizi ya “drone” kusafirisha mizigo

Ndani ya miaka mitano iliyopita kampuni kubwa duniani kwa uuzaji wa bidhaa mbalimbali ya Amazon na kampuni za usafirishaji kama UPS, FEDEX na DHL zimekuwa zikitafiti njia rahisi, salama na ya haraka zaidi kuweza kuifikisha mizigo sehemu husika kwa kutumia drones. Matatizo kadhaa yameorodheshwa ikiwa ni changamoto zinazoweza kujitokeza katika aina hii ya usafiri. Kwanza ni usalama wa anga inayotumiwa na ndege za kawaida za abiria na mizigo. Ukizingatia kuwa “drones” zenye uwezo wa kupaa na kufikia au kuweza kukutana na ndege za kawaida, hali ya usalama lazima itakuwa ni changamoto. Changamoto ya pili ni usalama wa matumizi ya drones kufanya uhalifu wa aina nyingine. Kwa mfano mapema mwaka 2016 watu wasiojulikana walifanikiwa kusafirisha na kufikisha madawa ya kulevya kwenye jela moja huko Uingereza. Pia kuna changamoto nyingine kama namna drone itakavyoweza kuutua mzigo baada ya kuufikisha kwenye anuani husika. Pamoja na changamoto hizi ni ukweli usiofichika kwamba miaka michche ijayo tutashuhudia matumizi makubwa zaidi na kwa wingi zaidi ya drone katika sekta mbalimbali.

Matumizi ya drone kusafirisha dawa

Nchini Rwanda, matumizi ya drone kwenye sekta ya afya yalianza rasmi mwaka 2016 baada ya serikali ya Rwanda kwa kushirikiana na kampuni ya kimarekani ya ZIPLINE walianza shughuli za usafirishaji wa damu na madawa au vifaa tiba muhimu kuweza kuzifikia hospitali zilizopo kijijini. Ifahamike kwamba kwa nchi kama Rwanda yenye miundombinu haba ya usafiri vijijini inaweza kuchukua hadi masaa manne kwa gari kufikisha bidhaa kama damu inayohitajika kwa dharura kutoka hospitali moja kwenda nyingine. Teknolojia ya kutumia drone inaweza kufanikisha safari hii kwa muda wa dakika 15 pekee.

Nchi ya Rwanda imekuwa ya kwanza Afrika na inawezekana ya kwanza duniani kuanza kuruhusu matumizi ya drone kwa usafirishaji wa bidhaa mbalimbali. Matumizi ya drone yamepokelewa tofauti na nchi mbalimbali duniani, nyingine zikihitaji mlolongo wa vibali na sheria za kuweza kusimamia shughuli zake huku nchi nyingine kama Morocco, Kenya na Uganda wamezuia utumiani wa drone katika shughuli mbalimbali na sheria kali zinasimamia hili. Nchini Ghana watumiaji wa drone wanaweza wakafungwa kifungo cha hadi miaka 30 kama hawataandikisha “drones” zao.

Miaka ijayo

Ni sahihi kukubali kuwa miaka michache ijayo teknolojia na matumizi ya drones na vifaa vingine vitakavyogundulika itakuwa sio hiari tena ila ni lazima kwani matumizi yake yatakuwa salama zaidi na bei rahisi kulinganisha na njia mbadala. Ni wakati mzuri sasa kwa serikali na nchi za bara la Afrika kuandaa na kutengeneza miswada na sheria zitakazowezesha serikali kuwa tayari kukumbatia teknolojia mbalimbali zinazokuja na kutoa mwongozo haraka iwezekanavyo. Kitendo cha kufungia au kukataza matumizi fulani ya teknolojia kadiri zinavyobuniwa ni kudorosha na kurudisha nyuma ubunifu na maendeleo ya nchi husika katika karne hii ya uchuni wa kidigitali.

Imepitiwa: 24 July 2017

Je Wajua: Saratani ya titi inatibika endapo itatambulika mapema

Saratani ya matiti ni nini?

Saratani ni aina ya ugonjwa unaosababisha ukuaji wa seli za mwili kubadilika na kukua bila mpangilio maalumu.

