Mtandao #1 kwa Afya ya Mama na Mtoto

Address:

P. O. Box 38995, Dar es Salaam, Tanzania

Maambukizi Katika Mshono Baada ya Kujifungua kwa Upasuaji.

Ijapokuwa nafasi ya kupata maambukizi ni ndogo sana siku hizi kwasababu ya maendeleo katika sekta ya matibabu na dawa, zipo sababu zinazoweza kuongeza hatari ya hali hii kutokea. Baadhi ya sababu hizo ni pamoja na:

  • Kupoteza damu nyingi wakati wa kujifungua, wakati upasuaji unaendelea au hata wakati wa uchungu.
  • Kujifungua kwa upasuaji na uchungu kuchukua mda mrefu zaidi ya kawaida.
  • Kutokea kwa maambukizi katika utando wa fetasi (kijusi) na maji yanayopatikana katika mji wa mimba yanayomlinda mtoto kipindi chote cha ujauzito (amniotic fluid) kupelekea mambukizi ya bakteria yanayojulikana kama “chorioamnionitis” wakati uchungu unaendelea.
  • Mjamzito akiwa na ugonjwa wa kisukari au ugonjwa unaodhohofisha kinga ya mwili kama virusi vya Ukimwi (HIV).
  • Mjamzito akiwa na mafuta yaliyozidi yanayosababisha kiribatumbo.

Ishara na Dalili za Maambukizi Katika Mshono Baada ya Kujifungua kwa Upasuaji.

Kuelewa kama kidonda kimepata maambukizi kunawea kujulikana kwa kuchunguza eneo la mshono. Ikiwa huwezi kuona kidonda mwenyewe, ruhusu mtu mwingine akaguwe eneo la mshono. Baadhi ya dalili kubwa zinaashiria maambukizi kuwepo katika kidonda ni pamoja na:

  • Wekundu au kuvimba kwenye eneo la mshono, ikiambatana na maumivu.
  • Maumivu katika tumbo la chini baada ya kujifungua yanaongezeka badala ya kupungua.
  • Kidonda kinaanza kutoa usaha.
  • Mama anapata homa kali (100.5˚F)
  • Mama anashindwa kukojoa kwasababu ya hali ya kuungua inayoambatana na maumivu wakati wa kukojoa.
  • Utokaji wa uchafu wenye harufu kali ukeni.
  • Utokaji wa damu ukeni kuongezeka, hali hii itamsababisha mama kubadilisha pedi daima.
  • Utokaji wa damu ukeni yenye matone au madonge madonge.
  • Miguu itaanza kuvimba tena na kuanza kuuma.

Utambuzi wa Maambukizi Katika Kidonda Baada ya Kujifungua kwa Upasuaji.

Madaktari wengi wanachunguza eneo la mshono na kidonda kabla ya kuruhusiwa ili kuhakikisha hakuna maambukizi yeyote. Lakini, wanawake wengi wanapata maambukizi wiki moja baada ya kurudi nyumbani.

Kwa kuanzia madaktari huchunguza eneo la nje la mshono bila kutoa nyuzi au bandeji, mara nyingi uwekundu na kuvimba katika eneo la mshono utamfahamisha vizuri daktari kama kuna maambukizi yeyote.

Muda mwingine, mshono utachunguzwa kwa ukaribu zaidi au kutoa bandeji ili kujua zaidi kwa jinsi gani kidonda kinaendelea kupona. Maambukizi yanaweza kusababisha mshono kuachia mapema zaidi ya ilivotarajiwa.

Kama kuna usaha katika eneo la mshono, daktari atatumia sindao kufyonza usaha wote polepole na kupunguza muwasho. Wakati huohuo sampuli itachukuliwa kutoka kwenye kidonda na kupelekwa maabara kwaajili ya kuchunguzwa zaidi.

Daktari atakuuliza utaratibu wako wa kuangalia kidonda mar azote ulivyokuwa nyumbani na kitu gani kilipita juu ya kidonda kwa wiki moja iliyopita. Hii itamsaidia kupata wazo zuri la chanzo cha maambukizi katika mshono.

Aina za Maambukizi Baada ya Kujifungua kwa Upasuaji.

Baadhi ya maambukizi yanayoweza kutokea baada ya kujifungua kwa upasuaji ni pamoja na:

“Cellulitis”-tishu kuzunguka eneo la mshono zinapoanza kuwa nyekundu na kuvimba. Haya ni matokeo ya kwanza yanayosababishwa na aina fulani ya bakteria (staphylococcal au streptococcal). Usaha unatokea mara chache katika aina hii ya maambukizi.

“Abdominal abscess”-aina hii ya maambukizi inatokea pale eneo la mshono linapoanza kuwasha na kuuma, pembezoni kunaanza kuvimba vilevile. Inapelekea bakteria kushambulia uvungu wa tishu na kusababisaha usaha kutengenezwa. Pia usaha unaanza kutoka nje ya mshono.

“Endometritis”-wakati mwingine maambukizi yanafika kwenye mji wa mimba (uterasi) na kuanza kushambulia ukuta wa ndani ya uterasi. Hali hii inasababisha maumivu makali ya tumbo la uzazi na utokaji uchafu ukeni kunakoambatana na homa kali. Maambukizi haya yanasababishwa na bakteria pia.

Maambukizi katika mfumo wa mkojo (UTI)- kuna baadhi ya wanawake wanaweza hitaji mpira maalumu wa kutoa mkojo wakati wa kujifungua. Matumizi ya mpira huu yanaongeza nafasi ya kupata UTI kwasababu ya bakteria ajulikanae kama “e-coli”.

Maambukizi yanayosababishwa na fangasi anayepatikana mwilini aitwaye candida (thrush)- maambukizi haya yanawashambuliwa wanawake walio na kinga hafifu ya mwili, husababisha fangasi ukeni au hata vidonda mdomoni.

Matatizo Yanayosababishwa na Maambukizi Katika Mshono Baada ya Kujifungua kwa Upasuaji.

  • Ushambuliaji wa tishu zenye afya mwilini “necrotizing fasciitis”
  • Tishu zenye afya za mwili kuwa wazi kupata kidonda
  • Kuachia kwa mshono na sehemu ya ndani ya mshono iliyoanza kupona “dehiscence of the wound”.
  • Kidonda kufunguka kabisa na kinyesi kuanza kutoka kupitia kwenye kidonda “wound evisceration”

 Matibabu ya Maambukizi katika Mshono Baada ya Kujifungua kwa Upasuaji.

  • Chunguza kidonda mara kwa mara kuhakikisha kinapona vizuri au kama kuna chochote kinachotoka kwenye eneo la mshono.
  • Usaha wowote unatakiwa kufyonza ili kurahisisha uponaji.
  • Dawa maalum itumike kusafisha kidonda vizuri na kuondoa aina yeyote ya bakteria.
  • Kusafisha na kubadilisha bandeji katika kidonda kufanyike mara kwa mara.

Njia Mbalimbali za Kuzuia Maambukizi Katika Mshono Baada ya Kujifungua kwa Upasuaji

  • Angalia vizuri kidonda baada ya upasuaji na mjulishe daktari mara moja ikiwa kuna dalili zisizo sawa utaziona.
  • Tumia na maliza dozi ya antibaiotiki ulizoandikiwa na daktari kipindi chote isipokuwa kama umeshauriwa vinginevyo na daktari.
  • Safisha kidonda mara kwa mara na badilisha bandeji kama ilivyoshauriwa na daktari.
  • Vaa nguo zilizolegea juu ya eneo la mshono, epuka kutumia kipodozi chochote.
  • Chagua njia tofauti za kumbeba mtoto wako wakati wa kunyonyesha kuepusha mgandamizo katika kidonda.
  • Usishike eneo la mshono.
  • Mjuze daktari au mkunga ikiwa mwili wako utaanza kupata joto juu ya 100˚F
  • Wasiliana na dakatari wako au mkunga ikiwa dalili za usaha, maumivu au kuvimba zikionekana.

Vidokezo Vitakavyokusaidia Katika Uponaji wa Mshono

  • Hakikisha unatumia dawa mara kwa mara kutibu maumivu na kuvimba eneo la mshono
  • Shika tumbo lako kila unapopiga chafya, tembea wima usipinde mgongo ili kuepusha maumivu ya mgongo hapo baadae.
  • Kunywa maji na vimiminika vya kutosha
  • Usinyanyue kitu chochote kizito.
  • Pumzika kadiri uwezavyo.

IMEPITIWA: OKTOBA, 2021.

Umuhimu wa Mazoezi Kabla na Baada ya Kujifungua

Afya yako baada ya kujifungua inabainishwa na mwili wako kabla ya kujifungua. Hivyo basi, inashauriwa mwanamke kufuata utaratibu mzuri wa mazoezi mara kwa mara kabla ya kushika ujauzito ili kuanda mwili wake kukabiliana na kazi nzito itakayokuja wakati wa uchungu na kujifungua. Mwanamke ambaye alikua imara katika mazoezi atakuwa na uchungu wa mda mfupi kuliko mwanamke ambaye hakuwa imara katika mazoezi. Habari nzuri ni kwamba unaweza kuanza aina yeyeote ya mazoezi, hata kama haujawahi kufanya mazoezi.

