Mtandao #1 kwa Afya ya Mama na Mtoto

Address:

P. O. Box 38995, Dar es Salaam, Tanzania

Zifahamu Aina Mbalimbali za Uzazi wa Mpango

Uzazi wa Mpango ni Nini?

Uzazi wa mpango ni maamuzi ya hiari ya mtu au wenza juu ya ni wakati gani waanze kuzaa, watoto wangapi wazae, wapishane kwa umri gani na lini waache kuzaa. Uzazi wa mpango unawahusu wenza wote wawili, kwahiyo ni vizuri kuliongelea hili pamoja. Hata hivyo chaguzi nyingi za uzazi wa mpango huanzia kwa mwanamke, kwahiyo ni muhimu kwa mwanamke kuamua kutumia njia ile itakayo kubaliana na mwili wake.

Uzazi wa Mpango una Faida Gani?

  • Pamoja na kumuwezesha mama na mtoto kuwa na afya njema, uzazi wa mpango una faida nyingi kwa wanawake, wanaume, watoto, familia na jamii kwa ujumla:
  • Unamsaidia mama kurudi katika hali yake ya zamani ambayo ilisumbuliwa na hali ya ujauzito, uchungu na kujifungua, mama atakuwa mwenye nguvu, afya nzuri na mchangamfu. Na pia atakuwa na muda mzuri wa kurudisha afya yake kabla ya kupata ujauzito mwingine.
  • Unamuwezesha kuhudumia familia yake vizuri na kuwa na maisha bora. Utakuwa na muda, fedha na mahitaji muhimu kwa familia yako kama chakula, mavazi, elimu, mapenzi na huduma zote muhimu. Mama anapata muda wa kutosha wakujishughulisha na mambo mengine ya kiuchumi na kimaendeleo kwa ajili ya familia na jamii kwa ujumla.
  • Mama na baba wanapata muda mzuri wa kujishughulisha zaidi na mambo na mahitaji yao binafsi.
  • Unasaidia kukuza uchumi na maendeleo ya nchi.

Nani Anapaswa Kutumia Uzazi wa Mpango?

Yoyote mwenye umri wa kuzaa au anatarajia kufikia umri huo anapaswa kufikiria kuhusu uzazi wa mpango. Uzazi wa mpango ni muhimu kwa:

  • Wanawake na wanaume
  • Watu walioa na kuolewa au ambao hawajaoa wala kuolewa
  • Watu wenye watoto au bado hawajapata watoto.

Ni Wakati Gani Mtu Atumie Uzazi wa Mpango?

Umri sahihi wa kuanza kutumia uzazi wa mpango ni kuanzia miaka ishirini (20) na thelathini na tano (35). Ujauzito ni hatari kwa mama na mtoto endapo mama atajifungua chini ya umri wa miaka ishirini (20) au zaidi ya miaka thelathini na tano (35) vilevile ni hatari kwa mama atakaejifungua zaidi ya watoto wanne au watoto wasipopishana. Wenza wanatakiwa kusubiri angalau miaka miwili kabla ya kupata mtoto mwingine pia wafikirie kutumia njia za kisasa za uzazi wa mpango wakati wote ambao hawajapanga kupata mtoto.

Njia za Uzazi wa Mpango ni Zipi?

Kuna njia nyingi za uzazi wa mpango ambazo zinaweza kutumiwa na mtu au wenza waweze kusubiri, kuchelewesha, au kupunguza idadi ya watoto watakaowazaa. Zipo njia za mda mfupi, mda mrefu na za kudumu.

Njia za muda mfupi

Hizi ni njia za kisasa za uzazi wa mpango ambazo unaweza kuzibadilisha. Unaweza kupata ujauzito pindi utakapoacha kuzitumia. Njia hizi ni nzuri kwa mama anayetaka kupata ujauzito baada ya miaka miwili baada ya kujifungua. Nazo ni:

Njia ya vichecheo-njia hizi zina vichocheo ni sawa na vichocheo vya kawaida vilivyomo kwenye mwili wa mwanamke.

Njia ya vidonge-vidonge hivi hutumiwa na wanawake kila siku. Vidonge vya uzazi wa mpango ambavyo hutumiwa na mwanamke huwa na homoni ambazo huepusha mwanamke kupata mimba kwa kuzuia yai la mwanamke kutokupevuka. Vidonge vya uzazi wa mpango havizuii maambukizi ya magonjwa ya ngono.

Njia ya sindano-mama huchoma sindano kila baada ya miezi mitatu (3). Sindano ni kama vidonge na kipandikizi huzuia yai la mwanamke kupevuka kwa kutoa homoni itakayo kukinga usipate mimba. Njia hizi hazitakuzuia kupata/ kuambukizwa magonjwa ya ngono.

Njia ya dharura ya vidonge vya uzazi wa mpango-humezwa na mama ili kuzuia kupata mimba kwa mama aliyejamiana bila kutumia kinga yeyote. Hivi vinaweza kuzuia mimba hadi siku tano baada ya kujamiana.

Njia za Kizuizi

Kondom za kike na kiume-ni muhimu kutumia ipasavyo kila unapofanya ngono. Hii ni njia pekee ya uzazi wa mpango ambayo inazuia vyote, mimba, magonjwa ya ngono ukiwemo virusi vya ukimwi. Zinazuia shahawa za mwanaume kuingia kwenye uke wa mwanamke.

Njia za asili

Kukosa hedhi kwa kunyonyesha mfululizo

Hii ni njia ya asili ambayo inatokea kwa mwanamke anayenyonyesha na ni ya kuaminika zaidi wakati mama huyo bado hajaanza kuona siku zake za hedhi na ili hayo yote yatokee ni lazima mama awe anamnyonyesha mwanae mara kwa mara usiku na mchana na mtoto awe na umri chini ya miezi sita (6).

Elimu ya kujua siku hatari katika uzazi

Hii inawezekana ikiwa mama anaufahamu mzunguko wake mzima wa siku zake za hedhi na kujua ni zipi siku za hatari za kushika mimba. Yeye na mwenza wanatakiwa kuacha kabisa kufanya ngono siku hizo za hatari.

Kukojoa nje

Hii inafanywa na mwanamume wakati wa tendo la ndoa ambapo humwaga shahawa zake nje ya uke.

Njia za muda mrefu

Hizi ni njia ambazo pia zinaweza kurudiwa. Unaweza kupata ujauzito mara utakapoacha kuzitumia. Hizi ni nzuri ikiwa unataka kusubiri zaidi ya miaka miwili kabla ya kupata mtoto mwingine.

Njia ya vipandikizi

Hiki ni kijiti cha plastiki (chenye urefu wa milimita nne) anachowekewa mwanamke chini ya ngozi kwenye mkono wake kinaweza kuwa kimoja au viwili. Hivi huzuia mwanamke asipate ujauzito kwa muda kati ya miaka 3 hadi 5 kutegemea na aina ya vipandikizi alivyotumia. Hutoa homoni ambazo hulizuia yai la mwanamke kupevuka na kukuepusha kupata mimba. Kipandikizi hiki kinauwezo wa kukaa kwa miaka mitatu hadi mitano lakini hakitakuzuia kupata/kuambukizwa magonjwa ya ngono.

Njia ya kitanzi

Ni kifaa kidogo chenye shaba na plastiki ambacho huwekwa kwenye mji wa mimba. Hichi hukuzuia usipate mimba mpaka miaka kumi na mbili (12), unaweza kukitoa wakati wowote utakapoamua au kuhitajia kupata mtoto.

Njia ya kudumu

Hizi ni njia huwezi kuzirudia na ukitumia huwezi kupata mtoto tena. Na hutumiwa na watu ambao hawataki kupata mtoto tena. Nazo ni;

Kufunga kizazi kwa mwanaume

Njia hii inahusisha upasuaji mdogo ambapo mirija ya uzazi ya mwanaume ukatwa au kufungwa hivyo kuzuia yai kusafiri na kukutana na shahawa. Mwanaume anaendelea kuwa na hamu ya kujamiiana na kutoa mbegu lakini mbegu zake hazitaweza kutunga mimba

Kufunga kizazi kwa mwanamke

Njia hii inahusisha upasuaji mdogo inafanyika kwa kuziba au kukata mirija ya kizazi kuzuia yai kukutana na mbegu. Mwanamke ataendelea kuwa na hamu ya kujamiiana na kuona siku zake za hedhi.

Utafahamu Vipi Kuwa Njia Gani ya Uzazi wa Mpango ni Sahihi Kwako?

Inategemea na mtu mwenyewe au wenza kuamua njia gani ni sahihi kwao. Tembelea kituo cha afya kilicho karibu nawe uonane na wahudumu wa afya wataweza kukufahamisha njia sahihi kwako.

Kumbuka sio njia hizi zote zinaweza kupatikana kila mahali, kwahiyo zungumza kuhusu njia hizi za uzazi wa mpango na muhudumu wa afya unaemwamini mahali ulipo

IMEPITIWA: OKTOBA, 2021.

Umuhimu wa Kunywa Maji Wakati wa Ujauzito.

Ninywe Maji Kiasi Gani Kila Siku Wakati wa Ujauzito?

Uhitaji wa maji wakati wa ujauzito ni mkubwa zaidi ili kuhakikisha mfumo wa mwili unaosimamia maisha ya viumbe wawili unafanya kazi vizuri. Ijapokuwa utofauti upo wa kiasi gani cha maji unywe kwa siku kutokana na sababu mbalimbali kama aina na ukubwa wa mwili wako na kwa kiasi gani unaushughulisha mwili wako, kwa ujumla angalau glasi 8 mpaka 12 za maji kwa siku.

Inashauriwa ukiwa unakunywa maji, kunywa kidogo kidogo badala ya kugugumia maji mengi kwa wakati mmoja hali ambayo inaweza kukufanya kujisikia vibaya. Unaweza kujaza chupa mbili za maji asubuhi na kuhakikisha uko karibu nazo kila wakati itakusaidia kukumbusha kunywa maji kila utakapoiona.

Hakikisha unakunywa maji kabla, wakati na baada ya mazoezi. Kumbuka kiu ni ishara mwili wako unaelekea kupata upungufu wa maji.

Faida za Kunywa Maji Wakati wa Ujauzito

Maji yanasaidia kuzuia kukosa choo

Sasa wewe ni mjamzito, kumbuka unakula na kutoa taka za watu wawili. Hii ina maanisha utoaji taka mwilini ni mkubwa kuliko hapo awali. Maji ya kutosha mwili yatasaidia kuyeyusha takamwili na mabaki, kisha kuzisafirisha nje ya mwili. Unywaji wa maji ya kutosha unasaidia kutoa haraka nje ya mwili mabaki ya chakula baada ya kumeng’enywa kupitia njia ya mfumo wa umeng’enyaji. Ikumbukwe tatizo la kukosa choo linawapata wajawazito wengi bila kusahau athari zake ambazo zinahusisha kuota nyama sehemu ya haja kubwa (hemorrhoids).

Maji yanasaidia kuzuia maambukizi katika njia ya mkojo (UTI)

Unywaji wa maji ya kutosha unazimua mkojo, hali ambayo inasaidia mkojo kutolewa nje haraka na kuzuia bakteria zinazosababisha maambukizi katika kibofu kuzaliana (bakteria hizi zinazaliana mkojo unapobanwa kwa muda mrefu kwenye kibofu). Pia mama anayekunywa maji ya kutosha hana hatari ya kupata maambukizi katika kibofu na figo.

Maji yanapunguza joto la mwili.

Ni kweli ukiwa mjamzito joto la mwili ni kubwa. Lakini ukinywa maji ya kutosha wakati wa ujauzito unasaidia kupooza mwili na kufanya mwili kufanya kazi vizuri.

Maji yanapambana dhidi ya uchovu.

Moja ya ishara za awali za upungufu wa maji mwilini ni uchovu. Unywaji wa maji ya kutosha unasaidi kuhakikisha tatizo la uchovu wakati wa ujauzito linadhibitiwa, vilevile maumivu ya kichwa (ishara nyingine ya upungufu wa maji mwilini). Pia maji yanasiadia mwili kutoa sodiamu iliyozidi mwilini- hali ambayo itapunguza miguu kuvimba “edema”.

Je, Vinywaji Gani Vingine Mjamzito Anaweza Kutumia?

Maji ndio kinywaji cha kwanza kizuri na salama kwa mjamzito, lakini vipo vimiminika vingine vinavyoweza kutumiwa na mjamzito kusaidia mwili wake uwe na maji ya kutosha:

  • Maziwa
  • Maji yaliyotiwa ladha (ladha ya limao)
  • Juisi safi na salama ya matunda na mbogamboga (kuwa makini na sukari inayoongezwa katika juisi ya matunda)
  • Chai zisizo na kafeini.

Kwa hali yeyote, weka kikomo cha unywaji wa soda na vinywaji vingine vilivyo na kafeini kwasababu vina dutu inayosababisha kasi na kiwango cha kukojoa kuongezeka.

Kumbuka pia, karibia asilimia 20 za maji yanayoingia mwilini yanatoka kwenye vyakula. Matunda yana maji ya kutosha.

