Mtandao #1 kwa Afya ya Mama na Mtoto

Address:

P. O. Box 38995, Dar es Salaam, Tanzania

Umuhimu wa Asidi ya Foliki Kipindi cha Ujauzito.

Asidi ya foliki ni shujaa katika mimba! Kumeza vitamini kabla ya kupata ujauzito kwa kiwango kinachokubalika cha mikrogramu 400mcg kabla na wakati wa ujauzito huweza kusaidia matatizo ya kuzaliwa nayo kwenye ubongo, mgongo na uti wa mgongo wa mtoto wako. Ni vyema kumeza kidonge cha asidi ya foliki kila siku kama unategemea au wewe ni mjamzito tayari.

Asidi ya foliki (Folic acid) ni nini?

Asidi ya foliki ni aina ya vitamini B inayoitwa “folate” inayotengenezwa na mwanadamu maabara (inajulikana kama vitamini B9). “Folate” inafanya kazi muhimu kwenye utengenezaji wa chembe damu nyekundu na pia husaidia katika kukinga dhidi ya kasoro katika neva za fahamu na hivyo kuepusha dosari za kimaumbile katika ubongo, mgongo na uti wa mgongo. Chakula bora chenye wingi wa asidi ya foliki ni “fortified cereals”. Folati hupatikana zaidi kwenye mbogamboga zenye rangi kijani iliyokolea na matunda jamii ya chungwa.

Ni lini uanze kutumia asidi ya foliki?

Matatizo ya kuzaliwa nayo (dosari katika neva za fahamu) huanza kutokea ndani ya wiki ya 3-4 ya ujauzito (siku 28) baada ya mimba kutungwa, kabla hata mama kujua kuwa ni mjamzito. Hivyo ni muhimu kuwa na “folate” tayari kwenye mzunguko wa mwili wako kwenye kipindi hiki muhimu cha mwanzoni ambapo ndio ubongo na uti wa mgongo wa mtoto wako unajijenga.

Kama ulizungumza na daktari wako kipindi ulichokuwa unataka kupata ujauzito, inawezekana alishakushauri tayari kuanza kutumia vitamini na asidi ya foliki. Tafiti moja ilionesha wanawake waliotumia asidi ya foliki kwa kuanzia mwaka kabla ya kupata ujauzito walipunguza uwezekano wa kujifungua mapema kabla ya muda (kabla ya wiki 37) kwa asilimia 50 au zaidi.

Tafiti zinaonesha nusu ya mimba zote hazikuwa zimepangwa hivyo inapendekezwa kuwa mwanamke yeyote anayetarajia kupata ujauzito atumie mickrogramu 400 za vidonge vya foliki asidi kila siku, akianza kabla ya kupata ujauzito na kuendelea namna hiyo kwa wiki 12 za ujauzito. Muda huu wa wiki 12 za mwanzo wa ujauzito ndiyo muda ambao ubongo na mfumo wa neva unajengwa na kukua

Shirika la kuzuia magonjwa la Marekani (CDC) linashauri Vilevile shirika wanawake wote walio kwenye umri wa kuweza kuwa wajawazito kutumia asidi ya foliki kila siku. Hivyo hata ukiamua kuanza kutumia asidi ya foliki mapema zaidi ni vyema zaidi.

Kama utaamua kununua nyongeza ya vitamini wewe mwenyewe, ni vyema ukazungumza pia na daktari wako baada ya kupata ujauzito ili kuwa na uhakika kuwa nyongeza hiyo ya vitamini ina mjumuisho wa kila kitu unachotakiwa ukipate kwa ujauzito wako ikiwemo asidi ya foliki.

Kiasi gani cha asidi ya foliki nitumie?

Dozi inayoelekezwa kwa wanawake wote waliopo kwenye umri wa kuweza kupata ujauzito ni mikrogramu 400 au 400mcg za folati kila siku. Ikiwa wewe ni mjamzito au unajaribu kupata ujauzito unashauriwa kutumia foliki asidi mapema kadiri uwezavyo na ndani ya wiki 12 za kwanza za ujauzito. Kufanya hivi kutamsaidia mtoto kukua vizuri na kawaida.

Daktari anaweza kukushauri kutumia dozi kubwa zaidi ya foliki asidi ikiwa uko katika hatari kubwa ya kupata dosari katika neva za fahamu (neural tube defects) wakati wa ujauzito.

Huu ndio mchanganuo wa kiasi cha asidi ya foliki kinachoelekezwa kwa wanawake wajawazito kwa siku

  • Ukiwa unataka kupata ujauzito – 400mcg
  • Miezi mitatu ya kwanza ya ujauzito – 400mcg
  • Kuanzia mwezi wa 4 hadi wa 9 wa ujauzito – 600mcg
  • Ukiwa unanyonyesha – 500mcg.