Faida za Mazoezi

  • Yanapunguza kubana kwa misuli na msongo wa mawazo.
  • Yanapunguza maumivu ya mgongo.
  • Yananyoosha misuli na kuandaa mwili kwaajili ya siku ya kujifungua
  • Yanaimarisha mzunguko wa damu
  • Yanaimarisha uzazi (uwezo wa kupata ujauzito)
  • Yanaimarisha muonekano na mkao wa mwili.
  • Yanaimarisha ustahimili, wepesi na stamina ya mwili.

Fanya mazoezi mara 4 mpaka 5 kwa wiki ukizingatia mazoezi ya kuimarisha pumzi badala ya mazoezi ya kupunguza mwili. Kujinyoosha, kuogelea, kukimbia na kutembea yajumuishwe katika mpango wa mazoezi.

Muongozo wa Mazoezi Kabla ya Kujifungua

  • Epuka aina yeyote ya mazoezi yayohusisha kuruka na kusababisha majeraha/ kuumia katika tumbo.
  • Epuka mazoezi yanayofanya moyo kwenda kasi sana au kutoka jasho sana.
  • Epuka mazoezi ya kukata tumbo (sit-up & crunches).
  • Epuka kujinyoosha kupitiliza. Inaweza kusababisha jeraha linalotokana na kuachia kwa kiungo cha mwili.
  • Usibane pumzi wakati wa aina yeyote ya mazoezi.
  • Ujauzito unapoendelea kukua, mazoezi yote yapunguzwe na kuweka kikomo mazoezi yote yanayosababisha kupumua kwa nguvu miezi ya mwisho.

Muongozo wa Mazoezi Baada ya Kujifungua

Baada ya kujifungua sio mda wa kuutesa mwili, uruhusu mwili upone kabla ya kuanza mazoezi. Baada ya kupata kibali kutoka kwa daktari au mkunga, unaweza kuanza na mazoezi mepesi ndani ya nyumba yanayozingatia kunyoosha sehemu ya tumbo. Unaweza kujumuisha matembezi mepesi. Mazoezi yatakusaidia kurudia mwili wako wa awali kabla ya ujauzito.

  • Anza mazoezi ya kunyoosha tumbo lako ukiwa bado ndani ya nyumba yako.
  • Jumuisha matembezi mepesi
  • Baada ya miezi mitatu baada ya kujifungua, anza kujumuisha mazoezi ya kuimarisha pumzi na kutoa jasho kama kuogelea. Kama unapendelea kutumia vifaa wakati wa mazoezi unaweza kuanza kutumia pia, kumbuka isiwe vyuma vya kunyanyua.
  • Yoga inaweza kujumuishwa kwenye mpango wako wa mazoezi baada ya miezi mitatu.
  • Epuka mazoezi makali kama kukimbia na kuruka.
  • Epuka kunyanyua vyuma vizito na kujinyoosha sana.

Lishe

  • Hakikisha mwili una maji ya kutosha wakati wote.
  • Mama anatakiwa kula kawaida bila kuruka milo. Anatakiwa kujumuisha vyakula vinavyosaidia utengenezaji wa maziwa ya kutosha katika mlo wake.
  • Kula vyakula vyenye protini, mbogamboga za kijani za majani, vyakula jamii ya mikunde na matunda kwa wingi.
  • Kunywa angalau glasi moja ya maji kabla ya kunyonyesha.

Mazoezi na Vidokezo vya Kupunguza Tumbo Baada ya Kujifungua kwa Upasuaji

Ingawa kuwa mama ni jambo zuri na la kujivunia, wamama wengi wapya wanajaribu kurudia mwonekano wao kabla ya kujifungua. Walakini, baada ya kujifungua kwa upasuaji mwili wako unahitaji muda kupona kwanza. Kujilazimisha kupungua uzito ni hatari, kunaweza kusababisha matatizo yasiyo hitajika. Katika Makala hii, tutakupatia baadhi ya njia salama na madhubuti za kupunguza tumbo baada ya kujifungua kwa upasuaji.

Unatakiwa kusubiri mda gani mpaka kuanza mazoezi?

Kwanini?

Madaktari wanashauri kusubiria wiki 6 mpaka 8 kabla ya kuanza mazoezi yeyote. Usiposubiria mwili wako kupona vizuri unaweza kupata matatizo hatari kama vile:

  • Kutoka damu kwa wingi
  • Majeraha ya viungo na misuli
  • Mshono kufunguka

Hivyo, pata maoni ya daktari kwanza kabla ya kuanza kufanya mazoezi.

Vidokezo vya Kupunguza Tumbo Baada ya Kujifungua kwa Upasuaji.

Kazi ya kuhakikisha tumbo lako linapungua inaweza kuonekana ngumu na isiyo na matumaini, lakini tunakuhakikishia, ni rahisi kufanikishwa kwa vidokezo hivi:

Pata “massage”

Wiki mbili baada ya kujifungua, ni salama kufanyiwa “massage”. Kufanyiwa massage kutasaidia kuvunjavunja fati iliyopo maeneo ya tumbo na kupunguza majimaji kutoka kwenye vifundo (lymph nodes) vinazopatikana katika shingo, kifua, makwapa, nyonga na tumbo. Lakini, epuka eneo la mshono siku za awali, badala yake zingatia maeneo ya mgongo, mikono na miguu. Wiki nne baada ya mshono kuanza kupona, “massage” eneo la tumbo inaweza kufanyika bila maumivu.

Tembeza mwili wako.

Kuchanwa katika baadhi ya misuli ya tumbo kunapelekea ukusanyikaji wa fati kwenye tumbo lako. Hii inasababisha shinikizo katika misuli yako ya tumboni na sakafu ya nyonga. Hivyo ni muhimu kusubiri wiki 6-8 kabla ya kujaribu mazoezi mazito. Kutembea ni zoezi rahisi linalounguza kalori nyingi kwa njia salama. Nenda kwenye matembezi na mtoto wako angalau mara tatu kwa wiki.

Kula mlo wenye afya

Mama wote wanaonyonyesha wanahitaji nguvu ya kutosha. Hakikisha mlo wako una kabohaidreti kwa wingi, fati kidogo na madini na vitamini muhimu za kutosha. Epuka vitu vitamu na vyakula vya kuangwa na mafuta mengi na soda. Kula matunda mengi, mbogamboga na protini. Inashauriwa kurekodi chakula unachokula kwa siku na kiasi cha kalori, kwa kufanya hivi itakusaidia kudumu katika kipimo cha kueleweka cha chakula chako.

Funga tumbo

Unaweza kufunga tumbo baada ya mshono kupona vizuri.

Kunyonyesha

Hii ni njia rahisi ya kupoteza tumbo. Mnyonyeshe mwanao miezi 6 baada ya upasuaji. Kunyonyesha kunaunguza takribani kalori 500 kwa siku, lakini pia homoni ya “oxytocin” inatolewa wakati wa kunyonyesha inayochochea mibano ya uterasi, na kusaidia uterasai kurudia saizi yake ya awali kabla ya ujauzito.

Kunywa maji na vimiminika vya kutosha

Unywaji maji baada ya kujifungua utakusaidia kuweka uwiano wa maji katika mwili wako, vilevile kuunguza fati iliyozidi kuzunguka kiuno chako. Maji yenye limao ni njia rahisi ya kupunguza uzito wako na kusafisha mwili wako. Changanya juisi ya limao, asali na maji ya moto kisha kunywa mara moja kwa siku, inafaa zaidi asubuhi.

Pata usingizi wa kutosha

Njia nyingine ya kufikia lengo la kupoteza tumbo baada ya upasuaji ni kupata usingizi sio chini ya masaa 5. Ni ngumu lakini, ujanja ni mmoja- lala pale mwanao anapolala! Kufanya hivi kutaimarisha hisia zako pia.

Mazoezi ya yoga

Yoga inakusaidia kukaza na kunyoosha misuli ya tumbo. Inasaidia wamama wapya kukabiliana na msongo wa mawazo na mabadiliko katika maisha. Hata hivyo, unashauriwa kuanza yoga wiki ya 6 mpaka 8 baada ya kujifungua. Ongea na daktari wako kuhusiana na hili kabla ya kuanza.

Mazoezi ya Kupunguza Tumbo Baada ya Kujifungua.

Yapo mazoezi kadhaa ya kupunguza tumbo baada ya kujifungua kwa upasuaji. Unaweza kufuata utaratibu mara utakapopona na daktari wako au mkunga kukuruhusu. Unaweza kuanza mazoezi mepesi taratibu ukahamia kwenye magumu, ukiwa na muongozo wa mtaalamu wa mazoezi. Baadhi ya mazoezi unayoweza kujaribu ni pamoja na:

Zoezi la kwanza: unaweza ukafanya zoezi hili ukiwa umesimama, kaa au kulala chini.

Zoezi la pili: fanya zoezi hili kwa angalau sekunde 30 kisha rudia tena mara tatu.

Zoezi la tatu: lala kwa mgongo kisha nyanyua kiuno na mgongo juu, hakikisha mabega yako yako kwenye sakafu. Shikilia mkao huu kwa sekunde 10 kisha laza mwili wako wote kwenye sakafu. Rudia zoezi hili mara 4-6 ili kunyoosha nyonga na kukaza tumbo.