Ishara Mwili Wako Una Upungufu wa Maji.

Mwili wako utakuonyesha hauna maji ya kutosha kwa kuangalia ishara zifuatazo:

  • Kiu na njaa
  • Midomo kukauka na kuchanika.
  • Mabadiliko ya rangi ya mkojo. Mwili ukiwa na maji ya kutosha mkojo wako utakuwa na rangi ya njano ya kupauka (yaani “pale-yellow color”). Wakati mkojo wenye rangi ya njano iliyokolea ni ishara ya kukosa maji ya kutosha mwilini.
  • Kupungua kwa safari za kwenda uwani
  • Kutotoka jasho hata wakati wa joto
  • Tatizo la kukosa choo au kupata choo kigumu
  • Uchovu, kizunguzungu na maumivu ya kichwa. Upungufu wa maji mwilini unasababisha uchovu na maumivu ya kichwa, hakikisha unakunywa maji ya kutosha kutunza nguvu uliyo nayo kwasababu ujauzito ni kazi kubwa inayohitaji nishati ya kutosha haswa miezi ya kwanza.
  • Kusahau, kuchanganyikiwa kushindwa kuelewa na kukosa mwelekeo ni baadhi ya dalili za mtu mwenye hali inayoitwa “brain fog”.
  • Ngozi mwili kukauka.
  • Baadhi ya wajawazito wanapitia leba ya uongo (Braxton Hicks contractions)

Dalili kama kizunguzungu na kuchanganyikiwa, mapigo kasi ya moyo, mabadiliko ya kucheza kwa mtoto tumboni,shinikizo dogo la damu, mshtuko na ogani kushindwa kufanya kazi zinawapata wajawazito walio na tatizo kubwa la ukosefu wa maji.

Vidokezo Vitakavyokusaidia Kuhakikisha mwili una Maji ya Kutosha Muda Wote

Zipo baadhi ya siku unaweza kuhitaji msaada kuhakikisha unafikia dozi yako ya kila siku ya maji. Vifuatavyo ni vidokezo vitakavyokusaidia kuendelea kunywa maji:

  • Ongeza ladha, unaweza kuongeza kipande cha tango, limao majani ya mnanaa (mint) katika maji.
  • Jaribu chai zenye majani ya mitishamba, hakikisha daktari au mkunga wako anakupa kibali cha kutumia kiungo hicho.
  • Hakikisha una chupa ya maji mkononi mwako. Ni rahisi kufuatilia unywaji wako wa maji ukiwa na chupa yako ya maji mkononi nyakati zote.
  • Anza siku kwa kunywa glasi moja ya maji. Kunywa maji mara baada ya kuamka ni njia nzuri ya kujijengea tabia ya kunywa maji.
  • Kula vyakula vyenye maji kwa wingi kama vile supu, tikitimaji, nanasi n.k.

Kumbuka

Ukosefu wa maji ya kutosha mwilini wakati wa ujauzito unaweza kuwa hatari kwa mama na mtoto tumboni.Inaweza kusababisha matatizo makubwa na hatari kwa afya kama vile:

  • Kupungua viwango vya maji yanayomzunguka mtoto ndani ya uterasi “amniotic fluid” ambayo ni muhimu katika maendeleo na ukuaji wa mtoto.
  • Mama kujifungua kabla ya wiki 37 za ujauzito kwasababu ya kupungua kwa “amniotic fluid”.
  • Mtoto kuzaliwa na kasoro za mirija ya neva za fahamu
  • Kiasi kidogo cha uzalishaji wa maziwa
  • Mtoto kuzaliwa na kasoro kwasababu ya ukosefu wa maji na virutubisho muhimu vya kumsaidia mtoto.
  • Mara chache,kukosa maji ya kutosha kunaweza hatarisha uhai au kusababisha mama kulazwa chumba cha wagonjwa mahutihuti.

IMEPITIWA: SEPTEMBA, 2021.

Kunyonyesha Ukiwa Mjamzito

Je, ni Sawa Kuendelea Kunyonyesha Mtoto Wakati una Mimba Nyingine?

Kunyonyesha kunasaidia kuzuia kupata ujauzito, lakini sio mara zote. Inategemea na vitu kama vile mara ngapi unanyonyesha mwanao na umri wa mtoto wako. Kumbuka, inawezekana kushika mimba tena huku unanyonyesha mtoto wako.

Ikiwa utagundua wewe ni mjamzito tena, iwe ulipanga au bila kupanga, utakuwa na maswali mengi- kama kuendelea kumnyonyesha mtoto kutaathiri ujauzito wako mpya, mtoto anayenyonya, utokaji wa maziwa na mwili wako.

Ikiwa mama akagundua kuwa ni mjamzito wakati bado ananyonyesha. Mtoto anayenyonyeshwa anaweza kuwa mdogo hajafikia umri wa kuachishwa au mama mwenyewe anakuwa bado anapenda kumnyonyesha mtoto wake. Ikiwa mimba ni ya kawaida na yenye afya, inapendekezwa kuwa ni salama kabisa kuendelea kunyonyesha katika kipindi chote cha ujauzito. Katika makala hii utajifunza mambo muhimu na mikakati thabiti unayotakiwa kujua kuhusu unyonyeshaji ukiwa mjamzito.

Je, Nimuachishe Mtoto Kunyonya Mara Baada ya Kugundua Nina Ujauzito Mwingine?

Ujauzito mpya ni sababu iliyozoeleka ya kumuachisha mtoto kunyonya. Baadhi ya watoto wanaacha wenyewe na baadhi ya kina mama wanawahamasisha watoto wao kuacha kunyonya ili kujiandaa kwa ujio wa mtoto mpya atakayezaliwa. Lakini ikumbukwe hakuna haja ya kumuachisha mtoto kwasababu umeshika ujauzito mwingine. Unaweza kuendelea kumnyonyesha. Unaweza pia kuamua kuwanyonyesha wote wawili- mtoto mkubwa na kichanga wako atakayezaliwa.

Usalama wa Kunyonyesha Wakati wa Ujauzito

Kama umegundua umeshika ujauzito mwingine, hakikisha unaongea na mkunga au daktari wako juu ya historia ya afya yako. Daktari atakusaidia kufanya maamuzi sahihi kuhusu kuendelea kunyonyesha au kumuachisha mwanao.

Kawaida kunyonyesha baada ya kugundua una ujauzito mpya ni salama kabisa. Ikiwa una afya nzuri na ujauzito wako hausababishi matatizo yeyote ya kiafya, unaweza kuendelea kunyonyesa. Ingawa, zipo baadhi ya hali daktari akizishuhudia katika afya yako atakushauri umwachishe mwano kunyonya.

Wakati unanyonyesha mwili wako unatoa kichocheo kinachoitwa “oxytocin”. Homoni hii inawaunganisha mtoto na mama na kuleta upendo, vilevile homoni hii inasababisha mibano na mikazo ya mfuko wa uzazi (uterasi). Mibano na mikazo (The Braxton Hicks Contractions) hii sio hatari kwa ujauzito wa kawaida na wenye afya.

Sababu Ambazo Daktari Atakushauri Umuachishe Mtoto Kunyonya

Daktari anaweza kuwa na wasiwasi na kukushauri umwachishe mtoto kunyonya kama:

  • Ujauzito wako uko katika hatari kubwa ya kutoka
  • Ulishapitia tatizo la mimba changa kuharibika au kutoka
  • Ulijifungua kabla ya mda katika ujauzito uliopita (kabla ya wiki ya 37)
  • Unapata maumivu ya tumbo yanayoambatana na kutoka damu ukeni
  • Una ujauzito wa mapacha au zaidi
  • Hauongezeki uzito sahihi wenye afya.

Je, Kunyonyesha Kunaweza Athiri Mtoto Aliye Tumboni?

Hakuna ushahidi kuwa kunyonyesha ukiwa mjamzito kutaumiza ujauzito wako mpya au kuingilia ukuaji na maendeleo ya mtoto anayekuwa tumboni. Mwili wako unaweza kutengeneza maziwa ya mtoto anaye endelea kunyonya huku ukimtoa virutubisho vyote anavyohitaji mtoto aliye tumboni. Vifuatavyo vidokezo muhimu unavyotakiwa kukumbuka:

  • Mwili wako unahitaji nishati ya kutosha ili kutengeneza maziwa, kutoa virutubisho muhimu kwaajili ya mtoto anayekua tumboni, na kukuweka mwenye afya na imara. Ili mwili wako kuwa na nguvu na kuepusha upungufu wa aina yeyote ya virutubisho muhimu, kunywa maji ya kutosha, kula mlo kamili ulio na nyongeza ya kalori zenye afya, na pata mapumziko ya ziada.
  • Ongea na daktari wako ikiwa una tatizo lolote la kiafya kama vile kisukari au anemia, ili kuhakikisha unapata virutubisho muhimu na kalori sahihi unazohitaji.
  • Hudhuria miadi yako kila mwezi na fanya uchunguzi mara kwa mara kila unapoweza, ni muhimu ili kuwa na uhakika kuwa ujauzito wako unaendelea vizuri na unaongezeka uzito kama inavyotakiwa.

Je, Ujauzito Wako Mpya Unaweza Kumuathiri Mtoto Anayenyonya?

Mabadiliko katika ladha ya maziwa na kupungua kwa kiwango cha maziwa huweza kumuathiri mtoto anayenyonya. Mambo haya mawili yanaweza kusababisha mtoto mwenyewe kukataa kunyonya. Ikiwa mtoto wako yuko chini ya mwaka mmoja, mabadiliko haya yaangaliwe kwa umakini zaidi ili kuhakikisha mtoto anapata virutubisho vya kutosha. Endelea kumnyonyesha ili asikose virutubisho muhimu kutoka kwenye maziwa ya mama. Lakini, ikiwa mtoto wako ni mkubwa na tayari kaanza kula vyakula vigumu na kula mwenyewe, mabadiliko ya ladha na kiwango cha maziwa hayawezi kumuathiri.

Mabadiliko ya ladha ya maziwa

Wakati mtoto wako amezaliwa, atapokea maziwa ya kwanza yanayoitwa “colostrum”. Kadiri ujauzito wako unavyoendelea kukua ndivyo ladha ya maziwa itakavyobadilika kuelekea kwenye “colostrum” kwaajili ya ujio wa mtoto mpya. Mambo machache unayotakiwa kujua kuhusu mabadiliko haya ni kuwa:

  • “Colostrum” imejaa kingamwili na virutubisho, hivyo ni nzuri kwa mtoto mkubwa anayenyonya. Lakini, mwili hautengenezi “colostrum” nyingi hakikisha kichanga wako anapata kwa wingi maziwa haya yenye kingamwili na virutubisho vya kutosha haswa kama utaamua kunyonyesha mtoto mkubwa na kichanga wako baada ya kujifungua.
  • Mtoto anaweza kuendelea kunyonya bila tatizo hata baada ya mabadiliko ya ladha ya maziwa, au anaweza asipende utofauti wa ladha na kuacha mwenyewe kunyonya.
  • Maziwa haya ya awali “colostrum” yanamsaidia mtoto mchanga kutoa kinyesi cha kwanza nje ya miili yao “meconium”, vilevile kwa mtoto mkubwa ambaye bado ananyonya anaweza kupata dalili za kuharisha kutokana na maziwa haya ya awali yaliyojaa virutubisho na kingamwili za kutosha.

Mabadiliko ya kiwango cha maziwa

Ujauzito ni moja ya sababu ya upungufu wa kiwango cha maziwa. Mambo machache unayotakiwa kujua ni kwamba:

  • Unaweza kuona kupungua kwa kiwango cha maziwa mara baada ya kushika ujauzito au baadae kidogo.
  • Ikiwa mtoto wako anayenyonya yuko chini ya mwaka mmoja na umegundua upungufu wa kiwango cha maziwa ongea na mkunga wako. Inaweza kukuhitaji kutumia maziwa ya fomula sambamba na kunyonyesha ili kuhakikisha mtoto anapata virutubisho anavyohitaji.
  • Kama mtoto wako ana umri zaidi ya mwaka mmoja, hakikisha anapata virutubisho anavyohitaji kutoka kwenye vyakula mbalimbali vigumu anavyokula. Unaweza kuendelea kumnyonyesha kama afya yako inaruhusu na mwanao yuko tayari kunyonya.
  • Upungufu wa kiwango cha maziwa unasababisha maziwa kutoka taratibu kwenye titi. Baadhi ya watoto wanakatishwa tamaa na hali hii na kuacha kunyonya wenyewe.

Je, Ujauzito Mpya Unaweza Kumuathiri Mama Anayenyonyesha?

Ingawa inawezekana kuendelea kunyonyesha wakati wa ujauzito, zipo changamoto. Zipo njia nyingi ambazo ujauzito unaweza kukuathiri kama mama anayenyonyesha. Zifuatazo ni baadhi ya changamoto unazoweza kupitia wakati wa kunyonyesha na vidokezo vitakavyokusaidia kukabiliana na changamoto hizo.