Saratani ya matiti hutokea kwenye titi ambalo kwa kawaida lina sehemu ya kutengeneza maziwa ijulikanayo kama “lobules” na aina fulani ya mishipa inayounganisha hizi lobules na chuchu za titi. Sehemu kubwa iliyobakia ya matiti inajumuisha mafuta na zile kitaalamu tunazoita “connective” na “lymphatic tissue”. Saratani ya matiti inayotokea kwenye “lobules” huitwa “lobular carcinoma” na ile inayotokea kwenye “ducts” huitwa “ductal carcinoma”.

Vihatarishi vya Saratani

Kuna mambo kadhaa ambayo yameonekana kuwa na uhusiano, ama wa moja kwa moja au kwa kupitia vitu vingine, wa kusababisha saratani ya matiti, au kumfanya mtu au kundi la watu kuwa katika hatari ya kupata ugonjwa huu kuliko wengine. Mambo hayo ni pamoja na:
Jinsia: Ingawa, saratani ya matiti huweza kutokea kwa wote wanawake na wanaume, imeonekana kuwa wanawake ni waathirika wakubwa zaidi wa saratani hii ikilinganishwa na wanaume.
Umri: Uwezekano wa kupata saratani hii huendana na umri wa mtu. Kadiri umri wa mtu unavyoongezeka ndivyo pia uwezekano wa kupata saratani hii unavyozidi kuwa mkubwa. Wanawake walio na umri wa kuanzia miaka 50 wapo kwenye hatari kubwa (mara 2 au 3 zaidi) kuliko walio na umri wa miaka 45.
Uasili wa mtu (ethnicity): Saratani ya matiti hutokea zaidi kwa wanawake wazungu kuliko wanawake wa kiafrika au wenye asili ya afrika (weusi).
Uzazi: Wanawake ambao hawajazaa au kunyonyesha wapo kwenye hatari kubwa ya kupata saratani ya matiti. Wanawake wanaopata ujauzito kwa mara ya kwanza baada ya miaka 30 nao pia wapo kwenye hatari kubwa ya kupata saratani hii.
Historia ya ugonjwa huu katika familia: Wanawake walio katika familia zenye historia ya ugonjwa huu wana uwezekano mkubwa wa kupata saratani ya matiti ukilinganisha na wale ambao hawana historia ya ugonjwa huu katika familia zao. Kwa mwanamke aliye na ndugu (mama, dada au mtoto) ambaye aliwahi kupata saratani hii kabla ya umri wa miaka 50, uwezekano wa mwanamke huyu kupata ugonjwa huu ni mara mbili ya yule ambaye hana historia hii.
Umri wa kuvunja ungo: Wanawake wanaovunja ungo (kupata hedhi) kabla ya umri wa miaka 12 wapo kwenye hatari zaidi ya kupata ugonjwa huu.
Kuacha kupata hedhi: Kwa kawaida wanawake huacha kupata hedhi wafikapo miaka 45, hali ambayo kitaalamu hujulikana kama menopause. Wanawake wanaochelewa kuacha kupata hedhi, kwa mfano wale wanaoendelea kupata hedhi wakiwa na zaidi ya miaka 45, wapo kwenye hatari kubwa zaidi ya kupata saratani ya matiti.
Historia ya saratani ya matiti: Wanawake ambao wamewahi kupata ugonjwa huu kwenye titi la upande mmoja hapo kabla, wana uwezekano mkubwa wa kupata tena saratani kwenye titi la upande mwingine hapo siku za usoni.
Ulaji wa vyakula venye mafuta mengi: Tafiti zinaonesha kuwa, wanawake wanaopendelea kula vyakula vyenye mafuta mengi wapo kwenye hatari zaidi ya kupata ugonjwa huu.
Kuongezeka uzito: Tafiti nyingine zimeonesha kuwa, wanawake wanene wana uwezekano mkubwa wa kupata saratani ya matiti ukilinganisha na wale wa uzito mdogo au wa kati.
Uvutaji sigara: Kuna matokeo yenye kukinzana kuhusu uhusiano wa uvutaji sigara na hatari ya kupata saratani ya matiti. Wakati baadhi ya tafiti zinaonesha uhusiano wa karibu kati ya uvutaji sigara na uwezekano wa kupata saratani ya matiti, tafiti nyingine zinaonesha majibu yenye kutofautiana kuhusu uhusiano wa uvutaji wa sigara na saratani ya matiti. Hata hivyo, kwa ujumla, wanawake wanaojizuia kuvuta sigara wanakuwa na afya njema zaidi kuliko wale wanaovuta sigara.
Unywaji pombe: Imeonekana kuwa wanawake wanaokunywa pombe zaidi ya chupa moja kwa siku wana uwezekano wa kupata saratani ya matiti kwa asilimia zaidi ya ishirini.
Historia ya tiba ya mionzi: Wanawake ambao wamewahi kupata tiba ya mionzi hususani wakati wa ukuaji wa matiti, wapo kwenye hatari zaidi ya kupata ugonjwa huu. Hali hii husababishwa na ukweli kuwa mojawapo ya madhara ya mionzi ni kuongeza uwezekano wa kupata saratani ya aina yoyote.
Matumizi ya dawa za kupanga uzazi: Kuna ushahidi kuwa saratani ya matiti ina uhusiano na matumizi ya muda mrefu ya vidonge vya kupanga uzazi.
Kuwepo kwa kiwango kikubwa cha homoni mwilini: Kwa wale wanaotumia tiba ya homoni inayojulikana kama hormone replacement therapy, kwa sababu nyingine yeyote ile, au wale wenye kiwango kikubwa cha homoni kama vile oestrogen na progesterone mwilini mwao wapo kwenye hatari zaidi ya kuugua saratani ya matiti.
Kuwa na matiti makubwa: Wanawake wenye matiti makubwa (dense breast tissue) wana uwezekano mkubwa wa kupata saratani ya matiti. Hali hii hutokana na ukweli kuwa wakati mwingine ni vigumu sana kwa madaktari kutambua kama wana saratani au la kutokana na ukubwa wa matiti yao.