Zoezi la nne: simama wima kisha taratibu inama kuelekea chini mikono yako ikiwa pembeni mpaka kichwa chako kiwe usawa wa magoti yako. Kaa mkao huo kwa sekunde 10 alafu nyoosha tena mwili wako. Rudia mara 4-5 ili kunyoosha mgongo na kuunguza kalori eneo la tumbo.

Zoezi la tano: bana misuli yako ya sakafu ya nyonga, bana ndani kwa sekunde tano kisha achia. Kumbuka usibane pumzi wakati unafanya zoezi hili. Jaribu tena mara 4 mpaka 5, sekunde 10 za mapumziko. Zoezi hili linanyoosha misuli ya nyonga.

Mazoezi baada ya kujifungua kwa njia ya kawaida ni pamoja na:

  • Kutembea
  • Mazoezi ya kubana pumzi ukiwa unakaza tumbo-ukiwa umekaa kitako wima, anza kupumua kwa kuvuta pumzi ndani. Kaza misuli ya tumbo ukiwa unavuta hewa ndani, kisha shusha pumzi taratibu na achia tumbo. Zoezi hili linakusaidia kutuliza misuli ya tumbo na njia nzuri ya kukaza na kunyoosha misuli ya fumbatio na tumbo lako.

  • Zoezi hili linakusaidia kubana tumbo na misuli ya tumbo.

  • Mazoezi ya shingo- kaa kitako wima, taratibu sogeza kichwa chako upande wa kulia alafu upande wa kushoto. Jaribu kushika bega lako la kushoto kwa sikio lako la kushoto, na sikio la kulia kwenye bega la kulia. Shusha kidevu chako chini, kisha angalia juu kwenye paa. Fanya zoezi hili taratibu, aina yeyote ya kugeuka haraka itapelekea kusikia kizunguzungu. Ikiwa umepata kizunguzungu acha zoezi hili haraka wasiliana na mkunga wako ikiwa dalili hii imechukua mda kupotea. Zoezi hili litaimarisha mkao wa mwili wako unaoweza kujikunja kwasababu ya kumbeba mtoto au kunyonyesha.

KUMBUKA

Mama aliyejifungua kwa njia ya kawaida anaweza kufanya mazoezi ya mama aliyejifungua kwa upasuaji, lakini aliyejifungua kwa upasuaji asijihusishe na mazoezi ya mama aliyejifungua kwa njia ya kawaida bila kujadiliana na mkunga au daktari kwanza ili kupatiwa kibali kama ni salama kwako au sio.

Baada ya mazoezi tumia dakika 5 kupumzika ili mapigo ya moyo yarudi kawaida. Unaweza kunyoosha misuli ili kuepuka kuumwa misuli na viungo. Lala chini kwa utulivu macho yakiwa yamefungwa, baada ya hapo unaweza kuendelea na shughuli zako.

Je, nitawezaje kudumu katika mazoezi mara baada ya kuanza? Weka malengo na mafanikio yanayoweza kufikiwa. Ukiweka malengo makubwa mwanzoni mwa mazoezi na mwili wako haujapona vizuri itakuwa vigumu kuendelea na mazoezi. Jipongeze ikiwa utaweza kufanya mazoezi mara 3 kwa wiki au kuongeza mda wa mazoezi kwa siku hata kwa dakika kumi tu. Epuka kabisa mazoezi ya kukata tumbo (crunches & sit-ups).

Jifunze kujua lini upunguze kasi ya mazoezi, mazoezi kupita kiasi yatasababisha afya yako kudhohofika. Mara uonapo ishara zifuatazo, hakikisha unapunguza kasi ya kufanya mazoezi kabla aina yeyote ya mazoezi haijaathiri afya yako:

  • Kujisikia kuchoka badala ya kujisikia safi (fresh).
  • Misuli yako kuuma kwa mda mrefu na wakati mwingine kutetemeka.
  • Kuongezeka kwa mapigo ya moyo asubuhi- ishara kuwa unafanya mazoezi ya mwili makubwa.
  • Misuli na viungo kuuma au maumivu yanayohusiana na kujifungua kujirudi ukiwa unafanya mazoezi.
  • Kutokwa damu ukeni au uchafu, uchafu unaotoka unakuwa na rangi nyeusi.

Mazoezi baada ya kujifungua hayana athari kwenye kunyonyesha. Ukweli ni kwamba, mazoezi haya yanachangia katika uzima na afya ya mama. Ni mazuri kwasababu yanamsaidia mama kujirudi katika hali yake ya awali baada ya msongo wa mawazo aliopata wakati wa ujauzito na kujifungua. Pia mazoezi haya yanamsaidia mama kuwa mkakamavu, mwenye uwezo wa kusimamia malezi ya mtoto wake na aina yeyote ya majukumu yatakayoongezeka.

IMEPITIWA: AGUSTI,2021.

Utunzaji wa Mshono Baada ya Kujifungua kwa Upasuaji.

Kama mama, lengo kuu ni mtoto wako kuzaliwa akiwa mwenye afya na salama. Hata kama, inabidi upasuaji kufanyika, ili kumleta kiumbe wako mzuri duniani.

Wakati huohuo, ni jitihada zinazoeleweka kujaribu kila kitu ili kuhakikisha mshono unapona vizuri na kovu linaonekana kwa mbali sana.

Nini cha kufanya ili mshono upone vizuri?

  • Usafi. Jitahidi kuhakikisha sehemu ya mshono inasafishwa vizuri mara moja kwa siku kwa maji na sabuni. Hakuna haja ya kuumwagia mshono maji kila mara na epuka kusugua kwa nguvu. Unapomaliza kusafisha, kausha taratibu kwa taulo.
  • Tumia mafuta. Baadhi ya madaktari wanasema ni vizuri kupaka mafuta ya mgando kisha kukifunika kidonda na kitambaa safi au bandeji bila kukaza; madaktari wengine wanasema ni vizuri kutopaka chochote na kuacha mshono wazi. Ni vizuri ukiongea na daktari wako au mkunga aliyehusika katika upasuaji wako kuhusu njia ipi ni nzuri kwa mshono wako.
  • Ruhusu hewa kwenye eneo la mshono. Wakati wa usiku vaa gauni linaloachia itasaidia sana hewa kuzunguka, kwasababu hewa inahamasisha uponaji wa majeraha katika ngozi.
  • Hudhuria miadi yako na daktari. Hakikisha nyuzi zinatolewa kwa wakati ili kuepusha kovu baya kutokea. Hivyo kabla ya kuondoka hospitali hakikisha unakumbuka kumuuliza mkunga wako au daktari tarehe ya kurudi kutolewa nyuzi.
  • Epuka mazoezi kwa muda. Itakubidi kupunguza mazoezi ili kuruhusu majeraha katika uterasi na tumbo kupona. Hivyo epuka kuinama au kugeuza mwili ghafla, vilevile usinyanyue kitu chochote kizito zaidi ya mtoto wako. Inashauriwa kusubiri daktari akuruhusu kama ni salama kuanza mazoezi.
  • Tembea kila uwezapo. Jitahidi kutembea, inasaidia kuongeza mzunguko wa damu, inasaidia pia kuponya jeraha na kupunguza nafasi ya damu kuganda kwenye mishipa ya miguu au ogani za nyonga, hali ambayo inawapata wamama waliotoka kujifungua. Pale unapoona unaweza kutembea mbebe mwanao kwenye kigari chake (kama unacho) au mfunge mtoto mbeleko kwa mbele kisha fanya matembezi jioni karibu na nyumbani kwako au kuzunguka nyumba yako.

Ishara kuwa mshono wako umepata maambukizi.

Maambukizi haya husababishwa bakteria katika eneo la mshono baada ya upasuaji. Ikiwa unapitia dalili zifuatazo, wasiliana na daktari wako mara moja:

  • Uwekundu au kuvimba eneo la mshono au ngozi kuzunguka eneo hilo.
  • Homa kali zaidi ya (100.4˚F)
  • Harufu mbaya kutoka kwenye mshono
  • Kuvuja au majimji kuzunguka mshono
  • Usaha kutungika katika mshono
  • Kidonda kuwa kigumu au kusikia ongezeko la maumivu kuzunguka kidonda.
  • Maumivu katika sehemu moja ya mshono (kumbuka kuwa wiki za awali baada ya upasuaji maumivu ni kawaida, lakini pia usipuuzie kama eneo moja tu la mshono linakupa maumivu makali)
  • Mshono kuachia.
  • Maumivu wakati wa kukojoa
  • Uchafu wenye harufu mbaya kutoka ukeni
  • Miguu kuvimba au kuuma
  • Kutokwa damu inayojaza pedi ndani ya lisaa. Wakati mwingine damu inayotoka inakuwa mapande ya damu (damu iliyoganda).

Hali Hatari Zinazosababisha Maambukizi Katika Mshono Baada ya Upasuaji.