Kuvimba kwa matiti na chuchu.

Ujauzito unaweza kurejesha tatizo la kunyonyesha la zamani. Mabadiliko ya homoni yanayotokea wakati wa ujauzito yanaweza kusababisha tena maumivu ya chuchu na matiti. Kunyonyesha huku chuchu zimevimba kunaweza kuwa kugumu au kusababisha maumivu. Kwa bahati mbaya, suluhisho la chuchu zilizovimba wakati wa kunyonyesha halifanyi kazi wakati wa awali wa ujauzito kwasababu chanzo cha chuchu kuvimba ni mabadaliko ya vichocheo. Suluhisho la hali hii ni kuwa mvumilivu. Hali hii itadumu kwa miezi mitatu ya kwanza, japo kwa baadhi ya kina mama hali hii inaweza kuendelea kipindi chote cha ujauzito.

Unaweza kufanya yafuatayo ili kukabiliana na hali hii:

  • Weka kitu cha baridi juu ya chuchu zako
  • Vaa sidiria inayokufanya uwe huru (isikubane sana)
  • Jitahidi kumnyonyesha mtoto katika mazingira matulivu yatakayomfanya mtoto apunguze kuhangaika ili asisababishe kuvuta chuchu. Badala ya kumnyonyeshea sebuleni ambapo anaweza kubabaishwa na kelele za luninga au ndugu zake, nenda chumbani ambapo hakuna kelele au watu.
  • Jaribu mikao tofauti ya kunyonyesha.

Kuchoka

Ni kawaida kusikia uchovu kuliko kawaida ukiwa mjamzito kwasababu ya mabadiliko yote ya homoni yanayoendelea katika mwili wako. Kumlea mtoto mwingine na kumnyonyesha inaongezea uchovu huo. Kama unaweza, pata mapumziko ya kutosha. Inaweza kuwa ngumu haswa kama una mtoto anayetambaa au kukimbia kimbia, lakini fanya jitihada ya:

  • Kulala wakati mwanao akilala
  • Kaa kitako au lala kisha nyoosha miguu yako juu ukiwa unanyonyesha
  • Usiruke milo na kumbuka kunywa maji ya kutosha

Kadiri ujauzito unavyoendelea kukua, inakuwa ngumu kupata mkao mzuri wa kunyonyeshea mtoto wako. Fanya majaribio na tafuta mkao mpya utakaokupa unafuu wewe na mwanao. Pia unaweza kunyonyesha ukiwa umelala kwa ubavu.

Kumbuka

Wanawake wengi wanacha kunyonyesha mara baada ya kugundua wameshika ujauzito mwingine. Ikiwa hauko tayari, na daktari wako amekuhakikishia hakuna tatizo la kiafya linalokukabili hauna haja ya kumuachisha mwanao. Unaweza kuendelea kumnyonyesha mtoto wako kipindi chote cha ujauzito kwa usalama. Unaweza pia kuendelea kunyonyesha mwanao mkubwa hata baada ya kichanga wako kuzaliwa. Inaitwa “tandem nursing” kwa lugha ya kigeni.

Ni kweli, ujauzito unaleta kuvimba na maumivu ya matiti, kupungua kwa kiwango cha maziwa na uhitaji wa nishati ya zaidi mwilini. Ni rahisi kuchoka na kuelemewa. Unaweza kuamua kumuachisha mtoto wako kunyonya, na hii ni sawa kabisa. Ikumbukwe pia kuwa kipindi cha ujauzito kumuachisha mtoto kunyonya ni rahisi zaidi kwasababu ya mabadiliko ya ladha na kiwango cha maziwa, hivyo unaweza kuamua ni mda mzuri wa kuacha kunyonyesha. Fanya kile ambacho ni sahihi kwako na familia yako na usisikie hatia juu ya hilo.

IMEPITIWA: SEPTEMBA, 2021.

Kujifungua kwa Njia ya Kawaida Baada ya Kujifungua kwa Upasuaji (VBAC)

Ikiwa unajiuliza kama kujifungua kwa njia ya kawaida inawezekana baada ya kujifungua kwa njia ya upasuaji ujauzito uliopita, jibu ni kwamba inawezekana kwa wanawake wengi lakini kuna sababu zitakazo wasaidia wewe na daktari wako kufikia hitimisho kama inawezekana kwako au la.

Usalama kwako na mtoto wako ni jambo muhimu la kuzingatia. Kujifungua kwa kawaida baada ya kujifungua kwa upasuaji sio salama kwa kila mwanamke.

Ikiwa unajaribu kujifungua kwa njia ya kawaida unakuwa katika hatari kubwa ya kupata matatizo, ambayo yanaweza kusababisha utata wa afya ya wewe na mtoto wako- baadhi kuhatarisha maisha. Ndiyo maana ni muhimu kuongea na daktari wako kuhusu hatari hizi.

Ili daktari na wewe kufikiria uwezekano wa kujifungua kwa njia ya kawaida baada ya upasuaji, inakubidi wewe na mtoto wako muwe katika afya njema. Unaweza kujaribu kujifungua kwa kawaida hata ukiwa na ujauzito wa mapacha, cha msingi ni daktari kuhakikisha na kusema wote mko katika afya nzuri ya kuhimili zoezi zima.

Sababu hatari ambazo daktari hatakuruhusu kujifungua kwa kawaida baada ya kujifungua kwa upasuaji ujauzito uliopita ni pamoja na:

  • Uzito uliopitiliza (kama BMI yako ni 30 au zaidi)
  • Shinikizo kubwa la damu wakati wa ujauzito (Pre-eclampsia)
  • Umri mkubwa (kawaida zaidi ya 35)
  • Upasuaji wako wa awali ulifanyika miezi 19 iliyopita.
  • Mtoto wako tumboni ni mkubwa sana.
  • Kama wakati wa upasuaji ulichanwa kwa wima (vertical cut) hauruhusiwi kujaribu kujifungua kwa njia ya kawaida. Kuna nafasi kubwa ya mshono wako kuachia wakati wa kusukuma mtoto, hali ambayo italeta madhara makubwa kwako na mtoto wako. Itakubidi kufanyiwa upasuaji tena.

 Faida za Kujifungua kwa Njia ya Kawaida Baada ya Kujifungua kwa Upasuaji.

Asilimia 70 ya wanawake wanaojaribu kujifungua kwa njia ya kawaida wanafanikiwa, wengine inashindikana kwasababu ya dharura zinazotekea wakati wa kujaribu, wanaishia kufanyiwa upasuaji.

Unaweza kutamani kujaribu kujifungua kwa kawaida baada ya upasuaji kwasababu ya sababu mbalimbali, jaribio hili likifanikiwa kuna faida ambazo ni:

  • Hakuna upasuaji utakaofanyika
  • Kiasi kidogo cha damu kitapotea
  • Uponaji wa haraka
  • Inapunguza nafasi ya maambukizi
  • Sio rahisi kusumbuka na kidonda kwenye kibofu, utumbo au ogani nyingine.
  • Inapunguza nafasi ya kuwa na matatizo makubwa wakati wa kujifungua kwa ujauzito ujao.

Kumbuka

Sio kila hospitali inatoa huduma ya mjamzito kujifungua kwa njia ya kawaida baada ya upasuaji katika ujauzito wake wa awali, hivyo katika mpango wako wa kujifungua hakikisha unahusisha hospitali unayotarajia katika mkakati wako ili kujua kama inatoa huduma hiyo. Hata kama nafasi ya mshono uliopita kuachia wakati wa kusukuma ni ndogo, hospitali inatakiwa kujiandaa kwa hali yeyote ya dharura inayoweza kutokea. Baadhi ya hospitali hazina utayari wa vifaa na watu wenye ujuzi kukabiliana na hali ya dharura.

IMEPITIWA: SEPTEMBA, 2021.

Njia Mbalimbali za Kujifungua na Faida Zake

Kipindi hiki tofauti na zamani kumekuwa na njia mbali mbali za kujifungua. Hii intokana na maendeleo ya teknolojia na uwepo wa wataalamu mpaka kwenye vituo vya chini kabisa vya afya. Hali hii imesaidia kupunguza kwa kasi vifo vya mama na mtoto. Zifuatazo ni njia mbalimbali zinazotumika kujifungua. Ni vyema kuzitambua na kuzielewa mapema ili uweze kufahamu mapema ni njia gani ambayo itatumika wakati wa kujifungua kwako.

Ukweli Unaotakiwa Kujua Kuhusu Njia za Kujifungua

  • Chaguo zilizopo wakati wa kujifungua ni pamoja na: kujifungua bila msaada (kawaida), kujifungua kwa msaada na kujifungua kwa upasuaji.
  • Unaweza kujifungulia nyumbani, zahanati/kituo cha afya au hospitalini.
  • Kujifungua kwa njia ya kawaida bila dawa hakuna maumivu, ni rahisi kama mama atajifunza mbinu za kupumua wakati wa kusukuma mtoto katika chumba cha kujifungulia.
  • Katika kuhakikisha njia gani ni sahihi kwa mama wakati wa kujifungua upimaji wa faida na hasara za njia hiyo uende sambamba na pendekezo la mjamzito ambalo ni salama kwake.
  • Kila mwanamke ana uzoefu wa kipekee wakati wa kujifungua, wnaawake wengi wanakiri wakati wa kuzaa mtoto kuna amabatana na maumivu. Hata hivyo, maumivu hay ani ya mada mfupi, zipo aina na njia madhubutu za kupunguza ukali wa maumivu wakati wa kujifungua.

Kujifungua kwa Njia ya Kawaida (Kujifungua Bila Msaada- Unassisted birth)

Kujifungua kwa njia ya kawaida

Wewe na familia yako mnaweza kubaini ishara za kawaida za uchungu. Mwanamke anaweza kujifungua siku kadhaa au hata wiki kadhaa kabla au baada ya tarehe iliyotarajiwa, kulingana na tarehe ya kipindi cha mwisho cha hedhi ya kawaida. Mwanamke anapofahamu maana ya uchungu, ataweza kufahamu kitakachotokea. Ufahamu huu humsaidia kutulia zaidi na kuwa na ujasiri katika siku au wiki za mwisho za ujauzito.

Yafahamu maagizo dhahiri ya jambo la kufanya pale uchungu unapoanza (kwa mfano ikiwa utakuwa na maumivu ya mkakamao wa misuli ya fumbatio ya tumbo la uzazi au kuvuja kwa kilowevu cha amniotiki, maarufu kama kupasuka chupa). Hakikisha kuwa kuna mtu atakaye mwita mkunga au mtaalamu mwingine ili kukuzalisha haraka iwezekanavyo.

Mkunga wako anafaa kuzingatia maandalizi ya kujifungua na:

  • Kuheshimu chaguo la mama. Anapaswa kumpa mama habari zote zinazohitajika kuhusu uzalishaji safi na salama, lakini hatimaye anapaswa kuheshimu chaguo lake kuhusu mahali pa kujifungulia na mtu angelipenda kuandamana naye.
  • Kukusaidia kutambua mahali pa kupata usaidizi wakati wa kujifungua na kipindi cha baada ya kujifungua kinachofuata punde.
  • Kupangia gharama yoyote ya ziada inayohusiana na kujifungua kwako.
  • Kutayarisha vifaa vya kumtunza mama na mtoto wake atakayezaliwa.

Faida za Kujifungua kwa Njia ya Kawaida

  • Watoto wanaozaliwa kwa njia ya kawaida wanakuwa na matatizo madogo ya upumuaji.
  • Mama anapona haraka na kuepuka aina yeyote ya matatizo yanayohusiana na upasuaji kama vile uchanwaji wa utumbo au ogani za eneo la tumbo wakati wa upasuaji.
  • Njia hii ya kujifungua ina kiasi kidogo cha maambukizi na ukaaji mfupi hospitali au kituo cha afya.

Hasara za Kujifungua kwa Kawaida

  • Kuchanwa eneo kati ya njia ya haja kubwa na uke.

Njia za kujifungua kwa Msaada (Assisted Births)

Kujifungua kwa njia ya kawaida kwa msaada wa vifaa maalumu

Vifaa hivi huwasaidia akina mama na watoto pale watoto wanapotakiwa kuzaliwa haraka. Ni zana muhimu sana kwa mtu mwenye ujuzi wa kuzitumia.

Kifaa cha kunyonyea cha utupu (vacuum extractor) ni kifuniko kidogo cha kunyonyea ambacho hutosha kwenye kichwa cha mtoto kinachotokeza angali akiwa ndani ya uke. Hewa hujazwa ndani ya kile kifuniko ili kiweze kushikilia vizuri ngozi ya kichwa cha mtoto wakati mtaalam anapokivuta. Utaratibu huu unaweza kusababisha damu kuganda kwenye kichwa cha mtoto, kitaalam inaitwa (cephalohematoma)

Koleo hufanana na mikasi mirefu yenye bawaba ambayo mwishoni imejikunja ili kutosha kwenye kichwa cha mtoto. Kifaa hiki kinaweza kuleta madhara makubwa sana kwa watoto na mama vikitumiwa vibaya au vkitumiwa na mtu asiye na ujuzi.