Dalili za Saratani ya Matiti

Dalili ya awali inayoweza kutambulisha saratani ya matiti ni kuwepo kwa uvimbe kwenye titi ambao huwa na hali tofauti na sehemu nyingine za titi. Hata hivyo, si kila uvimbe kwenye titi unaashiria uwepo wa saratani ya matiti.
Uvimbe huu huwa mgumu, unaochezacheza kwenye titi, ambapo wakati mwingine unaweza kuwa na maumivu makali au kusiwe na maumivu yeyote. Uvimbe huu huwepo zaidi ya mzunguko mmoja wa hedhi kwa wale ambao hawajaacha kupata hedhi.
Dalili nyingine ni pamoja na:

  • kuwepo kwa uvimbe kwenye sehemu za kwapa
  • Sehemu ya titi kuingia ndani inayoashiria uvimbe usioonekana au usioweza kuhisiwa
  • Mabadiliko kwenye chuchu, kama vile chuchu kuzama ndani au kuwa na nundu ndogo ndogo, chuchu kuwasha, kuhisi kama kuchoma, kidonda kwenye chuchu au chuchu kuwa na kovu ambalo huashiria saratani ya sehemu hiyo
  • Kubadilika kwa umbo la titi, ngozi ya titi kuwa kama ganda la chungwa (peu de orange), ngozi kuwa na rangi nyekundu, na kuongezeka kwa joto kwenye titi. Dalili hizi huashiria kusambaa kwa saratani mwilini.
  • Dalili nyingine ni chuchu kutoa maji yasiyo ya kawaida ambayo hayana rangi. Aidha wakati mwingine, chuchu hutokwa damu au majimaji yenye rangi nyingine tofauti.
  • Ugunduzi wa Saratani ya Matiti

    Pamoja na mgonjwa kufanyiwa uchunguzi wa kitabibu na wataalamu wa afya kuweza kutambua uwepo wa tatizo hili, anaweza pia kufanyiwa vipimo vifuatavyo ili kusaidia kutambua ugonjwa huu.