Baadhi ya wanawake wako katika nafasi ya kupata maambukizi ya bakteria katika eneo la mshono kwa sababu zifuatazo:

  • Unene uliopitiliza
  • Ugonjwa wa kisukari au dosari yeyote katika kinga ya mwili, (mfano HIV)
  • Matumizi ya mda mrefu ya steroidi
  • “Chorioamnionitis”- maambukizo ya bakteria ya papo kwa hapo yanayoathiri utando wa nje, amnion na maji ya amniotic. Hutokea wakati wa ujauzito au uchungu, bila kutibiwa mapema husababisha maambukizo mazito kwa mama na mtoto.
  • Kutohudhuria miadi ya kliniki (mara chache)
  • Kujifungua kwa upasuaji ujauzito zilizopita
  • Ukosefu wa dawa ya tahadhari kabla ya kuchanwa
  • Uchungu au upasuaji uliochukua wa mda mrefu
  • Upotevu mkubwa wa damu wakati wa uchungu, kuzaa au upasuaji

Maambukizi katika eneo la mshono baada ya upasuaji hutibiwa kwa antibaotiki zinazotolewa hospitali, daktari atakuandikia nyingine upate kurudi nazo nyumbani. Daktari atafungua mshono wako kama ulianza kutoa usaha, kisha atatoa usaha wote. Baada ya kusafisha vizuri daktari ataepusha usaha kujikusanya kwa kuweka kitambaa safi chenye antiseptiki ili kuzuia ukuaji wa bakteria katika mshono. Kidonda kinahitajika kuangaliwa mara kwa mara ili kuhakikisha kinapoa vizuri.

Baada ya siku kadhaa za matibabu ya antibaotiki na daktari kuangalia mshono mara kwa mara, kidonda kitaanza kujifunga vizuri au kupona chenyewe.

Jinsi Gani ya Kuzuia Maambukizi ya Mshono Baada ya Upasuaji

Baadhi ya maambukizi katika mshono hayaepukiki. Lakini ikiwa ulifanyiwa upasuaji wakati wa kujifungua, unaweza chukua hatua kupunguza nafasi ya kupata maambukizi tena, baadhi ya hatua hizo ni pamoja na:

  • Tumia dawa ulizoandikiwa na fuata maelekezo ya kuangalia kidonda yaliyotolewa na daktari au mkunga, ikiwa una swali usisite kuwasiliana na daktari.
  • Kama umepewa dawa za kutumia kutibu au kuzuia maambukizi, hakikisha unatumia dozi nzima bila kuruka au kuacha kuzitumia kipindi kizima cha matibabu.
  • Safisha kidonda chako na badili vitambaa vinavyofunga kidonda mara kwa mara.
  • Usivae nguo zinazobana au kupaka losheni juu ya kidonda.
  • Omba ushauri jinsi gani ya kumpakata mtoto wakati wa kumnyonyesha ili kuepuka mgandamizo mbaya katika kidonda.
  • Angalia joto la mwili wako mara kwa mara, tafuta msaada wa kitiba ikiwa jotoridi lako ni zaidi ya 100˚F (37.7˚C)

KUMBUKA

Kama bado haujajifungua kwa upasuaji, hizi ni hatua unazotakiwa kuchukua:

  • Dumisha uzito wenye afya. Kama wewe sio mjamzito, fanya mazoezi na kula mlo wenye afya ili kuepuka uzito uliopitiliza (kiribatumbo) ukiwa mjamzito.
  • Chagua kujifungua kwa njia ya kawaida kama inawezekana. Wanawake wanaojifungua kwa njia ya kawaida hawana nafasi ya kupata maambukizi baada ya kujifungua.
  • Jitahidi kutibu hali yeyote inayoleta dosari katika kinga ya mwili kabla ya kushika mimba. Ni salama kwako na mtoto ikiwa utatibu aina yeyote ya maambukizi au ugonjwa kabla ya kushika ujauzito.

Maambukizi katika eneo la mshono yanayosababishwa na bakteria baada ya upasuaji yanaweza sababisha matatizo makubwa kama: uharibifu wa tishu zenye afya katika ngozi, mshono kuachia na utokaji wa kinyesi baada ya mshono kuachia. Ikiwa mama atapata matatizo haya, upasuaji wa kurekebisha utafanyika. Inaweza kuchukua mda mrefu kupona, kwa wachache inaweza kusababisha kifo.

IMEPITIWA: AGUSTI, 2021.

Vidokezo Vitakavyomsaidia Mama Kupona Haraka Baada ya Kujifungua kwa Njia ya Upasuaji.

Kujifungua salama ni muda wa furaha sana. Ni wakati unaofanikiwa kukutana na mtoto aliyekuwa anakua ndani yako kwa kipindi cha miezi tisa. Lakini pia kujifungua inaweza kukugharimu, hususa kama umejifungua kwa njia ya upasuaji. Itakuchukua mda mrefu kupona kuliko aliyejifungua kwa njia ya kawaida.

Ufuatao ni ushauri utakao kumsaidia mama aliyejifungua kwa njia ya upasuaji kupona haraka, ili upate muda wa kutosha kumjua na kumlea mtoto wako mchanga.

Pata Mapumziko ya Kutosha.

Kujifungua kwa njia ya upasuaji ni upasuaji mkubwa. Kama ilivyo upasuaji mwingine, mwili wako unahitaji mda wa kupona baada ya hapo. Tegemea kubaki hospitali kwa siku tatu mpaka nne baada ya kujifungua (au zaidi ya hapo kama kulitokea tatizo lingine la kiafya), kisha upe mwili wako wiki sita kupona kabisa.

Ni rahisi kusema zaidi ya kutenda. Ni vigumu kwenda kulala kwa masaa kadhaa huku una mtoto anayehitaji uangalifu mwingi kutoka kwako.

Huenda umesikia ushauri huu wa “lala kila mtoto wako akilala” kwa marafiki na ndugu zako wa karibu. Wako sahihi. Jaribu kulala kila mtoto anapolala. Omba msaada wa kubadilisha nepi na kazi mbalimbali za nyumbani kwa rafiki na ndugu zako wa karibu ili upate muda wa kupumzika kidogo pale inapowezekana. Dakika chache za kupumzika hapa na pale katikati ya siku zinasaidia.

Uangalie Mwili Wako

Kuwa makini zaidi kila unachofanya huku ukiendelea kupona. Epuka kupanda na kushuka ngazi kadiri uwezavyo. Weka mahitaji muhimu ya mtoto na wewe (chakula, nepi, kanga,nguo zako na mtoto) karibu na wewe ili usiamke kila mara.

Usinyanyue kitu chochote kizito zaidi ya mtoto wako. Omba msaada kwa mpenzi/mme wako au rafiki au ndugu yako.

Ni vizuri ukashika sehemu ya kidonda kila unapokohoa au kupiga chafya.

Inaweza kukuchukua mpaka wiki nane kurudia ratiba zako za kwaida. Ni vizuri kumuuliza daktarin wako lini inafaa wewe kufanya mazoezi tena, kurudi kazini na kuendesha gari. Pia subiria mpaka daktari atakapo kuruhusu kujamiana tena.

Epuka mazoezi mazito, ila unaweza kufanya mazoezi mepesi kama kutembea taratibu kila unapoweza. Mzunguko huu utasaidia mwili wako kupona na kuzuia tatizo la kukosa choo na damu kuganda. Pia kutembea ni moja ya njia ya kumtambulisha mtoto katika ulimwengu.

Kama unavyoangalia afya yako ya mwili usisahau hali ya hisia zako. Kuwa na mtoto inaleta hisia ambazo hujawahi kutarajia. Kama ukisikia kuchoka,huzuni au kuvunjika moyo usizipuuzie hisia hizo. Ongea na rafiki yako wa karibu,mwenzi wako, daktari yako au hata mshauri nasaa.

Punguza Maumivu Yako ya Mwili

Katika wakati huu unaonyonyesha, ni vema kumuuliza daktari au mkunga wako dawa gani ya maumivu unaweza tumia.

Kulingana na kiwango cha maumivu, daktari atakuandikia dawa ya kupunguza maumivu au kukushauri utumie dawa za kutuliza maumivu kama ibuprofen (Advil,Motrin)

Unaweza kutumia mpira wa maji ya moto kupunguza maumivu katika eneo la mshono na tumbo la chini kwa ujumla, hakikisha unatumia maji ya uvuguvugu.

Lenga katika Ulaji wa Lishe Bora.

Lishe bora ni muhimu katika miezi baada ya kujifungua kama ilivyokuwa kipindi ukiwa mjamzito. Bado wewe ni chanzo kikuu cha virutubisho kwa mwanao kama unanyonyesha. Kula vyakula vya kila aina itasaidia mtoto kukua katika afya na nguvu.

Utafiti unaonyesha ulaji wa mbogamboga za majani wakati unanyonyesha unasaidia kuyapa maziwa ladha ambayo inaongeza kasi ya mtoto kunyonya na kufurahia maziwa ya mama kadiri anavyokua.

Pia kunywa vimiminika vingi, hususani maji. Unahitaji vimiminika vya ziada kuongeza upatikanaji wa maziwa na kuzuia kukosa choo.

Wasiliana na Daktari Endapo:

Bado utapata maumivu katika eneo la mshono, unaweza kutoka damu au kutoka usaha mpaka wiki ya sita baada ya upasuaji. Hii ni kawaida.

Lakini dalili zifuatazo zinakupa  haki ya kuwasiliana na daktari wako, kwasababu zinaweza kuwa ishara za maambukizo:

  • Kuvimba, uwekundu, au usaha kutungika katika mshono
  • Maumivu kuzunguka mshono
  • Homa kali zaidi ya 38⁰C (100.4⁰F)
  • Usaha wenye harufu mbaya kutoka ukeni
  • Kutoka damu nyingi ukeni
  • Kuvimba au uwekundu katika ngozi ya miguuni
  • Kupumua kwa shida
  • Maumivu ya kifua
  • Maumivu ya matiti

Pia wasiliana na daktari wako kama unasikia huzuni na unyonge.