Matumizi ya kifaa cha kunyonyea (vacuum-cup) yameongezeka. Sababu tatu zilizosababisha ongezeko la matumizi ya vifaa hivi ni kwasababu ya:

  • Ongezeko la matumizi ya dawa ya usingizi ya epidural, ambayo hurefusha hatua ya kusukuma
  • Muda maalum wa kusukuma uliotengwa kwa wanawake katika baadhi ya hospitali
  • Jitihada za hospitali kupunguza uwezekano wa kufanyiwa upasuaji.

Kifaa cha kunyonyea (vacuum-cup) mara nyingi hutumiwa pamoja na dawa ya ganzi ya mgongoni (epidural) kwa sababu ganzi huzuia hisia za kusukuma. Kama ulipewa dawa ya ganzi ya mgongoni (epidural), vuta subira mpaka mlango wa kizazi utakapokuwa umeshatanuka vya kutosha. Unaweza pia ukaongeza uwezekano wa kuepuka kujifungua kwa kutumia vifaa hivi au kwa upasuaji kwa kutoanza kusukuma haraka mpaka pale mlango wako wa kizazi unapokuwa umekamilika kutanuka. Kama utasubiri mpaka utakapohisi hali ya kusukuma, au kichwa cha mtoto wako kimezidi kutokeza,utakuwa na nguvu zaidi na unaweza kusukuma vizuri zaidi.

Kabla ya kutumia njia hii kama hakuna dharura yoyote, kaa mikao tofauti ambayo itasaidia kufungua nyonga zako. Jaribu kuchuchumaa au kutekenya chuchu ili kuongeza nguvu uchungu na kupata nguvu zaidi ya kusukuma.

Kuchanwa eneo kati ya uke na njia ya haja ndogo (Episiotomy). Hii ni aina nyingine ya kujifungua kwa njia ya kawaida kwa msaada ambapo madaktari watafanya utaratibu huu ikiwa wanataka kumtoa mtoto haraka.

Kitendo cha kupasua chupa ya maji ya uchungu (Amniotomy). Daktari kifaa maalum chenye muonekano wa ndoana (plastiki) kutengeneza uwazi katika “amniotic sac”.

Kuanzishiwa uchungu (Induced labor)-hali hii inatokea pale daktari anapokuanzishia uchungu kabla haujaanza wenyewe. Kitendo hichi kitapendekezwa ikiwa daktari ana wasiwasi na afya yako au mtoto wako.

Kujifungua kwa upasuaji mkubwa (Cesarean Section)

Kujifungua kwa njia ya upasuaji hutokea kwa sababu kadhaa. Kama mtoto ni mkubwa au mdogo sana, kama unajifungua mapema au baada ya muda wa kujifungua kupita, una umri mkubwa au ni mwoga sana, kuchoka sana kwa sababu ya ujauzito au kuchoka sana kwa sababu ya uchungu, kama una mapacha, kama mtoto alitanguliza makalio, au kama wakati uliopita alijifungua kwa upasuaji.

Kiwango cha watu wanaojifungua kwa njia ya upasuaji mkubwa kimeongezeka sana kwa kipindi cha miaka thelathini iliyopita. Kujifungua kwa upasuaji huhusisha upasuaji mkubwa wa tumbo. Lazima ufanyike hospitalini, mahali ambapo dawa ya nusu kaputi, dawa za kuua bakteria (antibiotiki), na damu ya akiba pia inapatikana. Kujifungua kwa upasuaji ni operesheni zinazookoa maisha wanapofanyiwa wanawake wenye matatizo fulani wakati wa kujifungua, ikiwa ni pamoja na matatizo ya kitovu (kamba ya kitovu kutangulia kichwa cha mtoto), kondo la nyuma linapoziba mlango wa uzazi (placenta previa), kondo la nyuma kushindwa kufanya kazi yake vizuri na kusababisha mtoto kushindwa kushuka kupitia kwenye fupa nyonga.

Kama unataka kujifungua kwa upasuaji mkubwa, utapelekwa kwenye chumba cha upasuaji, mahali ambapo utachomwa sindano ya dawa ya usingizi au utachomwa sindano ya ganzi kwenye uti wa mgongo (epidural) ili tumbo na miguu yako ife ganzi kabisa. Utaingiziwa Mpira wa kutolea mkojo ili kuhakikisha kibofu chako kinakuwa kitupu. Utaendelea kubaki macho. Kwa nadra sana wakati ambapo upasuaji unatakiwa ufanywe haraka sana, utachomwa sindano ya dawa ya nusu kaputi ili usinzie kwa sababu hufanya kazi kwa haraka zaidi kuliko ya uti wa mgongo (epidural).

Dawa ya nusu kaputi inapoanza kufanya kazi, daktari atakupasua kwa mlalo chini ya tumbo karibia kwenye kinena (Upasuaji wa wima hufanywa kwenye matukio ya dharura), upasuaji mwingine hufanyika tena kwenye misuli ya mlango wa kizazi ili kurahisisha mtoto kutoka. Halafu atamfyonza pua na mdomo mtoto wako, atakibana kitovu na kukikata na kuangalia upumuaji wa mtoto kama ni wa kawaida. Mambo yote yakienda vizuri, wewe na mwenzi wako mnaweza kumshikilia mtoto wenu wakati daktari akiendela kutoa kondo la nyuma na kushona kidonda. Utaratibu mzima huchukua muda wa saa moja. Kujifungua kwa upasuaji mkubwa kunaweza kuokoa maisha na kuboresha afya katika mazingira ya dharura, lakini sio kwamba ni njia ya kawaida tu ya kukimbilia kuchagua.

KUMBUKA

Vifaa vya kujifungua ambavyo mwanamke mjamzito na familia yake wanapaswa kushauriwa watayarishe kabla ya siku ya kujifungua ni:

  • Nguo safi kabisa za mama kulalia na za kumpangusa mtoto mzawa na kumfunika
  • Wembe mpya wa kukata kamba kitovu
  • Uzi safi mpya wa kufungia kitovu au kibana kitovu maalumu
  • Sabuni, kitambaa safi cha kusafishia na ikiwezekana, pombe tiba tiba ili kuepuka maambukizi
  • Maji safi ya kunywa, kumwosha mama mikono na mikono yako.
  • Ndoo tatu kubwa au bakuli.
  • Vifaa vya kutengenezea vinywaji vya kuongeza maji mwilini au chai.
  • Tochi ikiwa hakuna umeme katika eneo husika.

Kumbuka kuwa, matatizo yanayohusiana na ujauzito kama vile shinikizo la juu la damu na kuvuja damu yanaweza kutokea wakati wowote katika ujauzito, na ugonjwa wowote unaweza kutokea wakati wa ujauzito. Hali hizi zinapohisiwa katika awamu yoyote ya ujauzito, unapaswa kupatiwa rufaa mara moja na mkunga atakushauri kumuona  au kutafuta huduma ya kitabibu haraka iwapo dalili za hatari zitaonekana.

Katika hali ya dharura

Hakikisha kuwa wewe na mwenza wako pamoja na watu wengine katika familia wanajua mahali pa kutafuta usaidizi.

  • Fanya utaratibu wa usafiri
  • Akiba ya pesa za usafiri, dawa na matibabu mengine.
  • Nani ataandamana na wewe hadi kwenye kituo cha afya?
  • Nani ataangalia familia wakati mama hayupo.

Mwanamke mjamzito anaweza kuvuja damu kwa wingi wakati wa kujifungua au baada ya kuzaa hivyo anaweza kuhitaji kuongezewa damu. Hakikisha kuwa wewe au mume wako mmewatambua watu wazima wawili wenye afya watakaokubali kukutolea damu ikiwa mama atahitaji.  Na wasiliana na mtaalamu wa afya ili ahakikishe watu waliojitolea kutoa damu kuwa hawataathirika kwa kutoa damu, na kwamba afya yao kwa ujumla itakaguliwa kabla ya kutoa damu.

IMEPITIWA: SEPTEMBA, 2021.

Kujifungua kwa Njia ya Upasuaji

Kujifungua kwa njia ya upasuaji, kwa lugha ya kigeni “C-section” ni njia ya kujifungua mtoto kwa kuchana kuta za sehemu ya chini ya tumbo na mji wa mimba (uterasi) ili kutoa mtoto aliye kwenye mji wa mimba.

Katika kipindi fulani kabla uchungu kutokea mama anajua kwa uhakika atajifungua kwa njia fulani, lakini hali tofauti za kiafya zinaweza kubadilisha mpango huo.

Daktari au mkunga anaweza kuamua utajifungua kwa njia ya upasuaji mara moja ukiwa katika uchungu au ukiwa katika chumba cha kujifungua. Mabadiliko haya ya haraka yanaweza kutokea ikiwa afya yako au mtoto aliyeko tumboni imebadilika ghafla na kuwa mbaya, hivyo kufanya kujifungua kwa njia ya kawaida kuwe hatari kwa afya ya mama.

Ni busara kujifunza anachopitia mama wakati wa kujifungua kwa njia ya upasuaji hata kama sio mpango wako wa kujifungua, itakusaidia ikiwa mabadiliko yatatokea katika chumba cha kujifungulia na kuhitajika upasuaji ili kuokoa maisha yako na mtoto wako.

Kujifungua kwa njia ya upasuaji ni salama kwa mama na mtoto. Lakini ni upasuaji mkubwa, inashauriwa isichukuliwe kimzaha.

Aina za Kujifungua kwa Njia ya Upasuaji

Upasuaji Uliopangwa

Ikiwa unajua mapema utajifungua kwa njia ya upasuaji, unapata nafasi ya kujua tarehe ya kujifungua na kutopitia uchungu wa kuzaa. Kabla ya utaratibu huu kufanyika utapata dripu ili mwili wako uwe na dawa na majimaji. Utawekewa pia mpira wa mkojo kusaidia kukusanya mkojo katika kibofu chako kipindi cha upasuaji na wakati ukiendelea kupona wodini.

Kama utajua mapema kuwa utajifungua kwa upasuaji, utapata muda kwa kutosha kujitayarisha, lakini kama ni upasuaji wa dharura inaweza kukushtua. Utachomwa sindano ya kaputi kisha kulazwa kwenye kitanda cha upasuaji. Wakati mwingine inaweza ikahitajika kuchomwa sindano ya kaputi ambapo utakuwa hutambui kinachoendelea mpaka utakapoamka. Faida nyingine ni kwamba utaweza kumuona mtoto wako mara tu anapotolewa tumboni. Daktari atakuruhusu umbebe mara baada ya upasuaji kumalizika. Kama una mpango wa kumnyonyesha mtoto wako, unaweza kujaribu kumlisha mtoto. Lakini sio kila mama anapata nafasi ya kumbeba mtoto wake mara baada ya upasuaji.

Wakati mwingine watoto waliozaliwa kwa njia ya upasuaji wanapata shida ya upumuaji, hali hii inawafanya kuhitaji msaada kutoka kwa madaktari. Usiwe na wasiwasi utaweza kumbeba mtoto wako mara baada ya daktari kuamua kuwa ana afya nzuri na hali yake iko salama.

Baada ya mtoto kuzaliwa, daktari atatoa plasenta yako na kukushona. Utaratibu wote huu utachukua dakika 45 mpaka lisaa limoja tu.