  • X-ray ya matiti au Mammogram ambayo ina uwezo wa kuonesha ulipo uvimbe kwenye matiti
  • Ultra-Sonography ni kipimo kinachosaidia kutambua iwapo uvimbe uliopo ndani ya matiti umejaa maji ama la ili ufanyiwe vipimo zaidi
  • Kipimo kinachofanywa kwa kuchukua sehemu ya uvimbe (Aspiration) kwa kutumia aina fulani ya sindano (fine needle) na kisha kupeleka maabara sehemu iliyochukuliwa kwa ajili ya kutafitiwa zaidi ili kugundua uwepo wa saratani. Kwa kitabibu kipimo hiki hujulikana kama Fine Needle Aspiration and Cytology (FNAC)
  • Kipimo kingine ni upasuaji mdogo unaofanywa kwenye titi lililoathirika kwa ajili ya kuchukua sehemu ya titi (surgical biopsy) na kisha kuipeleka maabara kwa ajili ya uchunguzi zaidi.
  • Aidha kwa nchi zilizopiga hatua ya kimaendeleo, mgonjwa anaweza pia kufanyiwa vipimo kama:

  • PET Scan: Hii ni aina mpya ya kipimo ambacho kinahusisha CT Scan na PET kwa pamoja. Kipimo hiki kina uwezo wa kutambua uwepo wa saratani ya matiti, iwapo saratani hiyo imesambaa ama bado, na kama itakuwa imeshasambaa, basi ni sehemu gani ya mwili iliyoathirika.
  • Aidha kipimo hiki, kina uwezo wa kutofautisha tezi au lymph nodes zilizovimba zina uhusiano na saratani (Metastatic lymph nodes) au hazina uhusiano na saratani (Benign lymph nodes).

    Baadhi ya matabibu huwiwa ugumu kutofautisha kati ya kuvimba kwa tezi kunakosababishwa na saratani na kule kunakosababishwa na vitu vingine tofauti na saratani. Hali hii hutokea kwa wagonjwa wa saratani wenye tezi zilizovimba ambao hudhani kuwa kuvimba huko ni sababu ya saratani (metastatic lymph nodes).
    Kipimo hiki pia husaidia madaktari kuwatibu wagonjwa wa saratani kwa kutumia mionzi kwa usahihi zaidi ( Precise Radiotherapy) au kutumia mionzi inayolekezwa na kipimo hiki (PET Scan guided radiotherapy). Aidha, PET Scan huweza pia kutumika kuonesha maendeleo ya mgonjwa wa saratani baada ya kupata tiba ya mionzi (Radiotherapy) au dawa za kutibu saratani (Chemotherapy).

  • Kipimo kingine hujulikana kama DCE MRI (Dynamic contrast MRI). Hiki nacho ni kipimo kipya kwenye ugunduzi na tiba ya saratani. Aina ya kipimo hiki hutofautina na kipimo cha MRI ya kawaida kwani DCE MRI ina uwezo wa kutoa maelezo ya ziada namna uvimbe wa saratani unavyopata damu yake kupitia mishipa ya damu (blood vessels of the tumor) na hivyo kukua na kuongezeka zaidi. Uwezo mwingine wa DCE MRI ni kutoa maelezo mengine sawa na PET Scan.
  • Hata hivyo, vipimo hivi vya PET Scan na DCE MRI kwa sasa havipatikani nchini Tanzania.

    Tiba ya saratani ya matiti

    Upasuaji

    Lengo kuu la upasuaji ni kuondoa saratani kwenye titi pamoja na tezi (lymph nodes). Zipo aina kadhaa za upasuaji unaoweza kufanywa kwenye titi lililogundulika kuwa na saratani.
    Aina hizo ni pamoja na:

    Lumpectomy: Huu ni upasuaji unaofanywa kuondoa sehemu ya saratani pamoja na sehemu ya titi ambayo haijaathirika kwa saratani. Hii hufuatiwa na tiba ya mionzi (radiotherapy) kwa muda wa kati ya wiki 6 au 7. Mgonjwa anayefanyiwa aina hii ya upasuaji anakuwa na uwezekano wa kuishi muda mrefu sawa na anayefanyiwa upasuaji wa kuondoa titi lote lililoathirika.
    Simple au Total mastectomy: Ni aina ya upasuaji inayohusisha uondoaji wa titi lote lililoathirika kwa ugonjwa wa saratani.
    Radical mastectomy: Aina hii ya upasuaji uhusisha uondoaji wa titi lote na kundi la tezi liloathirika kwa saratani, pamoja na misuli ya sehemu za kifua (chest wall muscles). Hata hivyo, upasuaji wa aina hii ni nadra sana kutumika siku hizi.
    Modified radical mastectomy: Ni aina ya upasuaji inayohusisha uondoaji wa titi lote lililoathirika pamoja na kundi lote la tezi (lymph nodes) chini ya mkono (axilla) bila kuhusisha uondoaji wa misuli ya kifua.