Mwisho kabisa, kama una rafiki au ndugu ambaye alipitia hali hii ya kujifungua kwa njia ya upasuaji, usijilinganishe nao. Kila mwanamke ana uzoefu wa tofauti katika njia hii ya kujifungua. Lenga katika kupona na upatie muda mwili wako kurudia hali yake ya awali.

IMEPITIWA:02 APRIL 2020

Ugonjwa wa Anemia Baada ya Kujifungua

Anemia(upungufu wa seli nyekundu za damu kwenye damu)  baada ya kujifungua ni ugonjwa wa muda mrefu unasobabishwa na upungufu wa madini ya chuma baada ya kujifungua.

Kuna hatua tatu za anemia:

Hatua ya kwanza

Hakuna dalili zozote zinazoonekana katika hatua hii, kiwango cha chuma ndani ya uboho wa mfupa kinapotea na kusababisha kupungua kiwango cha chuma ndani ya damu.

Hatua ya pili

Athari za anemia zinaanza kuonekana. Kichwa kuuma na kusikia kuchoka ni dalili mojawapo. Upungufu wa madini unaweza kuonekana baada ya kipimo cha damu kufanyika. Katika hatua hii uzalishaji wa haemoglobini unaanza kuathiriwa.

Hatua ya tatu

Viwango vya haemoglobini (protini nyekundu iliyo na madini ya chuma, inayosafirisha oksijeni ndani ya viumbe hai) vinapungua, na kusababisha athari za anemia kuongezeka. Kuchoka sana na uchovu ni dalili kuu katika hatua hii, zinazosababisha kuumwa.

Chanzo cha Anemia baada ya kujifungua

  • Mlo hafifu: ulaji haba wa madini ya chuma kabla na bada ya ujauzito unaweza kusababisha anemia baada ya kujifungua. Madini ya chuma yanayohitajika mwilini wakati wa ujauzito ni 4.4 mg kwa siku. Kwa kuwa madini ya chuma kwenye chakula hayatoshi, ni muhimu kutumia virutubisho vya madini chuma wakati wa ujauzito na kabla ya kupata ujauzito. Upoteaji wa damu kipindi cha hedhi inaweza kusababisha upungufu wa madini ya chuma mwilini kabla ya kupata ujauzito.
  • Upotevu wa damu nyingi wakati wa kujifungua inasababisha upungufu wa madini yaliyotunzwa mwilini na kupelekea anemia naada ya kujifungua. Upotevu wa damu nyingi unaongeza hatari za mama kupata anemia.
  • Magonjwa ya tumbo la chakula, kama uvimbe yanaongeza ufyonzaji wa madini ya chuma kwa wingi.

Dalili za Anemia baada ya Kujifungua

Zifuatazo ni baadhi ya anemia zinazoonyesha upungufu wa madini ya chuma baada ya kujifungua:

  • Kuchoka na kujisikia mchovu.
  • Ngozi kupauka.
  • Kuwa mnyonge.
  • Kupungua wingi na ubora wa maziwa ya mama,inayopelekea uzito wa watoto kupungua.
  • Kichwa kuuma.
  • Moyo kwenda mbio.
  • Kupungua hamu ya tendo la ndoa.
  • Upungufu wa kinga ya mwili.

Hatari zinazoletwa na Anemia baada ya Kujifungua

Anemia inaweza kuleta hatari kwa mama ikiwa tiba haitapatikana kwa muda:

  • Kushindwa kumaliza kazi za kila siku kwasababu ya kuchoka na uchovu
  • Kushindwa kutulia na kufanya kazi.
  • Ongezeko la nafasi ya kuzaa mtoto njiti au kupata shida wakati wa kujifungua, mimba zijazo.
  • Kufariki ghafla kwasababu ya athari kubwa ya kizunguzungu na uchovu.

Wanawake walio katika makundi yafuatayo wana hatari ya kupata Anemia baada ya kujifungua:

  • Upungufu wa madini ya chuma kabla na wakati wa ujauzito.
  • Ujauzito wa mapacha au zaidi.
  • Uzito wa BMI zaidi ya 24
  • Kujifungua kwa njia ya upasuaji
  • Kupata ujauzito mwingine baada ya mda mfupi tangu mimba ya mwisho.
  • Kutoka damu wakati wa ujauzito.
  • Kujifungua kabla ya muda.
  • Shinikizo kubwa la damu kipindi cha ujauzito
  • Plasenta previa- ni tatizo ambapo plasenta inashindwa kusogea kwenda juu hivyo inakuwa chini karibu kabisa na mlango wa kizazi.
  • Kipato kidogo

Anemia inaathiri unyonyeshaji?

Ndio. Anemia inahusiana na tatizo la kukosa maziwa ya kutosha, ambayo inapunguza unyonyeshaji wa kutosha wa mtoto na kupelekea mtoto kuachishwa kunyonya mapema

Mtoto kuachishwa kunyonya mapema kunafanya uzito duni kwa mtoto. Matibabu ya anemia mapema yanazuia matatizo ya unyonyeshaji.

Jinsi Anemia baada ya kujifungua inavyotibiwa

Matibabu ya anemia baada ya kujifungua inajumuisha mabadiliko ya mlo na maisha yako. Vifuatavyo ni vidokezo 11 vya kukusaidia:

  • Tumia virutubisho vya madini ya chuma, kuimarisha viwango vya madini chuma kwenye damu.
  • Kula vyakula vyenye madini chuma kwa wingi navyo ni kama: mboga za kijani kama spinachi, maharage,boga, nafaka, mchele wa kahawia, viazi,nyama, kuku,matunda kama strawberi na vyakula vingine vya asili.
  • Punguza matumizi ya chai, chai ina “tannin” inayopunguza kasi ya madini ya chuma kufyonzwa ndani ya mwili. Pia ulaji wa ya vyakula vyenye kalsiamu unapunguza kasi ya ufyonzaji wa madini ya chuma ndani ya mwili.
  • Kula vyakula vyenye vitamin C vitakusaidia kuongeza ufyonzaji wa madini chuma ndani ya mwili. Matunda kama machungwa na strawberi ni vyanzo vizuri.
  • Kunywa vimiminika zaidi ili mwili wako uwe na maji ya kutosha itayosaidia kuimarisha usambaaji wa damu baada ya kujifungua. Vimiminika kama maji vinasaidia kupunguza damu kuganda na maambukizi ya kibofu cha mkojo (UTI). Kunywa angalau lita mbili za maji kwa siku. Maji yanasaidia kulainisha kinyesi na kuzuia kukosa choo.
  • Pata mapumziko ya kutosha
  • Maambukizi ya mwili yataongezeka ikiwa kinga ya mwili itapungua. Madini ya chuma yanapopungua mwilini, onana na daktari mapema kupata antibaiotiki.
  • Muone daktari mapema kama umepata anemia baada ya kujifungua. Fanya vipimo vya damu itamsaidia daktari kujua hali yako na kuchukua hatua stahiki.

Tumbo Lako Baada ya Kujifungua

Kwanini naoneka kama bado nina ujauzito?

Itachukua muda mwili wako kurudia hali yake ya awali, haswa tumbo lako baada ya ujauzito.Umeshajifungua lakini utaonekana kama bado una ujauzito wa miezi sita, ndani ya tumbo lililobonyea-bonyea na kubwa.

Ili kuelewa zaidi, chukulia tumbo lako kama pulizo linalojaa kadiri mtoto anavyokua tumboni. Kujifungua hakumaanishi pulizo linapasuka ila linaanza kuisha upepo taratibu. Kupungua kwa ukubwa wa tumbo lako kunaweza chukua mda lakini kutafanikiwa.

Tangu mtoto anapozaliwa,mabadiliko ya homoni yatasababisha tumbo lako lipungue ukubwa. Itachukua karibu wiki nne kwa mfuko wa uzazii kujibana na kurudia hali yake ya kawaida.

Seli za mwili zilizojazwa wakati wa ujauzito zitaanza kutolewa nje ya mwili kwa mfumo wa mkojo, uchafu ukeni, jasho. Na mafuta ya mwili ya ziada yataanza kupungua kwaajili ya kumlishia mtoto,yataanza kuunguzwa, hususani kama unanyonyesha na kufanya mazoezi. Itachukua angalau wiki kadhaa kuona matokeo. Baada ya kujifungua mstari mweusi uliopo tumboni ujulikanao kama “linea nigra” bado utaonekana pamoja na michirizi.

Mstari huu (linea nigra) unasababishwa na rangi ndani ya ngozi ambapo misuli ya tumbo lako imevutwa na kuachanishwa, ili mtoto apate nafasi ya kuishi kadiri anavyoendelea kukua. Mstari huu unapotea miezi michache baada ya kujifungua.

Michirizi inasababishwa na kunyooshwa kwa ngozi ya tumboni kumudu ukuaji wa haraka wa mwili wako kipindi cha ujauzito. Michirizi hii inaweza kuwepo kwenye tumbo,makalio,mapaja na matiti.