Sababu za Upasuaji Uliopangwa

Daktari au mkunga wako anaweza kukupangia kujifungua kwa upasuaji siku ya kujifungua ikiwa una:

  • Aina fulani ya matatizo ya kiafya. Magonjwa makubwa kama magonjwa ya moyo, kusukari, shinikizo kubwa la damu au tatizo la kibofu cha mkojo ni baadhi ya matatizo yatakayofanya kujifungua kwa kawaida kuwe hatari kwa mwili wa mjamzito.
  • Maambukizi. Ikiwa wewe ni muathirika wa ugonjwa wa Ukimwi au una ugonjwa wa zinaa ambao haujapona, upasuaji wakati wa kujifungua ni jambo lisilo epukika. Hii ni kwasababu virusi vinavyosababisha magonjwa haya vinaweza ambukizwa kwa mtoto kipindi cha kujifungua.
  • Afya ya mtoto. Ugonjwa kurithi unaweza fanya safari ya mtoto kupita ukeni kuwa changamoto kwa mtoto wako.
  • Mtoto mkubwa.
  • Uzito wa mjamzito. Kuwa na uzito mkubwa au uzito uliopitiliza kunaongeza nafasi ya mjamzito kujifungua kwa njia ya upasuaji kwa sababu ya shida mbalimbali zinazoambatana na uzito mkubwa kama vile kisukari wakati wa ujauzito, lakini pia kwasababu wanawake wenye uzito mkubwa wa mwili wanapitia uchungu wa kuzaa unaochukua muda mrefu.
  • Mtoto akikaa mkao wa tofauti tumboni (breech position). Mtoto anapotanguliza miguu kwanza na ikashindikana kumgeuza, mkunga wako ataamua upasuaji ni lazima.
  • Ujauzito wa mapacha au zaidi.
  • Tatizo ya kondo la nyuma kujishikiza karibu na mlango wa kizazi. Pale kondo la nyuma limejishikiza karibu na shingo ya uzazi, sio rahisi kujifungua kwa njia ya kawaida kwasababu mtoto hatapita vizuri. Kawaida plasenta ina kazi ya kuingiza virutubisho kwa mtoto, kumpa hewa safi na kuondoa hewa chafu. Ikiwa plasenta imezuia kidogo au sana mlango wa uzazi (placenta previa) upasuaji ni njia pekee salama kwako na mtoto wako.
  • Kondo la nyuma kuachia kabla ya muda wa kujifungua (placenta abruption). Endapo kondo la nyuma limenyofoka au sehemu ndogo kuachana na ukuta wa kizazi, upasuaji wa haraka hauna budi kufanyika ili kuokoa maisha ya mtoto. Upasuaji ukichelewa kufanyika mtoto atazaliwa amechoka au wakati mwingine kufia tumboni kwasababu ya ukosefu wa virutubisho na hewa safi.
  • Matatizo mengine hatari ya kiafya. Matatizo kama ujauzito unaosababisha shinikizo kubwa la damu au shinikizo la damu linalokua taratibu na kuathiri mfumo wa kati wa fahamu na kusababisha mama kupoteza fahamu na wakati huohuo hakuna tiba inayofanya kazi. Mkunga wako atashauri upasuaji ili kulinda afya za wote.
  • Ombi la mama. Mjamzito anaweza kuomba kufanyiwa upasuaji kwasababu za kibinafsi. Mkunga anaweza kumzikiliza mama na kumshauri njia salama kulingana na ombi la mama.
  • Ikiwa ulijifungua kwa upasuaji ujauzito wa awali. Mama aliyejifungua kwa upasuaji ujauzito wake wa awali anaweza kujaribu kujifungua kwa njia ya kawaida endapo kovu limepona vizuri, afya yako iko salama na sababu iliyokufanya ukafanyiwa upasuaji katika ujauzito wako wa awali hazipo.
  • Upasuaji unafanyika ikiwa mtoto ni wa kipekee. Kwa wanandoa ambao wamepata shida katika kutafuta mtoto kwa muda mrefu, wanaweza kuamua upasuaji ufanyike wakati wa kujifungua ili kuhakikisha mama na mtoto hawapati madhara wakati wa kujifungua. Wanawake waliopata mimba ya kwanza kwenye umri mkubwa sana kwa mfano miaka zaidi ya 35, wanawake waliopata shida ya mimba kuharibika sana au mtoto kufariki wakati wa kujifungua huchagua upasuaji wakati wa kujifungua.

Upasuaji wa Dharura

Wakati wa upasuaji wa dharura, mambo machache yatabadilika ikiwa ni pamoja na kasi na uharaka wa operesheni. Daktari anaweza kumzalisha mtoto wako kwa dakika mbili baada ya kuchana uterasi yako (inachuka dakika 10 mpaka 15 kwa upasuaji uliopangwa).

Ikiwa mtoto wako anashida katika upumuaji au mapigo ya moyo hayako sawa, madaktari watahitaji kumtoa haraka ndani ya mji wa mimba na kumuwahisha hosspitali kwaajili ya huduma za kitabibu haraka ili aweze kuwa salama.

Katika upasuaji wa dharura kwa kawaida utachomwa sindano ya uti wa mgongo, itakayokufanya usisikie maumivu kuanzia kwenye nyonga kwenda chini. Au ukapigwa kaputi na kulala upasuaji mzima. Kwa bahati mbaya hutasikia au kumuona mtoto wako akiwa anazaliwa, ila hautasikia maumivu au mkandamizo wowote katika tumbo lako la uzazi. Habari njema ni kwamba, baada ya kuzinduka utaweza kumbeba, kumuona na kumlisha kichanga wako.

Upasuaji wa dharura unafanyika pale:

  • Ikiwa kitovu kitatoka nje kabla mtoto, hali hii itasababisha usambazaji wa hewa ya oksijeni kukatishwa.
  • Uterasi ikichanika.
  • Uchungu umechelewa kuanza au hauendi kama inavyotakiwa. Kutoendelea au kusimama kwa uchungu ni moja ya sababu kubwa inayopelekea wajawazito wengi kujifungua kwa upasuaji. Hali hii inapelekea shingo ya uzazi kutofunguka na kupelekea mtoto kushindwa kutoka. Kwa kawaida mkunga au daktari huangalia hali ya shingo ya kizazi mara kwa mara kwa kuingiza vidole viwili kupitia uke, kwa kufanya hivi atagundua kwa kiasi gani (sentimita) ngapi shingo ya uzazi imetanuka. Hii ni njia mojawapo ya kuangalia maendeleo ya uchungu.
  • Mjamzito kuchoka au mtoto kuchoka. Ikiwa daktari atakuona umechoka au kipimo maalum kinachowekwa kwenye tumbo kuangalia mapigo ya moyo ya mtoto kuonyesha dalili za mtoto kuchoka daktari ataamua upasuaji wa haraka ufanyike.

 Upasuaji wakati wa kujifungua unachukua muda gani?

Upasuaji ni haraka, procedure yenyewe inachukua dakika 10 au pungufu, ikifuatiwa na dakika nyingine 30 za kushona.

Nini hutokea wakati wa upasuaji?

Iwe ni upasuaji uliopangwa tangu awali au wa dharura, upasuaji wa kawaida unafuata mpango maalum.

Maandalizi na sindano ya nusu kaputi

Utafanyiwa vipimo vya damu ili kuangalia wingi wa dam una kundi la damu ili pale itakapotokea shida baada ya upasuaji damu iongozwe kiurahisi. Upasuaji unaanza kwa utaratibu wa dripu na sindano ya kaputi ili sehemu ya chini ya mwili ili usiweze kusikia maumivu na mgandamizo wowote lakini utakua macho na utafanikiwa kushuhudia pale mwanao anapotolewa ndani ya mji wa mimba. Kisha sehemu cha chini ya tumbo la uzazi litanyolewa (kama inahitajika) na kusafishwa kwa dawa maalum ya kuua vijidudu. Utawekwa mpira wa kukusanya mkojo kipindi cha upasuaji na wakati ukiendelea kupona wodini.

Ikiwa unahitajika kufanyiwa upasuaji wa dharura, utachomwa dawa ya kukufanya ulale kipindi kizima cha upasuaji ambayo mara nyingi huchukua dakika chache. Ukiamka utasikia kusinzia kwasababu ya dawa ya usingizi, utajisikia kichefuchefu na kuchoka sana. Unaweza pia kuwa na koo kavu iliyosababishwa na mrija wa kupeleka hewa kwenye mapafu unaowekwa wakati wa upasuaji.

Kuchanwa na kuzaa

Mara baada ya sehemu ya chini ya mwili kufa ganzi au kulala, daktari atachana kidogo kwenye sehemu ya chini ya tumbo-juu kidogo ya uke. Kovu la mchano huu hupotea kadiri mda unavyoenda ikiwa kazi ilifanyika kwa umakini. Daktari atachana tena ndani sehemu ya chini ya uterasi. Zipo aina mbili za michano:

Mchano mlalo. Unatumika kwa asilimia 95 wakati wa upasuaji, kwasababu misuli chini ya uterasi ni mwembamba hivyo damu kutoka kidogo. Pia sio rahisi kuachia wakati wa kujifungua kwa njia ya kawaida hapo baadae.

Mchano wima. Aina hii ya mchano inafanyika pale mtoto amekaa sehemu ya chini ya uterasi au amekaa katika mkao usio kawaida.

Baada ya hapo maji yanayopatikana tumboni mwa mama mjamzito yanayomzunguka mtoto kwenye hatua zake zote za ukuaji hufyonzwa nje, kisha mtoto wako atatolewa nje. Kwasababu uteute wa ziada haukutolewa vizuri nje ya njia ya hewa ya mtoto wako, ufyonzwaji wa ziada utahitajika ili kuhakikisha mapafu ya mwanao ni safi kabla ya kumsikia mtoto wako akilia kwa mara ya kwanza.

Kumbeba mtoto wako kwa mara ya kwanza

Baada ya kitovu kukatwa, daktari ataondoa placenta, kisha kukagua haraka ogani zako za uzazi kabla ya kuanza kukushona. Kisha ushonaji wa sehemu uliochanwa utafanyika, ambao unachukua dakika 30 au zaidi.

Utapokea dawa ya kupunguza nafasi ya kidonda kupata maambukizi na “oxytocin” ya kudhibiti damu kutoka na kusaidia uterasi kubana na kurudi katika hali yake ya awali katika dripu. Shinikizo lako la damu, mapigo ya moyo na kasi yako ya upumuaji na wingi wa damu inayotoka utaangaliwa mara kwa mara.

Kama utakuwa umejifungua kwa upasuaji utahitaji kuendelea kukaa hospitali kwa siku kadhaa uanze kupona. Kupona baada ya upasuaji ni sawa tu na kupona kwa upasuaji mwingine wa eneo la tumbo. Tofauti kubwa ni kwamba badala ya kupoteza kiungo kimoja kama figo au “appendix” unapata mtoto.

Mojawapo ya matatizo unayoweza kuyaona baada ya kujifungua ambayo ni ya kawaida ni kama hali ya kusikia maumivu kwenye uke, kutokwa na damu nzito nyeusi, matiti kuvimba, nywele kudondoka, uchovu na kutokwa jasho jingi.

Tegemea Yafuatayo Baada ya Kutoka Chumba cha Upasuaji.

Daktari wako atakuchunguza kwa karibu mpaka pale dalili zote za dawa za kuondoa maumivu zimeisha. Kumbukumbu zako zinaweza zikawa zinasumbua kama ulitumia dawa ya usingizi au nusu kaputi. Madhara ya sindano ya nusu kaputi inayochomwa kwenye uti wa mgongo huchukua muda mrefu zaidi kuliko madhara ya dawa za usingizi.

Baada ya dawa ya kuondoa maumivu kuisha utaanza kusikia kidonda kinauma. Ukali wa maumivu unategemea sababu tofauti, ikiwemo uwezo wako wa kusikia maumivu na kama una historia ya kujifungua kwa upasuaji hapo awali, kwani maumivu ya upasuaji wa pili na kuendelea huwa yanaonekana sio makubwa sana kama yale uliyoyasikia kwenye upasuaji wa kwanza. Utapewa dawa za maumivu kupambana na hali hii.

Unaweza ukasikia kichefuchefu, ambapo daktari atakupatia dawa itakayokuzuia kupata kichefuchefu au kutapika.

Nesi atakuwa anakuchunguza mara kwa mara. Atakuwa anachukua vipimo vyako muhimu (joto, shinikizo la damu (BP), na upumuaji). Atakuwa pia anaupima mkojo wako na chochote kinachotoka ukeni. Pia atakuwa anaangalia mfungo wa kidonga chako cha upasuaji, sehemu mfuko wako wa uzazi ulipo na ugumu wake na wakati huo huo akihakikisha mirija ya dripu na mpira wa mkojo ipo sehemu yake.

Kama hali yako itaendelea vizuri, utapelekwa kwenye wodi ndani ya masaa kadhaa baada ya upasuaji kufanyika. Uchunguzi wa vipimo vyako muhimu utafanyika kwa mara nyingine. Kama una uwezo wa kukojoa mwenyewe basi mpira wa mkojo utatolewa masaa 24 baada ya upasuaji.

Unaweza ukawa unasikia maumivu kwenye uke kama mwanamke aliyejifungua kwa njia ya kawaida. Hii isikupe wasiwasi maumivu haya ni kutokana na kukaza kwa misuli ya mfuko wako wa uzazi ukiwa unajirudia kwenye hali yake kabla ya ujauzito.

Dripu za maji zitatolewa na utaruhusuwa kuanza kutumia vinywaji kwa kunywa mwenyewe masaa 24 baada ya upasuaji (Huu ndio muda ambao utumbo wako utakuwa umeshaanza kusogeza chakula kawaida na kufanikiwa kutoa hewa chafu nje kwa njia ya kujamba). Taratibu utaruhusiwa kurudia mlo wako wa kawaida kadiri siku zinavyosogea. Mama wanaonyonyesha inabidi wapate maji ya kutosha mwilini.

Utategemea kutolewa nyuzi zako (Kama sio zile zinazoyeyuka zenyewe) ndani ya siku 4 hadi 6 baada ya upasuaji.

Mwishoni kabisa kama kila kitu kitakuwa kimeenda sawa kwako na mtoto, utaruhusiwa kurudi nyumbani ndani ya siku 3 hadi 7 baada ya upasuaji.

Hali gani hatari za kiafya zinazoweza kutokea baada ya kujifungua kwa upasuaji?

Kujifungua kwa njia ya upasuaji ni salama kabisa, lakini mara chache matatizo ya kiafya yanatokea kwa mama na mtoto baada ya upasuaji kufanyika.