    Kwa ujumla, lumpectomy na mastectomy, zote zinahusisha uondoaji wa kundi la tezi ambalo lipo karibu na uvimbe wa saratani (regional lymph nodes).

    Tiba ya mionzi

    Mionzi inaweza kutumika kuharibu seli za saratani zilizobaki kwenye matiti, kifua (chest wall), au/na eneo la chini ya mkono mara baada ya upasuaji kufanyika. Mionzi pia inaweza kutumika kupunguza ukubwa wa uvimbe wa saratani kabla ya kufanyika kwa upasuaji.

    Tiba ya saratani kwa njia ya dawa (Systemic therapy)

    Tiba ya aina hii inahusisha matumizi ya kemikali maalum za kutibu saratani (chemotherapy) pamoja na matumizi ya homoni (hormonal therapy).
    Tiba kwa kutumia homoni (Adjuvant hormonal therapy) hutumika ili kuua seli za saratani ambazo hazikugundulika hapo awali na ambazo yawezekana zimesambaa sehemu nyingine za mwili. Tiba hii hutolewa baada ya kufanyika kwa upasuaji wa kuondoa uvimbe wa saratani.
    Aina hii ya tiba hutegemea na ukubwa wa uvimbe, matokeo ya vipimo vya kimaabara vya saratani (histological results), na iwapo saratani imesambaa hadi kwenye tezi za kwenye kwapa la mgonjwa ama la. Tiba hii pia yaweza kutolewa kwa mgonjwa ambaye saratani imeshasambaa mwilini kwake kwa muda mrefu, na ambaye hawezi kufanyiwa upasuaji.
    Baadhi ya kemikali zinazotumika kutibu saratani ya matiti ni cyclophosphamide, methotrexate, na flouracil. Kwa kawaida dawa hizi hutolewa kwa kujumuisha dawa 2 au 3 kwa wakati mmoja.
    Ieleweke pia kuwa, kama ilivyo kwa dawa nyingine za kutibu magonjwa mengine tofauti na saratani, kemikali (dawa) hizi za saratani pia zina madhara mbalimbali kwa mtumiaji. Madhara haya huletwa na ukweli kuwa, pamoja na kuwa kazi kuu ya kemikali hizi ni kuua seli zenye saratani, hutokea pia kuua na kuathiri seli za kawaida yaani zisizo na ugonjwa wa saratani kama vile seli zilizo kwenye mdomo, nywele, pua, kucha, utumbo na hata sehemu za siri za mwanamke.
    Hata hivyo, tofauti na seli za saratani, seli za kawaida huwa na uwezo wa kujizaa tena, kukua na kurudi katika hali yake ya kawaida wakati zile za saratani hazina uwezo huo.
    Madhara ya dawa hutofautiana kati ya mgonjwa mmoja na mwingine.

    Imepitiwa: July 2017

    Mazoezi Mepesi Kipindi cha Ujauzito

    Mazoezi kipindi cha ujauzito.
    Je ni salama?

    Kufanya mazoezi ni jambo ambalo binadamu wengi hulifanya mara kwa mara ikiwa ni mpango wa kimaisha au hulifanya mara moja moja. Mazoezi ni kitendo cha kuushughulisha mwili kwa njia mbalimbali. Mazoezi yaliyojipatia umaarufu ni kama kutembea, kukimbia, kushiriki michezo mbalimbali na hata watu hutumia vifaa maalumu vya mazoezi kuishughulisha miili yao. Hivi karibuni vituo vingi vya mazoezi ambavyo vilikuwa maarufu kwenye nchi zilizoendelea vinaanza pia kuonekana barani Afrika.