Je, itachukua mda gani tumbo langu kurudia hali yake ya awali?

Tumesikia stori nyingi za wanamama wapya waliorudia miili yao ya awali ndani ya wiki chache. Japokuwa inawezekana lakini haitokei kwa wamama wote.  Kumbuka! Mwili wako unaweza badilika umbile lake baada ya ujauzito. Inaweza kuwa ngumu kurudia umbile lako na uzito wako wa awali.

Uvumilivu ndio ufunguo. Ilichukua miezi tisa misuli ya tumbo lako kunyooka ili kumudu mtoto mzima ndani yake. Hivyo ni sawa kuchukua muda na muda zaidi kukaza tena katika hali yake ya awali.

Kasi na digrii ya kukaza kwa tumbo kunategemea yafuatayo:

  • Umbile na ukubwa gani uliokua nao kabla ya kubeba mimba
  • Kiasi gani cha uzito uliongezeka wakati wa ujauzito
  • Unafanya kazi kiasi gani
  • Jeni (gene) zako ulizorithi

Utagundua kupoteza uzito ni rahisi kama;

  • Uliongezeka chini ya 13kg na ulifanya mazoezi mara kwa mara wakati wa ujauzito.
  • Kama unanyonyesha
  • Mtoto wako wa kwanza.

Unaweza kurudia uzito wako wa awali mpaka miezi sita baada ya mtoto kuzaliwa.

Nawezaje kupungua uzito na kufanya tumbo langu kuwa na muonekano mzuri?

Kunyonyesha inasaidia, hasa miezi ya kwanza baada ya kujifungua. Ikiwa unanyonyesha, utaunguza kalori za ziada zitakazo tengeneza maziwa –karibu 500 kwa siku. Unaweza kupoteza uzito mapema zaidi ya wamama wanaonyonyesha kwa chupa.

Kunyonyesha kunasababisha kubana misuli ya tumbo, na kuufanyisha mwili mzima mazoezi. Lakini kama unakula zaidi ya kuufanyisha mwili mazoezi ili kuunguza mafuta mwillini, utaongezeka uzito, hata kama unanyonyesha.

Ni sawa kupungua uzito wakati wa kunyonyesha. Mwili wako una ufanisi katika kutengeneza maziwa, na kupungua mpaka kilo 1 kwa wiki ambayo haina athari kwenye wingi wa maziwa unayotengeneza.

Walakini, kama una mtoto mdogo wa kuangalia unahitaji nguvu nyingi. Jaribu kupungua uzito baada ya kutoka kujifungua inaweza kuchelewesha kupona na kukufanya uhisi kuchoka zaidi. Na ni vema zaidi kuacha kujipunguza (diet). Subiri mpaka uchunguzi wa baada ya kujifungua utakapofanyika kabla ya kujaribu kupungua uzito.

Kula kwa afya, pamoja na mazoezi laini itakusaidia kurudia umbile lako. Vifuatavyo ni baadhi ya vitu vitakavyokusaidia kutunza uzito wenye afya:

  • Tenga muda wa kula kifungua kinywa.
  • Kula angalau sehemu tano ya matunda na mbogamboga.
  • Jumuisha vyakula vingi vyenye nyuzinyuzi (fiber) vitakavyosaidia usafirishaji wa chakula, kama vile shayiri, maharage, nafaka, mbegumbegu na mbogamboga.
  • Jumuisha vyakula vya ngano kama mkate, mchele, pasta au viazi kwenye milo yako.
  • Punguza vyakula vyenye fati nyingi na sukari kama biskuti na keki.

Nifanye nini kingine niweze kurudia tumbo langu la awali kabla ya ujauzito?

Mazoezi yanaweza kusaidi kukaza misuli ya tumboni na kuunguza kalori. Ikiwa ulikua unafanya mazoezi kipindi cha ujauzito mpaka mwisho unaweza kuanza kufanya mazoezi mepesi na kujinyoosha tangu mwanzo.

Kama uliacha kufanya mazoezi wakati wa ujauzito au wewe ni mgeni kwenye mazoezi ni vizuri ukaanza mazoezi taratibu zaidi.

Wamama wapya wanaweza kuanza na mazoezi ya sakafu ya nyonga na kufanyia kazi taratibu kupunguza tumbo la chini mara baada ya kujisikia wako tayari. Hii inaweza kukusadia kurudia umbile lako la awali na kupunguza tumbo.

Unaweza kumbeba mwanao na kuenda matembezi kidogo, hii itasaidia kuinua hisia na kufanya mazoezi mepesi ya mwili wako.

 

 

 

Njia 20 za Kupunguza Uzito Baada ya Kujifungua

Kwa sasa utakua unafurahia sana ujio wa kichanga chako, una furaha sana kuwa mama. Ujauzito umekupatia zawadi bora na ya milele, zawadi ya mtoto, lakini pia umekupatia kitu kingine cha ziada ambacho hujakipenda, nacho ni ongezeko la uzito kutokana na ujauzito.

Hakika utahitaji kupunguza uzito wa mwili wako lakini  hakikisha unafanya hivyo katika njia iliyo salama kinyume na hapo unaweza kumuumiza mtoto kwa kumkosesha chakula kama utajinyima chakula (diet) na kusababisha mtoto kukosa maziwa pia utaidhuru afya yako, ni vema kama utapunguza uzito zingatia njia asili na salama.

Zifuatazo ni njia 20 za kupunguza uzito baada ya kujifungua:

  1. Kula mara kwa mara

Unaweza kudhani kuacha kula ni njia sahihi ya kupunguza uzito kwa haraka lakini kwa bahati mbaya hii inaweza kuleta matokeo tofauti. Ukiwa kama mama mpya una mengi ya kuhofia kiasi kwamba mawazo yatazidi, utashindwa kula kwa usahihi, mawazo yataongezeka na kufanya uzito wako kuongezeka.

Hakikisha unakula mlo kamili na wenye afya kuliko kuacha kula kabisa. Hii inaweza kuwa njia bora ya kupunguza uzito.

  1. Kula mara nyingi kwa kiasi kidogo kidogo

Kuliko kula mara tatu kwa kiasi kikubwa kwa siku, kula milo sita katika kiasi kidogo kidogo. Weka kiasi kidogo cha chakula ambacho hautashiba kwa mara moja. Kula milo sita kuliko mitatu kwa siku pia itakusaidia mda wote kutokuhisi njaa.

  1. Kula vyakula vyenye kiasi kidogo cha mafuta.

Ukiwa tayari ni mama mpya mwili wako unahitaji virutubisho vya kutosha kwa ajili ya kulinda afya yako na kutengeneza maziwa kwa ajili ya mtoto. Epuka kula chakula ambacho kitakushibisha lakini kisiwe na kazi mwilini. Kula vyakula vyenye omega 3, asidi ya fati, kalsiam, protini, na vyakula vya nyuzi nyuzi kama samaki, nyama isiyo na mafuta,kuku, mayai,maharagwe,kunde,mtindi na vyakula vya mbegumbegu. Epuka vyakula vyenye mafuta mengi. Ulaji huu mzuri utasaidia kupunguza uzito.

  1. Kunywa maji mengi

Hakikisha unakunywa angalau glasi 8 hadi 10 za maji kila siku, hii itasaidia kutoa sumu mwilini. Kunywa maji kwa wingi kunasaidia kuondokana na ukosefu wa maji mwilini na kuimarisha metabolic (uvunjajivunjaji wa kemikali mwilini) ambayo husaidia kuweka sawa uzito wa mwili. Husisha vimiminika katika mlo wako wa kila siku kama vile maziwa, mchuzi, supu na maji ya matunda.

  1. Anza mazoezi

Ukiwa kama mama mpya una mengi ya kuzingatia lakini ni muhimu kuweka ratiba ya mazoezi katika ratiba yako ya siku. Zungumza na daktari kujua ni wakati gani sahihi kwako kufanya mazoezi. Fanya mazoezi mepesi nay a kawaida kuepuka uchovu na kujiumiza. Mazoezi ambayo unaweza kujaribu ni kama kutembea, kukimbia, kuogelea na yoga.

  1. Pata mapumziko

Ukiwa kama mama mpya si rahisi kulala kwa masaa8 moja kwa moja ila jitahidi upate mda wa kupumzika. Kukosa muda wa kupumzika kunaweza kuathiri “metabolic” yako na kukwamisha zoezi lako la kupunguza uzito. Jaribu kutafuta msaidizi wa kazi ili mtoto anapolala upate mda wa kupumzika pia, unaweza kumkamulia maziwa mtoto kwenye chupa na kumuonesha mwenza wako jinsi ya kumnywesha.

  1. Kupunguza uzito kwa kumtumia mwanao

Huna haja ya kwenda sehemu maalumu ya kufanyia mazoezi (gym) wala huhitaji mazoezi magumu. Unaweza kumtumia mwanao kupunguza uzito. Muweke mwanao kifuani ukiinama na kuinuka kila siku,hakikisha daktari amekubaliana na hilo hilo.Njia nyingine bora zaidi ni kumuweka mtoto mgongoni kisha panda na kushuka chini ukiwa umejilaza.