Kwa mama, matatizo haya ni pamoja:

  • Kupoteza damu,
  • Mama kupata maambukizi eneo la mshono.
  • Muitikio mbaya wa dawa zinazotumika kipindi cha upasuaji (dawa za nusu kaputi, dawa za kupunguza maumivu n.k).
  • Kujeruhiwa wakati wa upasuaji,
  • Damu kuganda kwenye mishipa ya damu haswa miguuni,viungo ndani ya nyonga na mapafu. Huku madaktari wakifanya kila namna kuhakikisha hali hii haitokei, ni vizuri ukatembea baada ya upasuaji kama unaweza.
  • Mara chache sana, uterasi inaweza kuvimba au kuwasha.
  • Maambukizi katika kuta za kizazi
  • Mama kupata hatari ya kujifungua kwa upasuaji upasuaji unaofuata.

Hatari za kiafya za muda mrefu ni pamoja na: kupata kovu baya kwenye eneo la mshono na kuchanika kizazi kwenye ujauzito unaofuata.

Mtoto aliyezaliwa kwa njia ya upasuaji anaweza:

  • Kupitia kipindi cha mpito cha kupumua haraka haraka, kitakachodumu kwa siku chache baada ya kujifungua, hali hii inasababishwa na mabaki ya maji (yanayopatikana ndani ya mji wa mimba kumzunguka mtoto kipindi chote cha ujauzito) ndani ya mapafu ya mtoto.
  • Kama upasuaji umefanyika kabala ya wiki ya 39 ya ujauzito, mtoto atakuwa katika hatari kubwa ya kupata matatizo ya kupumua ikiwa mapafu yake hayajakua vizuri-lakini kumbuka daktari atakua karibu nawe kumuangalia kwa ukaribu zaidi na kutibu aina yoyote ya tatizo litakalozuka ukiwa bado hospitalini.

Kumbuka

Ukishuhudia ongezeko la maumivu ya nyonga, kutokwa uchafu usio wa kawaida au homa baada ya mtoto kuzaliwa, wasiliana na daktari wako mara moja.

IMEPITIWA: AGUSTI, 2021.

Umuhimu wa Lishe Bora kwa Mjamzito Kabla ya Kujifungua.

Vitamini unazotumia kabla ya kujifungua zina virutubisho vingi mtoto wako anavyohitaji, hivyo basi kuna umuhimu gani waa mama mjamzito kuangalia kwa makini lishe yake?

Inaathiri afya ya mtoto wako maishani: Kila unachokula ukiwa mjamzito kinamuathiri mtoto na maisha yake kwa ujumla, hivyo ni muhimu kula vizui kwa manufaa ya mtoto hapo baadae. Kuna baadhi ya tafiti zinazoshauri ulaji wa vyakula vyenye chumvi, mafuta na sukari vinaathiri mapendekezo ya ladha ya mtoto hapo baadae. Hii inaweza kumsababisha mtoto kupata changamoto katika ulaji, afya na uzito kutokana na aina ya lishe uliyomtambulisha ukiwa mjamzito.

Chakula kinasaidia mwili kufyonza virutubisho vyenye afya: Ikiwa unakula mlo kamili mwili wako una nafasi kubwa ya kupata na kufyonza virutubisho na madini yanayohitajika katika mwili.

Chakula bora kinasaidia mwili kufanya kazi vizuri: Ukiwa unakula vizuri mwili wako utakushukuru. Utakuwa na nguvu ya kutosha, utajisikia vizuri na pengine kuepuka kero, usumbufu na maumivu ya kawaida ya ujauzito.

Aina za Matunda Mazuri Wakati wa Ujauzito

Ndizi

Ndizi ni chakula kizuri sana wakati wa ujauzito. Zinashibisha na zina viwango vikubwa vya madini ya kalishiamu na potasiamu ambayo yanasaidia matatizo ya misuli ya miguu kukaza. Ikiwa una hamu ya kitu chenye sukari kilicho salama kwako na mtoto tumboni, ndizi za kuiva ni chaguo sahihi. Lakini kama una kisukari kilichosababishwa na ubebaji mimba, chagua kula ndizi za kupikwa (mbichi).

Tufaha (apple)

Matunda haya yana vitamini A na C, maji ya kutosha na nyuzinyuzi (fiber) zitakazokusaidia kulainisha choo.

Tikiti Maji

Tunda hili lina kiwango kikubwa cha maji kuliko tunda linguine lolote-92%. Ikiwa unapambana na tatizo la kukosa maji mwili wakati wa ujauzito, unashauriwa kula tunda hili. Tikiti maji lina madini ya potasiamu, zinki na foliki asidi kwaajili ya kupambana na misuli ya miguu kukaza wakati wa usiku na kusaidia ukuaji wa uti wa mgongo wa mtoto tumboni.

Machungwa

Chungwa linaweza kuwa tamu au chachu, ladha hizi zina pendwa na wanawake wengi ambao wanasubuliwa na kichefuchefu wakati wa ujauzito. Yana kiwango kikubwa cha maji, ni chanzo kizuri sana cha vitamini C. Vitamini hii inachangia kukuza kinga yako na mtoto tumboni, na pia inasaidia kujenga tishu muhimu kwa ajili ya ukuaji wa kimwili wa mtoto.

Parachichi

Parachichi lina madini chuma,magnesiamu, potasiamu na nyuzinyuzi (fiber). Madini chuma yanayotumika kuzuia anemia, magnesiamu na potasiamu yanasaidia tatizo la misuli ya miguu kukaza na kichefuchefu. Parachichi ni chanzo cha fati unayotakiwa kupata ukiwa mjamzito.

Peasi

Ni chanzo kizuri cha nyuzinyuzi zinazosaidia kupambana na tatizo la kukosa choo. Ni chanzo kizuri pia cha vitamini C, pamoja na madini chuma, magnesiamu na foliki asidi.

Embe

Ni chanzo kizuri cha vitamini C na A, inayosaidia kukuza kinga ya mtoto.

Faida za Matunda Wakati wa Ujauzito

Je, unataka ujauzito salama na wenye afya?

Kuna sababu nyingi za kula matunda ukiwa mjamzito, nazo ni pamoja na:

Yanatoa virutubisho muhimu: Mtoto wako anahitaji virutubisho fulani ili kukua vizuri. Virutubisho vinavyotolewa na matunda ni pamoja na vitamini C na foliki. Vitamini C ni muhimu kujenga tishu, inasaidia kukuza kinga ya mwili ya mtoto na kuruhusu uhifadhi wa madini chuma yanayotumika kuzuia anemia. Foliki inasaidia kujenga uti wa mgongo na pia kumkinga mtoto anayekua dhidi ya kasoro katika neva za fahamu na hivyo kuepusha dosari katika ubongo, mgongo na uti wa mgongo (neural tube defects).

Yanasaidia kukidhi hamu ya vyakula vitamu: Utofauti mmojawapo wa matunda ni kuwa matamu au machachu, ladha zote hizi ni pendwa kwa wajawazito. Kuchagua tunda badala ya peremende au biskuti itakusaidia kumaliza hamu katika njia ya kuridhisha na salama kwa afya.

Ni chaguo zuri ukisikia kichefuchefu: Ikiwa unapata changamoto ya kichefuchefu wakati wa ujauzito, ni ngumu kuweka chakula tumboni kwa muda mrefu. Vyakula vitamu na baridi ni vizuri ikiwa una pambana na magonjwa ya asubuhi, hakikisha unatunza matunda ya kutosha kwenye friji kwaajili ya kifungua kinywa.

Yanasaidia kudhibiti sukari katika damu: Matunda yana nyuzinyuzi (fiber) zinazosaidia kuratibu ufyonzaji wa sukari katika mfumo wa damu.

Matunda yanakufanya uwe na maji ya kutosha mwilini: Unahitaji kunywa maji ya kutosha ukiwa mjamzito. Tunda lina zaidi ya asilimia 80 ya maji, hivyo ikiwa umechoka kunywa maji kila saa unaweza kuchagua kula matunda kuhakikisha mwili wako unakaa na maji.

Yanasaidia kukabiliana na tatizo la kukosa choo: Ukiwa mjamzito, umeng’enyaji wa chakula unakua polepole, hali hii inaweza sababisha kukosa choo- lalamiko la kawaida kipindi cha ujauzito. Ikiwa unatumia virutubisho vyenye madini ya chuma yanaweza kusababisha kukosa choo. Tatizo kubwa la kukosa choo linaweza kusababisha “hemorrhoids”. Njia nzuri ya kuondokana na tatizo la kukosa choo ni ulaji wa vyakula ambavyo ni vyanzo vizuri vya nyuzi nyuzi na kunywa maji (matunda yana vyote viwili-maji na nyuzi nyuzi).

Kiasi Gani cha Matunda Nile Nikiwa Mjamzito?

Ingawa ulaji wa matunda ni afya, lakini ikumbukwe matunda ni chanzo cha sukari, ambayo inatakiwa kuwekwa kikomo ukiwa mjamzito. Inashauriwa mjamzito kula matunda mara 2-4 kwa siku.

Je, Kuna Matunda Natakiwa Nisile Wakati wa Ujauzito?

Hakuna kikomo cha kula matunda ikiwa limeiva na safi. Ni muhimu kuhakikisha unasafisha vizuri matunda kabla ya kula ili kuepuka uchafu utakaosababisha ugonjwa. Mchanganyiko wa maji na vinegar ni mzuri na salama kusafishia matunda hasa yaliyokuzwa kwa kemikali za kiwandani (nyanya, tufaha, zabibu, peasi, strawberi n.k)

Kumbuka

  • Nanasi limepata sifa ya kusababisha mimba kutoka na kusadikika kuchochea uchungu kabla ya mda wa kujifungua. Ijapokuwa hakuna ushahidi wa kisayansi kuunga mkono madai haya, nanasi linajulikana kama tunda salama kutumia katika viwango sahihi wakati wa ujauzito.
  • Tunda pekee linalotakiwa kuepukwa ni papai bichi, papai ambalo halijaiva lina dutu ambayo inachochea mikazo ya mfuko wa mimba.

IMEPITIWA: JUNI,2021.

Ninawezaje Kuongeza Nafasi ya Kupata Mtoto wa Kike au Kiume?

Je, moyo wako unafarijika kila uonapo nguo ya mtoto wa kike au kiume dukani au sokoni?

Hakika unapata furaha ndani ya moyo wako ndio maana upo kusoma makala yetu hii. Makala hii itakujuza vidokezo mbalimbali vinavyoweza kuongeza nafasi ya kupata ujauzito wa mtoto wa kike au kiume. Jambo la kwanza unalotakiwa kujua ni kwamba njia hizi za kujaribu kupata mtoto wa kike au kiume hazihakikishi kufanikiwa na pia hazithibitishwi na ushaidi wa kisayansi.  Njia pekee ya kukuhakikishia kupata mtoto wa jinsia unayotaka ni kutumia utaratibu maalumu unaohusisha kupandikiza kiinitete (kike au kiume) ndani ya uterasi ya mama, njia hii inajulikana kama “IVF- in vitro fertilization”. Njia hii ni gharama sana na sio halali kwa baadhi ya nchi.  Hivyo basi sio mbaya kujaribu baadhi ya mbinu hizi hata kama hazikupati uhakika asilimia 100 wa kupata mtoto wa jinsia unayotaka.

Ni muhimu kujua kuwa mbegu ya mwanaume ndiyo inayotoa uamuzi wa jinsia ya mtoto. Ijapokuwa mbinu mbalimbali zinashauri vitu ambavyo wanandoa wanaweza kufanya ili kupata mtoto wa kike au kiume,mwisho wa siku uteuzi wa jinsia ya mtoto una amuliwa na mbegu ya kiume itakayolifikia yai la mwanamke. Mara baada ya urutubishaji kutokea, jinsia ya mtoto huamuliwa.

Vifuatavyo ni vidokezo vitakavyokusaidia kuongeza nafasi ya kupata mtoto wa kike au kiume:

Matumizi ya njia ya “Shettles”

Ingawa hakuna data zinazoweza kuthibitisha ufanisi wa njia hii inayoitwa “the shettles” baadhi ya wanandoa wamekiri imewasaidia na wengine wameamua kujaribu njia hii. Nadharia inayotumika hapa ni kwamba mbegu ya kiume inayobeba jinsia ya kike (X) inasafiri taratibu lakini pia ina nguvu na inaishi mda mrefu ukilinganisha na mbegu ya kiume iliyobeba jinsia ya kiume (Y) ambazo zinasafiri haraka sana lakini zinaishi kwa muda mfupi. Hii inamaanisha kwa wanandoa wanaofanya tendo la ndoa siku mbili mpaka tatu kabla ya siku yai linapevuka ndani ya mwili wa mwanamke, wanaweza kuongeza nafasi ya kupata mtoto wa kike. Hii ni kwasababu mbegu za kiume zenye jinsia ya kike zinaweza kuishi mda mrefu hadi kipindi yai linapevuka, siku chache baadae zitakuwa bado zinaishi ndani ya mirija ya uzazi.