    Mazoezi ni mazuri kwa afya ya mwili na akili. Pia mazoezi ni njia nzuri kupata afya bora. Ikiwa ni kawaida kabisa watu wa umri wowote ule kushiriki katika mazoezi, huwa inazua mjadala mara kwa mara ni kwa namna gani wajawazito wafanye mazoezi. Kwanza kabisa je wanaruhusiwa kisayansi kufanya mazoezi?
    Waandishi wa Idhaa ya Kiswahili ya DW waliwahi kuyasema haya kuhusu mabadiliko ya mtazamo wa kisayansi kuhusu kufanya mazoezi wakati wa ujauzito

    Nukuu

    Miaka 20 iliyopita, madaktari wangemuambia mama mjamzito kupumzika kadiri awezavyo, kwa kuhofia kuathiri ukuaji wa kiumbe aliye tumboni, na kusababisha uchungu wa mapema au hata mimba kutoka. Hata hivyo chuo cha wakunga na madaktari wa wanawake cha nchini Marekani ACOG, kinasema kujishughulisha kimwili kuna hatari ndogo sana na kunawasaidia wanawake wengi zaidi.
    Miongozo ya hivi karibuni ya chuo cha ACOG, kuanzia mwishoni mwa mwaka 2015, ambayo inatazamwa kama alama teule duniani kote, inabainisha kuwa wasiwasi kuhusu uzazi wa njiti, kutoka kwa mimba au kudumaa kwa kijusi kutokana na mazoezi haujathibitishwa. Kwa mujibu wa ACOG, wanawake wanatakiwa kuhimizwa kushiriki katika mazoezi ya viungo na kuimarisha misuli kabla na baada ya ujauzito.

    Nicole Goebel/Iddi Ssessanga – DW

    Aina za Mazoezi Kipindi cha Ujauzito

    Mazoezi ya dakika kati ya 20 hadi 30 yanapendekezwa kwa siku nyingi za wiki kwa mwenye ujauzito usio na matatizo yoyote – wakiwemo wale walio na uzito uliopitiliza au wasio na shughuli za kutosha. Haijalishi pia wewe ni mtu wa umri gani. Inapendekeza baadhi ya michezo, kama vile kuogelea au kutembea, ambayo ni rahisi kwa viungo.

    Faida za Mazoezi

    Mazoezi yanaweza kukusaidia kuwa mwenye afya na kukuepushia kisukari cha ujauzito, ambacho kinaweza kukidhuru kiumbe tumboni na kinachohitaji mlo makhsusi, na katika wakati mwingine sindano za insulini hata kama kwa kawaida hauna ugonjwa wa kisukari. Kulingana na ACOG, mazoezi yanaweza pia kupunguza hatari ya tatizo linalosababishwa na kupanda kwa shinikizo la damu na vilevile kujifungua kwa njia ya upasuaji.

    Wakati watafiti wakiendelea kutafuta njia za kuzuia uzito uliopitiliza hasa miongoni mwa watoto wadogo, faida za mazoezi wakati wa ujauzito zimevutia usikivu wa wanasayansi. Wakati hakuna ushahidi kuonyesha kuwa mtoto wako atakuwa na umbo la kimichezo kwa sababu umekuwa ukifanya mazoezi wakati wa ujauzito, mazoezi yanaweza kuathiri ukuaji wa viungo vya mtoto huyo, na hivyo kuwa na faida katika utoto wake na kuendelea.
    Ikiwa mazoezi laini ni jambo usilotegemea kufanya, mazoezi yalioboreshwa ya yoga yanaweza kukusaidia kubakia mnyumbufu na kukusaidia pia dhidi ya maumivu ya mgongo – ambayo ni tatizo la kawaida wakati wa ujauzito, kwa sababu kina mama wanakuwa na kawaida ya kuumwa mgongo kutokana na uzito ulioongezeka.

    Hivyo hakuna kisingizio cha kutokufanya mazoezi- lakini unapaswa kuchagua mazoezi yako kwa umakini. Michezo ya kugusana kama vile soka, ndondi, mpira wa kikapu/pete haishauriwi. Pia jiepushe na michezo ya kujitupa majini, kupanda, kupanda juu ya zaidi ya mita 2,000, na jambo lolote linaloweza kukuweka katika hatari ya kuanguka. Pia jihadhari sana wakati wa joto kali, vilevile pumzike ukiwa na dalili zozote za mafua, maumivu ya kichwa au kizunguzungu.

    IMEPITIWA: OKTOBA,2021.