  1. Angalia vitafunwa unavyokula

Ukiwa kama mama mpya ambaye unanyonyesha utakua unahisi njaa zaidi kuliko mwanzo. Ina maana kwamba utahitaji vitu vya kutafuna zaidi. Vitafunwa unavokula vinaweza kupunguza au kuongeza uzito wako.Pamoja na chakula chenye afya, katika orodha ya vyakula vyako ni vizuri jumuisha na vitafunwa kama vile nazi, matunda yaliyokatwakatwa, aina zote za nafaka, viazi vitamu vilivokaangwa na mchanganyiko wa mtindi.

  1. Punguza mawazo

Kuwa mama mpya kunakuja na majukumua mengi pamoja na hofu, unapaswa kuwa mtulivu na kupunguza kuwaza. Mawazo yanaweza kukwamisha zoezi lako la kupunguza uzito hivyo ni vema kupunguza mawazo. Muombe mwenza wako  akusaidie katika uangalizi wa mtoto ili ujipe mda wa kupumzika uwezavo, pumzika ili upunguze mawazo au fanya vitu ambavo vitakusaidia kuondoa mawazo. Hii ni njia bora ya kupunguza uzito baada ya kujifungua.

  1. Kucheza

Kucheza kutasaidia kupunguza mafuta mwilini. Weka mziki au kitu chochote ambacho kinaweza wafurahisha wewe na mwanao na kufanya mcheze. Haijalishi kama unajua miondoko ya mziki au haujui, cheza hadi utoe jasho mwilini.

  1. Mchanganyo wa mtindi na vitafunwa

Unapojihisi uchovu na hamu ya kula kula jitahidi kula vitu vitamu vyenye afya. Weka mtindi kwenye jokofu pamoja na nazi na matunda yaliyokatwa katwa. Pia unaweza kuongeza vyakula kama vanilla na kutengeneza mchanganyo. Kula mchanganyiko wako wa mtindi. Inaweza kua njia bora ya kupunguza uzito.

  1. Kunywa maji kabla ya kupata chakula

Kama unajihisi unakula kwa kiasi kikubwa kuliko unavohitaji ni vema ukanywa maji kabla ya chakula, hili linaweza kuwa jibu sahihi. Taratibu kunywa maji glasi iliyojaa kabla ya kuanza kula chakula. Itasaidia kujaza tumbo na utakula kiasi cha chakula utakacho, kinyume cha kula sana utakula kiasi kinachohitajika mwilini na kujihisi umeshiba.

  1. Punguza baadhi ya vyakula

Kwa kawaida kuna mazingira unaweza kushawishika kula sana pasipo na maana. Anza kupunguza kula vitu ambavo havina msaada mwilini na katika afya yako. Kama unakula wali au kachumbali epuka jibini na utumie mboga za majani kwa wingi.

  1. Kula mapema

Jitahidi kula cha kula cha jioni dakika za mwisho za jioni na siyo usiku. Kama inawezekana kula chakula cha jioni saa 1 na saa 1 na dakika 30 jioni , uwe umemaliza kabla ya saa 2 usiku,hii itakuza  “metabolic” yako na kupelekea kupunguza uzito. Kama unakaa macho hadi majira ya usiku sana, kunywa  glasi ya maziwa au chai ya rangi. Kula mapema ni njia bora ya kupunguza uzito baada ya kujifungua.

  1. Tembea pindi uwezavyo

Kama una ratiba ya kufanya mazoezi katika ratiba yako ya siku unahitaji kufanya matembezi ya kawaida. Jaribu kutembea kadri uwezavo,hata kama utatakiwa kumchukua na mtoto. Unaweza kutembea na mtoto bustanini, katika viwanja vya mazoezi, madukani au sokoni, au unaweza kumlaza mikononi mwako wakati unaizunguka zunguka nyumba.

  1. Jipe muda mwenyewe

Uliongezeka uzito katika kipindi cha miezi tisa ya ujauzito hivo usifikirie kupungua kwa mda wa mwezi mmoja tuu baada ya kujifungua. Mwaka wa kwanza mtoto kuzaliwa utakua mwaka mgumu kwako na itakuchukua muda kupunguza uzito. Usikate tamaa na kupunguza kasi ya kufanya mazoezi hata kama unaona hupungui, endelea kufanya mazoezi sahihi na kwa utaratibu, usijipe mawazo endelea kujitahidi na kujipa moyo kuwa bado miezi michache ufike unapohitaji.

  1. Fanya manunuzi sahihi

Ni rahisi kupata matamanio vyakula vitamu kama chokleti vinapo kuwa mbele yako. Hakikisha unaepuka vitu vitamu kama chokolati,ice creams na vitafunwa vingine vinavoongeza uzito, kama unahisi kutamani vinapokua kwenye jokofu epuka kununua. Kama unadhani ni vitu pendwa sana kwako na utataka kununua utakapoviona,muombe mwenza wako afanye manunuzi kwa ajili yako.

  1. Epuka kahawa na vilevi

Unaweza kudhani kikombe cha kahawa kitakusaidia kuondoa usingizi lakini kinaweza kuzuia uzito kupungua. Hata ikiwa umeacha kunyonyesha epuka kunywa pombe au jaribu kunywa chini ya chupa 2 kwa wiki. Kama unajihisi uchovu na unatamani kunywa kitu, kunywa kikombe cha chai ya majani au kahawa.

  1. Pata chakula cha nyumbani

Ingawaje ni sawa kula nje, jitahidi upate chakula nyumbani kadri uwezavyo. Kula nje kunaweza kusababisha ukatamani kula chakula ambacho unajua si rafiki kwa uzito wako. Ikiwa utahitaji kula nje jitahidi ule mara moja kwa wiki au wiki mbili. Kula nyumbani ni njia bora ya kupunguza uzito baada ya kujifungua.

  1. Hamasika

Kama ulikua na gauni nzuri ulilopendelea kuvaa, weka mbele ya kabati au sehemu ambayo ni rahisi kuliona kila mara. Itakusaidia kufanya uhamasike zaidi kufikia lengo lako la kupungua uzito ili uweze kulivaa tena.

Namna ya Kuondoa Michirizi Baada ya Kujifungua

Michirizi ni kitu cha kawaida baada ya kujifungua. Utakua na mistari myembamba kwenye maeneo yenye mafuta mengi kama matiti, mapaja, tumbo na mengineyo. Huweza kutokea kutokana na mabadiliko ya homoni au kupotea kwa mafuta katika maeneo haya.

Je, inawezekana kuondoa michirizi?

Michirizi huwa myembamba kadiri ya muda unavyoenda lakini huwa haipotei. Kuna njia za asili za kuweza kuifanya isionekane kwa urahisi. Unaweza ukatumia mafuta ya “massage”, losheni, mafuta ya kulainisha ngozi nk.

Baaada ya miezi kadhaa au hata miaka michirizi hubadilika na kuwa myembamba na kufanana na ngozi

Namna ya kuondoa michirizi kiwa nyumbani

Kuna njia za nyumbani za kuondoa michirizi kwa uhakika mara baada ya kujifungua kama vile;

1. Matibabu ya mafuta

Kusugua maeneo yenye michirizi kwa mafuta huweza kusaidia kupunguza michirizi kwa kiwango kikubwa na kulainisha ngozi.

Mafuta ya olive: olive ni mafuta yenye kulainisha ngozi na pia husaidia kuzunguka kwa damu, na kupunguza michirizi kwa kiwango kikubwa.

  • Weka mafuta katika kiganja chako na taratibu sugua eneo lenye michirizi
  • Acha dakika 30 ili vitamin A,D,na E ziingie kwenye ngozi yako.
  • Oga baada ya kusugua.
  • Ingawa ni kitendo kinachochukua muda kitakupa matokeo unapokifanya kila mara
  • Au unaweza kuandaa mchanganyiko wa olive maji na “vinegar”ili upake usiku wakati wa kulala.

Mafuta ya nyonyo

  • Paka mafuta ya nyonyo kwenye michirizi na usugue taratibu kwa mduara.
  • Tumia mfuko wa plastiki ufunike uliposugua joto litafungua vinyweleo ili mafuta yaingie.
  • Safisha eneo husika na urudie kula siku, ndani ya mwezi mmoja tu, utapata matokeo mazuri.

Matibabu ya Mafuta muhimu

  • Chukua mafuta ya kawaida kama vile mafuta ya nazi
  • Dondosha matone kadhaa ya mafuta muhimu kama ya ua waridi
  • Tumia mchanganyiko huu kusugua kwenye michirizi ndani ya dakika 30 itasaidia kuondoa michirizi.

2. Aloe Vera

Aloe vera inasaidia kulainisha ngozi. Tumia inayopatikana fresh kuliko ile ya sokoni.

  • Paka juu ya ngozi, acha dakika 15 na safisha kwa kutumia maji ya uvugvugu. Rudia mara kwa mara.

3. Asali

Viwango vya viondoa sumu ndani ya asali husaidia kuondoa michirizi.

  • Chukua kipande cha nguo paka asali
  • Kiweke kipande hicho kwenye eneo lilioathiriwa acha mpaka ikauke
  • Safisha na maji ya vuguvugu
  • Au unaweza kuandaaa mchanganyiko wa asali na grycelin, upake kwenye michirizi na uache mpaka ukauke na uoshe na maji ya vugu vugu

4. Sehemu nyeupe ya yai

Maji meupe ya yai ni mazuri kwa protin na husaidia kufanya ngozi iwe na unyevu na kuonekana mpya.