Lakini kama unataka kupata ujauzito wa mtoto wa kiume, wanandoa wanashuriwa kufanya tendo la ndoa siku moja kabla ya “ovulation” au siku yai linapevuka kujishindia nafasi ya mwanamke kubeba ujauzito wa mtoto wa kiume, kwasababu mbegu hizi zina kasi zaidi hivyo ni rahisi kulifikia yai haraka zaidi. Utafiti unaonyesha njia hii inaweza kuongeza nafasi ya kupata mtoto wa kike kwa asilimia 75, ijapokuwa hakuna utafiti wa kisayansi unaothi itisha iwapo njia hii inafanya au haifanyi kazi.

Matumizi ya njia ya “Whelan”

Njia hii ilianzishwa na Elizabeth Whelan. Njia hii inafanana na “shettles” kwani zote mbili zinaamini muda ni kitu muhimu katika kutafuta mtoto wa jinsia fulani. Nadharia inayotumika hapa inashauri ikiwa unataka kupata mtoto wa kike fanya tendo la ndoa siku 2 au tatu kabla ya yai kupevuka au siku ya ovulation kabisa. Wazo linatumika hapa kuunga mkono nadharia hii ni kwamba mbegu zenye kubeba jinsia ya kike na kiume zinafanya kazi tofauti katika kipindi tofauti ndani ya mzunguko wa hedhi wa mwanamke. Mbegu za kiume zenye kromosomu X zinaweza kurutubisha yai zaidi katika kipindi hichi cha mzunguko. Hivyo basi ikiwa utakutana kimwili na mwenza wako siku chache kabla ya “ovulation” au siku ya “ovulation” mbegu hizi zina nafasi kubwa ya kuishi. Kulingana na mvumbuzi wa nadharia hii- Elizabeth, kiwango cha kufanikiwa kupata mtoto wa kike kwa kutumia njia hii ni asilimia 57.

Njia hii ya Whelan inategemea wazo la kwamba mabadiliko ya dutu za kemikali ndani ya mwili wa mwanamke katika kipindi fulani ndani ya mzunguko wake yanafanya mbegu zilizobeba jinsia ya kiume “Y”kurutubisha yai, na wakati mwingine dutu za kikemikali kuruhusu mbegu zilizobeba jinsia ya kike “X” kurutubisha yai. Hivyo basi, ikiwa unatamani kupata mtoto wa kiume, dhana inasema, wanandoa wajitahidi kukutana kimwili siku nne mpaka sita kabla ya ovulation. Mbali na kuwa na rekodi za kuonyesha njia hii inafanya kazi, wakosoaji wanasema kufanya tendo la ndoa siku nne mpaka sita kabla ya yai kupevuka ni mbali sana na mara nyingi mbegu zilizobeba jinsia ya kiume haziishi mda mrefu.

Mikao wakati wa kujamiana

Zipo dhana nyingi kuhusu aina fulani ya mikao itakusaidia kupata mtoto wa kike au kiume, lakini ijulikane kwamba hakuna ushahidi wa kisayansi unaoonyesha hivyo, lakini pia hakuna madhara ikiwa wewe na mwenza wako mkajaribu. Mikao inayoruhusu uume kupenya kwa kina ndani ya uke (deep penetration),itasaidia kupata mtoto wa kiume wakati mikao ile isiyoruhusu upenyo wa kina inasaidia kupata ujauzito wa mtoto wa kike (shallow penetration). Kukusaidia kujua zaidi kuhusu mikao hii, soma makala yetu ya “mikao mizuri ya kujamiana ili kupata ujauzito haraka”.

Kufika kileleni “Orgasm”

Wataalamu wa mambo ya uchaguzi wa jinsia wanashauri ili kupata ujauzito wa mtoto wa kike mwanamke anatakiwa asifike kileleni. Mwanamke akifika kileleni anatoa alkali ambayo inasaidia mbegu zilizbeba jinsia ya kiume kuishi zaidi kwa kutengeneza mazingira yasiyohatarishi. Bila alkali hii inayotolewa pindi mwanamke amefika kileleni, mbegu zilizobeba jinsia ya kiume hushindwa kuishi na zina nafasi ndogo ya kufika kwenye yai lililotolewa na ovari tayari kwa kurutubishwa. Mwanamke akifika kileleni inaongeza nafasi ya kupata mtoto wa kiume.

Vidokezo vinginevyo ikiwa unajaribu kupata mtoto wa kike ni pamoja na:

  • Kutana na mwenza wako kimwili mara kwa mara
  • Punguza chumvi katika milo yako
  • Kula vyakula vyenye asidi nyingi (machungwa, machenza,n.k)na epuka vyakula vyenye alkali kama vile tango, tofaa, parachichi na almond. Mbegu za kiume zilizobeba jinsia ya kiume haziwezi kuishi katika mazingira yenye aside, hivyo kuongeza wingi wa aside mwili kupitia chakula kunasaidia kubadilisha kiwango cha Ph ya uke wako. Vilevile ikiwa mnatafuta mtoto wa kiume ulaji wa vyakula vyenye alkali ya kutosha utasaidia kuishi vizuri kwa mbegu zilizobeba jinsia ya kiiume.

Je, Vyakula Gani Vitaongeza Nafasi ya Kupata Mtoto wa Kike?

Vyakula vinavyofikiriwa kuongeza nafasi ya kupata mtoto wa kike ni pamoja na:

  • Maharagwe
  • Mboga za majani zenye kijani kilichokolea
  • Almond
  • Vyakula vya baharini hasa dagaa
  • Bidhaa za maziwa kama vile jibini, maziwa na mtindi
  • Bamia
  • Matunda jamii ya machungwa
  • Mayai
  • Karanga ya kusaga
  • Korosho
  • Mbegu kama mbegu za maboga na chia
  • Spinachi
  • Shayiri
  • Apple
  • Matunda kama strawberi,zabibu

Je, Vyakula Gani Vitaongeza Nafasi ya Kupata mtoto wa Kiume?

Vyakula vinavyofikiriwa kuongeza nafasi ya kupata mtoto wa kiume ni pamoja na:

  • Vyakula vyenye potasiamu ya kutosha kama vile ndizi, parachichi,uyoga,apple,almond, samaki aina ya salmon
  • Vyakula vyenye alkali ya kutosha kama vile machungwa, machenza,
  • Matunda freshi na mbogamboga
  • Nafaka ambazo hazijakobolewa
  • Epuka bidhaa za maziwa

Kumbuka

Kwa kadri unavyotamani kupata mtoto wa kike au kiume, ukweli ni kwamba hakuna njia inayoweza kuahidi matokeo unayotaka. Na ukweli ni kwamba, hakuna madhara katika kujaribu njia hizi – lakini utafiti zaidi unahitajika ili kujua ufanisi wa mapendekezo haya. Bila kujali kama utapata mtoto wa kike au kiume, jambo muhimu ni kuwa na ujauzito salama na kujifungua mtoto mwenye afya.

IMEPITIWA: APRILI 2021

Kutoka Kwa Mimba Changa (Miscarriage)

Kutoka kwa mimba changa ni nini?

Miscarriage au kutoka kwa mimba changa ni kupoteza ujauzito kabla haujafikia wiki ya 20. Jina la kitaalamu kwa upotevu huu wa ujamzito mchanga ni “Spontaneous abortion” ikimaanisha “upotevu mimba wa ghafla”.

Zaidi ya asilimia 80 ya upotevu mimba changa hutokea katika miezi mitatu ya mwanzo ya ujauzito. Upotevu wa mimba ni vigumu kutokea baada ya wiki 20 za mwanzo za ujauzito kupita. Na kama ikitokea madaktari huita hali hii kama upotevu mimba uliochelewa “Late miscarriage”.

Dalili za upotevu mimba changa

Dalili za “miscarriage” ni pamoja na:

  • Kutoka kwa damu inayoanza kutoka kidogo kidogo na kuendelea mpaka kuanza kutoka kwa wingi
  • Maumivu makali ya tumbo la kukata (cramps)
  • Maumivu ya tumbo
  • Uchovu
  • Maumivu ya mgongo yanayoongezeka
  • Homa inayoambatana na dalili zozote kati ya hizo hapo juu
  • Kupungua uzito
  • Kutoka uchafu mweupe wenye upinki ukeni
  • Kukaza kwa misuli ya nyonga (contractions)
  • Kutoka kwa vinyama nyama kama damu iliyoganda kutoka ukeni
  • Dalili dhoofu za ujauzito

Kama una dalili kati ya hizo hapo juu ni vyema kuhudhuria kituo cha afya kwa ushauri Zaidi. Watakuambia kama ni dalili za dharura au kufanyiwa vipimo kuchunguza ujauzito wako kwa ujumla.

Nini husababisha upotevu wa mimba changa kutokea?

Mara kwa mara kutoka kwa mimba changa hutokea pale mtoto anaekua tumboni akiwa na matatizo ya kigenetiki. Matatizo haya hayana uhusiano na mama.

Matatizo mengine yanayoweza kusababisha uwezekano wa kutoka kwa mimba changa ni kama:

  • Maambukizi
  • Matatizo ya kiafya kwa mama kama ugonjwa wa kisukari au matatizo ya thairoidi
  • Matatizo ya mfumo wa homoni
  • Matatizo katika uitikiaji kinga mwili (Immune response)
  • Matatizo ya kimaumbile kwa mama
  • Matatizo katika umbo la mfuko wa kizazi
  • Uvutaji wa sigara
  • Unywaji wa pombe
  • Matumizi ya madawa ya kulevya
  • Kuwa kwenye uwepo wa ukaribu na mionzi au viambata sumu

Mwanamke anakuwa kwenye uwezekano mkubwa wa kupoteza mimba ikiwa changa kama:

  1. Ana umri zaidi ya miaka 35
  2. Ana matatito mengine ya kiafya kama kisukari na matatizo ya kithairoidi
  3. Ameshawahi kupata kupoteza mimba changa mara tatu au zaidi

Udhoofu au kulegea kwa mlango wa mfuko wa uzazi (Cervical Insufficiency)

Kutoka kwa mimba ikiwa changa mara nyingine hutokea pale mama mjamzito anapokuwa na udhoofu au ulegevu wa mlango wa kizazi. Hii inamaanisha mlango wa kizazi hauwezi kuhimili ujauzito kikamilifu na hivyo kufunguka na ujauzito kutoka kabla ya muda wake. Mara nyingi aina hii ya upotevu wa ujauzito mchanga hutokea katika hatua ya pili ya ujauzito. Huwa kuna dalili chache sana kabla ya upotevu wa aina hii kutokea. Unaweza ukahisi mkandamizo wa ghafla, unaweza ukavunja chupa (maji mengi kutoka ukeni), na nyama nyama pamoja na kondo la nyuma la ujauzito kutoka ukeni bila ya kupata maumivu makali.

Madaktari kwenye nchi zilizoendelea hutibu aina hii ya upotevu mimba changa kwa kushona nyuzi kwenye mlango wa kizazi kwenye ujauzito wako utakaofuata. Hufanya hivi kwenye walau wiki ya 12 ya ujauzito. Nyuzi hizi zitasaidia kuufanya mlango wa kizazi uendelee kufungwa mpaka utakapokaribia kujifungua ndipo nyuzi hizi hutolewa na utajifungua kawaida.

Aina za kutoka kwa mimba changa

Kuna aina mbalimbali za upotevu mimba changa, kama:

Upotevu mimba changa hatarishi. Hii hutokea pale unapokuwa unatokwa na damu na kuna hali ya hatari kwa mama kupoteza ujauzito wake lakini mlango wa kizazi haujafunguka. Katika hali hii kama sababu za kutokwa kwa damu zitatatuliwa basi ujauzito huendelea bila matatizo.

Upotevu mimba changa usioepukika. Hapa mama mjamzito hutokwa na damu na pia anakuwa na maumivu ya tumbo mkazo (crampings), na pia mfuko wa kizazi umefunguka. Uwezekano wa kutoka kwa mimba changa kwenye hali hii ni wa hali ya juu sana.

Upotevu mimba changa usiokamilika. Baadhi ya nyama nyama kutoka kwa mtoto wako na sehemu ya kondo la nyuma na mfuko wa mimba vinatoka nje ya uke na baadhi vinabaki ndani ya uke.

Upotevu mimba changa uliokamilika. Ujauzito wote unatoka nje ya mwili wako. Kila kitu kinatoka, yaani, mtoto, mfuko wa mimba na kondo la nyuma. Aina hii mara nyingi hutokea kabla ya wiki ya 12 ya ujauzito kufika.

Upotevu mimba ulionusurika. Aina hii inahusisha kifo cha kiini cha mimba lakini nyama nyama za ujauzito husika zinabaki kwenye mfuko wa uzazi bila kutoka nje.

Upotevu mimba changa unaojirudia rudia. Aina hii inatambulika pale unapopoteza mimba zaidi ya tatu mfululizo ambazo hazikufikia umri wa zaidi ya wiki 12. Aina hii ya upotevu mimba changa hutokea kwa asilimia moja tu (1%) ya wenza wanaojaribu kupata mtoto.

Daktari atatambuaje kwamba una tatizo la upotevu mimba changa?