  • Koroge ute mweupe wa yai na uma
  • Safisha eneo lenye michirizi na upake eneo kwa kutumia brashi laini
  • Acha ikauke
  • Paka mafuta ya olive kufanya ngozi iwe laini
  • Rudia kila siku japo kwa wiki mbili mpaka michirizi ianze kupotea.

5. Siagi ya nazi

Siagi ya nazi inaweza kutumika kama tiba, ni moja ya vilivyomo katika losheni  nyingi tu. Chukua siagi kidogo, na upake kwenye michirizi kila mara, na usuuze mara kwa mara.

Matibabu haya husaidia uvutikaji wa ngozi,kuzuia kukauka kwa ngozi na kupunguza michirizi.

6. Sukari

Sukari ni moja kati ya tiba muhimu za kuondoa michirizi, ambayo huondoa ngozi iliokufa na kufanya ngozi kung’aa

  • Chukua kijiko cha chakula cha sukari
  • Tumia kwa kusugulia kabla ya kwenda kuoga
  • Fanya kila siku ndani ya mwezi.

7. Juisi ya limao

Viwango vya asidi vilivyoko ndani ya limao huondoa michirizi

  • Paka juisi freshi ya limao kwenye eneo lenye michirizi
  • Acha kwa dakika 10 ili juisi iingie
  • Safisha na maji ya vuguvugu
  • Paka kila siku kwa matokeo mazuri
  • Au unaweza kupaka mchanganyiko wa limao na tano uliolingana kwenye eneo lililoathirika.

8. Maji

Ngozi yako lazima iwe na maji ya kutosha ili kuweza kuondoa alama za michirizi katika ngozi yako, hivyo kunywa maji japo glasi 10 au 12 kila siku ili kukinga ngozi yako na sumu mbalimbali. Achana na soda chai kahawa kwani huondoa maji mwilini.

9. Juisi ya viazi

Viazi vina kemikali zinazosaidia mwonekao wa ngozi

  • Kata kiazi vipande viwili, paka kiazi kwenye michirizi
  • Ruhusu juisi ya kiazi kuingia kwenye ngozi na uache ikauke
  • Safisha na maji ya vuguvugu
  • Na utaona mabadiliko ndani ya muda mchache.

10. Binzari na msandali (Sandalwood)

Vinajulikana kwa kuongeza mng’ao na hisia ya ngozi

  • Andaa kijiko kimoja cha “sandalwood” kwa kusugua kipande cha “sandalwood” kwenye maji
  • Andaa mchanganyiko laini wa mzizi wa binzari
  • Changanya vyote kwenye kiwango sawa
  • Acha ikauke japo asilimia sitini 60% alafu sugua kwenye ngozi yako
  • Rudia kila siku japo kwa miezi sita utaona mabadiliko.

11. Maziwa, sukari na maji ya kijani ya tango na limao

  • Changanya vijiko viwili vya maziwa , na uchanganye na matone ya juisi ya limao na tango, na nusu kijiko cha sukari
  • Weka mchanganyiko kwenye michirizi ndani ya dakika 5.
  • Safisha na maji ya vuguvugu
  • Paka maji ya nazi na uache yakauke mpaka utakapohisi kuvutika kwa ngozi
  • Alafu paka aloe vera
  • Unaweza kurudia kitendo hiki mara tatu kwa wiki ili kuondoa michirizi

 

Msongo wa Mawazo Baada ya Kujifungua

Msongo wa mawazo ni jambo la kawaida linalowapata angalau mwanamke (wamama wapya) mmoja kati ya nane. Dalili zake ni pamoja na kusikia mchovu, kulia, mwenye shahuku, mnyonge na mabadiliko ya kula na kulala hasa wiki ya tano za kwanza baada ya kujifungua. Wakati mwingine kuwa na huzuni, kushindwa kufurahia chochote, kukosa matumaini, kusikia mwenye hatia.

Matibabu ya msongo wa mawazo ni pamoja na matumizi ya dawa za kupunguza mawazo, ushauri nasaha au yote pamoja.

Chanzo cha msongo wa mawazo

Wataalamu hawajui kwanini baadhi ya wanawake wanapata msongo wa mawazo na wengine hawapati. Unaweza kuwa sawa kwa mtoto wako wa kwanza lakini ukapata msongo wa mawazo kwa mtoto wako wa pili.

Wakati mwingine mambo unayopitia kila siku yanakua mengi na kukufanya ushindwe kujiangalia wewe na mwanao vizuri, kula na kupumzika vizuri. Baadhi ya hali zinakufanya uone maisha magumu kukubaliana nayo, baadhi ya hali hizo ni kama:

  • Ulishawahi kupata msongo wa mawazo hapo awali katika ujauzito uliopita au una tatizo la kiafya la msongo wa mawazo.
  • Hakuna msaada mzuri kutoka kwa baba wa mtoto, familia na marafiki.
  • Kipato cha shida, na kulea mtoto inakua mzigo.
  • Ulipata shida wakati wa kujifungua
  • Kunyonyesha ni kazi ngumu kwako.
  • Kumbukumbu mbaya kama kufiwa na mzazi wako.

 

Jinsi gani ya kutibu msongo wa mawazo?

Kwa msaada kutoka kwa familia,marafiki na mkunga wako au mshauri wako wa afya, utapona. Kumbuka kuwa na msongo wa mawazo haimaanishi wewe ni mama mbaya. Msongo wa mawazo unaweza kutibiwa kwa njia zifuatazo:

  • Ushauri nasaha katika kliniki za mama na mtoto na kuongea na marafiki, familia na mwenza wako kukusaidia
  • Matumizi ya dawa za kupunguza shahuku na zinazosaidia kurudisha homini katika hali ya kawaida. Ongea na daktari kupata uelewa mzuri katika hatari na faida za kuhusika katika matumizi ya dawa hizi ikiwa unanyonyesha.

 

Nifanye nini niweze kushindana na msongo wa mawazo?

Jaribu kupata mapumziko ya kutosha

Lala au pumzika unapoweza. Ikiwa kuna mtu wa kukusaidia kumuangalia mtoto pumzika masaa kadhaa, sikiliza mziki unaopenda (kama unapenda mziki), kunywa kinywaji cha moto kisha pumzika.

Kula kwa afya, mlo kamili

Kwasababu ya mahitaji mapya ya mwili wako, kula vizuri ni jambo la muhimu. Usikae mda mrefu bila kula. Mlo kamili utaongeza nguvu ndani ya mwili wako na kuzuia uchovu.

Fanya mazoezi

Mazoezi yanasaidia kujisikia vizuri mwili na akili, japokua ni jambo la mwisho unalo jisikia kufanya. Mazoezi ya kujinyoosha ya yoga ni mazuri wakati huu pamoja na mazoezi mepesi uliyokua unafanya wakati wa ujauzito.

Kutana na wamama wapya wengine.

Katika kliniki za mtoto kukutana na wamama wengine itakusaidia kupata ujuzi na njia za kukubaliana na kipindi hiki.

Jipende

Kujiangalia na kujipenda wewe na mwanao ni mambo ya muhimu. Usijilundikie kazi nyingi zisizo muhimu kwako na kusahau kupumzika na kumuangalia mwanao.

 

Miadi ya Mama Mjamzito Baada ya Kujifungua

Vipimo gani ninaweza kufanyiwa?

Daktari wako anaweza kukupima shinikizo la damu na kushika tumbo lako kuangalia kama mfuko wa uzazi umejirudi na kujibana vizuri. Anaweza kukupima uzito na kukushauri njia tofauti za kupunguza uzito ulioongezeka kipindi cha ujauzito.

Anaweza kukupima zaidi upungufu wa damu, kidonda ulichochanwa wakati wa kujifungua. Kidonda cha operesheni na matiti yako kama atakua ana wasiwasi.

Unaweza kushindwa kujizuia hasa ukiwa unasikia mkojo au wakati mwingine kukosa choo.Kama ulichanwa sana wakati wa kujifungua kwa njia ya kawaida ili kuongeza njia ya mtoto, utagundua unajamba bila kutegemea au kujisaidia haja kubwa(kidogo). Mazoezi ya sakafu ya nyonga yanaweza kusaidia kurejesha udhibiti wa mwili wako na daktari anaweza kukuelekeza njia nzuri ya kufanya.

Daktari anaweza kukuliza unajisikiaje juu ya ujio wa mwanao. Anaweza kuuliza kama unapata msaada wa kutosha kutoka kwa ndugu zako. Huu ni wakati mzuri wa kuleta hoja yeyote inayokusumbua, sema pia kama una wasiwasi au una kosa mda wa kulala.

Ni salama kujamiana tena baada ya wiki sita?

Sio lazima, maana kuamua kuanza kufanya mapenzi tena ni jambo binafsi. Ikiwa una wasiwasi juu ya hili au ulijaribu ukapata maumivu ongea na daktari wako.

Hata kama hujaanza kujamiana tena, daktari atakuuliza kama utapendelea kutumia njia za uzazi wa mpango. Uwezo wako wa kupata ujauzito utarudi haraka, hasa kama hunyonyeshi, hata wanawake wanaonyonyesha mayai yao yanaanza kupevushwa baada ya miezi michache baada ya kujifungua.