Kuhakikisha kwamba umepata upotevu mimba changa, daktari wako atafanya yafuatayo:

  • Uchunguzi wa mlango wako wa kizazi kuangalia kama umefunguka
  • Kipimo cha “ultrasound” Hapa atajaribu kuangalia maendeleo ya mtoto tumboni na kutafuta mapigo ya moyo ya mtoto. Kama itashindikana kupata jibu la moja kwa moja kipimo hiki kinaweza kurudiwa baada ya wiki moja.
  • Vipimo vya damu. Hapa daktari ataangalia uwepo wa homoni za ujauzito kwenye damu yako na kulinganisha kiwango cha homoni hizi na vipimo vilivyofanywa hapo awali. Pia ataangalia wingi wa damu kama umekuwa ukitokwa na damu nyingi ukeni.
  • Vipimo vya vinyama vinyama vilivyotoka ukeni pia huweza kufanyika kama vilikuwa vinatoka. Hii husaidia kuwa na uhakika kwamba umepata upotevu mimba changa na pia kuweza kutambua kama kuna matatizo mengine yanayosababisha kupatwa na tatizo hili.
  • Kipimo cha kromosomu (chromosome test). Kipimo hiki kinaweza kufanyika kama wewe na mwenza wako mmepoteza zaidi ya mimba changa mbili mfululizo. Daktari atachunguza kama mfumo wenu wa genetiki ndio unaosababisha upotevu huu.

Matibabu ya upotevu mimba changa

Asilimia 85% ya wanawake wanaopata upotevu mimba changa hufanikiwa kupata ujauzito salama na kujifungua salama baadae. Kupata upotevu mimba changa haimaanishi una tatizo la uwezo wa kupata watoto. Kwa upande mwingine, karibia asilimia 1 mpaka 2 ya wanawake hupata upotevu mimba changa unaojirudia rudia. Yani mara tatu au zaidi. Baadhi ya watafiti wanaihusisha hali hii na magonjwa ya ukinzani wa kinga mwili binafsi (autoimmune diseases)

Kama umepata upotevu mimba changa mara mbili mfululizo, ni vyema kuacha kujaribu kupata ujauzito, tumia uzazi wa mpango na wasiliana na mtaalamu wa afya ili waweze kutambua sababu ya upotevu wako wa mimba changa mfululizo.

Kama upotevu wako wa mimba changa ni uliokamilika na mfuko wa uzazi ni mtupu, inawezekana hautahitaji matibabu zaidi.

Wakati mwingine sio tishu zote na nyama nyama hutoka nje ya mfuko wa uzazi. Kama hili litatokea, daktari wako atafanya “Dilation and Curretage”. Haya ni matibabu ambayo itambidi daktari aupanue mlango wa uzazi na kutoa kila kitu kilichabaki kwenye mfuko wa uzazi kwa umakini. Pia kuna madawa ambayo ukitumia husaidia kutoa tishu zilizobaki kwenye mwili ziweze kutoka nje.

Baada ya utokaji wa damu kuisha unaweza ukaendelea na shughuli zako za kila siku. Kama mlango wako wa uzazi umefunguka lakini ujauzito bado upo salama daktari wako ataweza kufunga mlango wa kizazi kwa kuushona ili kuepusha ujauzito kutoka mpaka pale wakati wa kujifungua utakapofika.

Kama kundi la damu yako ni lile lenye Rh hasi (Rh-), daktari wako anaweza akakupa chembechembe tiba za damu ziitwazo (Rh Immune Globulin). Hizi husaidia kuepusha wewe kutengeneza kinga mwili (antibodies) ambazo zinaweza zikamdhuru mwanao au mimba zijazo.

Unaweza ukafanyiwa vipimo vya damu, vipimo vya genetiki au madawa kama umeshapata upotevu mimba changa mara mbili mfululizo. Kuweza kuhakikisha kwamba una upotevu mimba changa mfululizo (recurrent miscarriages) daktari wako atafanya vipimo vifuatavyo:

  • “Ultrasound” ya nyonga
  • Hysterosalpingogram (Hii ni X-ray ya mfuko wa uzazi na mirija ya uzazi kwa pamoja)
  • Hysteroscopy (Daktari wako atatumia mrija mrefu mwembaba wenye mwanga na kamera kuingia kwenye mfuko wako wa uzazi kuweza kuona kama una matatizo yoyote)

Dalili mbalimbali baada ya kupata upotevu mimba changa

Kutoka kwa damu na hali ya kujisikia vibaya ni dalili mojawapo baada ya kupata upotevu mimba changa. Kama utakuwa na kutoka kwa damu nyingi ikiambatana na homa, mwili kutetemeka na maumivu makali, hudhuria kituo cha afya haraka kwani hizi ni dalili za maambukizi.

Pamoja na dalili za kimwili unaweza pia ukawa unajihisi kuwa na hisia za huzuni, kujilaumu na pia kuwa na wasiwasi kuhusu mimba zitakazofuata. Unachojisikia ni kawaida na ni vyema kupitia hatua hii ya huzuni kuliko kuipotezea mbali na kuiacha ikusononeshe ndani kwa ndani.

Kama unaweza na hautajali, ni vyema kuliongelea swala hili na watu wako wa karibu kama mwenza wako, rafiki au mwanafamilia uliyemzoea. Vikundi vya wamama waliopoteza mimba kwenye jamii vinaweza kuwa na manufaa makubwa kwako na kwa mwenza wako. Pia muulize daktari wako kama kuna taarifa au ushauri wa ziada ambao anaweza kukupatia. Kumbuka kila mtu anapona na kuhuzunika na kurudia hali yake ya kawaida tofauti. Hivyo usikate tamaa.

Kupata mimba tena baada ya upotevu wa mimba changa

Unaweza ukapata ujauzito tena baada ya upotevu wa mimba changa. Zaidi ya 85% ya wanawake waliojaribu mara moja baada ya kupoteza mimba changa walipata ujauzito na kuendelea na kuja kujifungua salama. Kuwa na upotevu wa mimba changa haimaanishi kwamba una tatizo kwenye uwezo wako wa kupata mtoto. Hivyo hivyo asilimia 1 mpaka 2 ya wanawake wanaweza wakapata upotevu mimba changa unaojirudia rudia (mara tatu au zaidi).

Kama umepata upotevu mimba changa mara mbili mfululizo, ni vyema kuacha kujaribu kupata ujauzito, tumia uzazi wa mpango na wasiliana na mtaalamu wa afya ili waweze kutambua sababu ya upotevu wako wa mimba changa mfululizo.

Ni wakati gani ujaribu kupata ujauzito tena baada ya kupoteza mimba changa

Ni vyema kufanya mazungumzo haya na daktari wako. Wataalamu wengine wa afya wanasema ni vyema kusubiria kwa muda fulani kabla ya kupata ujauzito mwingine. Muda kati ya mzungumko mmoja wa hedhi mpaka miezi mitatu kabla ya kufikiri kujaribu tena kupata ujauzito. Kuzuia upotevu mwingine wa mimba changa daktari wako anaweza kukupa matibabu kutumia “Progesterone”, homoni inayosaidia kiini mimba kujishika kwenye mfuko wa uzazi na kusaidia maendeleo yake kwenye hatua za mwanzo za ujauzito.

Kuchukua muda kupona kimwili na kiakili ni muhimu pia baada ya kupoteza mimba changa. Ni vyema kutokujilaumu na kujiona mwenye makosa. Hakikisha unapata msaada wa kimawazo na ushauri kujitayarisha na kuwa tayari pale utakapoweza kujaribu tena.

Je, utazuiaje kutokea kwa upotevu mimba changa?

Upotevu mimba changa mara nyingi hutokea kwa sababu kuna tatizo kwenye ujauzito husika. Huwezi kuzuia hili. Kama daktari wako atakupima na kuona tatizo, aina mbalimbali za matibabu zinapatikana.

Kama una ugonjwa, kuutibu ugonjwa husika kutaongeza uwezekano wa kupata ujauzito ulio salama na kujifungua bila matatizo. Njia bora unayoweza kuchukua mwenyewe ni kuhakikisha unakuwa mwenye afya kadiri uwezavyo kabla ya kujaribu kupata ujauzito:

  • Fanya mazoezi ya mara kwa mara
  • Kula mlo kamili na wenye afya
  • Zingatia kuwa kwenye uzito wako kiafya
  • Epuka maambukizi
  • Usivute, kunywa pombe au kutumia madawa ya kulevya
  • Punguza utumiaji mkubwa wa “caffeine” kama kahawa.

IMEPITIWA: MARCH 2021

Vidokezo vya Urembo Kipindi cha Ujauzito

Ni vipi nitaonekana mrembo kipindi cha ujauzito ni swali wanalokuja nalo wakina mama wengi. Kuna njia kumi sahihi za kukusaidia kufurahia urembo wako hasa katika kipindi maalumu maishani mwako.

  1. Kunywa maji

Kipindi cha ujauzito unahitajika kupata maji mengi kwa siku. Yatakusaidia kusafisha na kutoa taka na sumu mwilini mwako. Zaidi maji yanasaidia kutunza kiasi cha kimiminika kinachotakiwa mwilini mwako. Maji ni muhimu zaidi kwa afya yako na mwanao. Kunywa angalau lita 2 za maji kwa siku.

  1. Mlo sahihi

Unahitaji uangalizi na umakini wa ziada katika chakula unachokula wakati wa ujauzito na afya yako. Inashauriwa kumuhusisha daktari wako kukuandalia ratiba ya aina ya chakula unachotakiwa kula. Fuatilia ratiba hii kwa umakini, kula kwa afya, ikiwa pia ni muhimu kwa ajili ya mtoto wako.

  1. Pata muda wa kulala

Uchovu ni dalili moja wapo anazopata mama mjamzito hasa katika kipindi cha mwanzo. Kupumzika vizuri ni muhimu kwa ajili ya mwili na akili yako mwenyewe. Hakikisha unapata muda mzuri na wa kutosha kupumzika kiasi kwamba mwili wako uwe unahisi uchovu kidogo. Jiweke huru wakati wa kulala. Pumzika kwa usahihi, unaweza kutaka kutumia mito au kitu kingine cha kukuweka huru unapolala.

  1. Uzito sahihi

Unahitajika kuangalia uzito wako kipindi cha ujauzito. Baadhi ya wakina mama wanakula chochote na kila kitu pasipo kuhofia kuhusu uzito. Ikiwa ni kawaida kuongezeka uzito wakati wa ujauzito, si vema kiafya kuongezeka katika njia tofauti. Uzito unaongezeka kwa kula vyakula ambavyo havina msaada mwilini, mara kwa mara kula mlo sahihi, unaweza kumuhusisha daktari wako kwa machaguo bora.

  1. Mazoezi

Ndio, ni muhimu! Kuna mazoezi maalumu kwa ajili ya wajawazito. Hudhuria darasa la mazoezi ya yoga yaliyoandaliwa kwa ajili ya wajawazito, pata muda wa kukutana na wajawazito wengine na kujifunza na kupata uzoefu. Unaweza pia kumuomba ushauri daktari ni michezo gani unaweza kushiriki.

  1. Epuka michirizi

Wakina mama wengi wanalalamika kupata michirizi baada ya kujifungua. Unahitaji kuchukulia uangalizi hili wakati wa ujauzito.  Tumia cream uliyoshauriwa au zinazouzwa kwa ajili ya kuondoa michirizi. Tumia kila siku kuukanda mwili wako. Unaweza pia kutaka kuepuka kukimbia, kuruka au kugonga kama njia ya kuepuka michirizi.

  1. Thamini umbo lako

Pindi unatoka katika matembezi vaa nguo ya kuonyesha umbo lako, umbo la mwanamke ni zuri wakati wa ujauzito, ujauzito unamuongezea hipsi mwanamke. Tumia nafasi hii kuvaa nguo za kushika mwili wako vizuri ili kuonyesha vema hipsi zako.

  1. Uangalizi wa ngozi

Pamoja na yote wakati wa ujauzito, usisahau ngozi yako. Urembo katika kipindi cha ujauzito ikiwemo urembo wa ngozi, kwa kupendelea mimea tiba katika kipindi sahihi. Kutokana na mabadiliko ya homoni kunaweza kuwa na athari kidogo katika ngozi yako. Unaeza kutumia bidhaa za kulinda ngozi kwa kuzingatia aina ya ngozi yako lakini hakikisha hutumii kemikali hatarishi.

  1. Make-Up

Mwanamke hachukizwi na make up! kutokana na mabadiliko ya homoni unaweza kupata madoa usoni hivyo poda ni mkombozi. Make up ndio mkombozi, tena angalia zile ambazo hazitumii kemikali kali.

  1. Pumzika

Mwisho na muhimu zaidi ni kukumbuka kupumzika, weka mapumziko katika ratiba yako. Lala chini kwa muda unapopata nafasi. Pumzisha mwili wako. Ujauzito unaweza kuja na stress sana lakini hakikisha hazikushindi, jinsi unavozidi kupumzika ndivo jinsi unaonekana mrembo.

IMEPITIWA: JUNI 2020