Mama ambaye tayari amepata mtoto mwenye dosari katika neva za nyuroni (mfumo wa fahamu) anahitaji ajadiliane na daktari wake kama atahitaji vidonge vya foliki na dozi yake itakuwa ni ipi. Tafiti zinaonesha kwamba matumizi ya mikrogramu 4,000 kwa mwezi mmoja kabla na katika kipindi cha miezi mitatu ya mwanzo wa ujauzito zinaweza kusaidia kutatua tatizo hili. Tafadhali usitumie dawa hizi mwenyewe bila kujadiliana na daktari kwanza.

Asidi ya foliki ina faida gani?

Bila kuwa na asidi ya foliki ya kutosha, dosari katika neva za fahamu na hivyo kuepusha kasoro za kimaumbile katika ubongo, mgongo na uti wa (neural tube defects). Magonjwa haya ni kama:

  • Spina bifida: Kutokukamilika ukuaji wa uti wa mgongo au pingili za uti wa mgongo.
  • Anencephaly: Kutokukamilika kwa ukuaji wa sehemu kubwa ya ubongo.

Watoto wenye “Anencephaly” mara nyingi hawaishi muda mrefu na wale wenye “spina bifida” huwa na ulemavu maisha yao yote. Habari njema ni kwamba kutumia nyongeza ya asidi ya foliki kipindi cha ujauzito inaweza kumuepusha mtoto wako kupata magonjwa haya kwa zaidi ya asilimia 50.

Kama utatumua kabla na wakati wa ujauzito, asidi ya foliki inaweza kumkinga mtoto wako dhidi ya:

  • Mdomo sungura
  • Kuzaliwa kabla ya muda (Njiti)
  • Kuzaliwa na uzito mdogo
  • Mimba kutoka
  • Ukuaji dhaifu tumboni

Asidi ya foliki pia inahusishwa na kupunguza hatari ya kupata:

  • Matatizo kwenye ujauzito
  • Magonjwa ya moyo
  • Kiharusi
  • Aina baadhi ya saratani
  • Ugonjwa wa “Alzheimer”

Je, kuna vyanzo vingine vya folati?

Vyakula vilivyo na foliki asidi katika kiwango kiubwa ni kama:

  • Mboga za majani kama spinachi, kabichi, loshu, broccoli
  • Mimea jamii ya kunde kama maharage, mbaazi, njegere, njugu
  • Karanga, njugumawe, nazi na korosho
  • Matunda jamii ya sitrusi kama machungwa, machenza, limao n.k
  • Nafaka zisizokobolewa
  • Maini na samaki
  • Vyakula vilivyoongezwa foliki asidi.

Kumbuka

  • Kichefuchefu, kupoteza hamu ya kulan a kuvimbiwa ni madhara yanayoweza kutokea kwa mjamzito kama matokeo ya kutumia vidonge hivi. Ulaji wa chakula kidogo kidogo badala ya kula milo mikubwa mitatu kwa siku, kula na kunywa taratibu na kufanya mazoezi mepesi mara kwa mara yanaweza kusaidia dalili hizi unazoweza kupata kama matokeo ya kutumia asidi ya foliki. Ikiwa dalili hizi zinaendelea kuwa mbaya, wasiliana na daktari/mkunga anayesimamia maendeleo ya ujauzito wako mara moja.
  • Mtoto tumboni yuko katika hatari ya kupata dosari katika mfumo wa fahamu ikiwa: mama mjamzito aliwahi kupata ujauzito ulipata dosari katika mfumo wa neva za fahamu, wewe au mwezi wako ana kasoro katika neva za fahamu aliyozaliwa nayo,katika familia yako au mwezi wako kuna historia ya watu kuzaliwa na dosari katika neva za fahamu, mjamzito ana kisukari,mjamzito ana uzito mkubwa uliopitiliza na mjamzito ana ugonjwa wa siko seli.
  • Mama ambaye hakutumia foliki asidi kabla au miezi ya awali ya ujauzito ajadiliane na daktari/mkunga anayesimamia maendeleo ya ujauzito wake, wataweza kukushauri nini kifanyike na dozi kiasi gani itumike kuokoa maisha ya mtoto tumboni. Tafadhali usitumie dawa hizi mwenyewe bila kujadiliana na daktari kwanza.

IMEPITIWA: JUNI,2021.

Vifahamu vyakula bora na vile vinavyokatazwa kipindi cha ujauzito

Ni vyakula gani vya kuepuka kutumiwa na wajawazito?

Ili mtoto azaliwe akiwa na afya njema pamoja na akili timamu, akiwa tumboni lazima alishwe lishe bora na mlo sahihi. Mwenye jukumu la kutoa lishe bora na sahihi kwa kiumbe kilichomo tumboni ni mama. Anatakiwa kujua aina ya vyakula anavyopaswa kula. Vivyo hivyo, anatakiwa kujua aina ya vyakula vya kuviepuka.

Katika makala ya leo, tunaangalia orodha ya vyakula vilivyokatazwa. Mama mja mzito haruhusiwi kuvila vyakula vifuatavyo kwa faida ya kiumbe kilichomo tumboni na kwa faida yake mwenyewe:

Nyama mbichi

Epuka kula samaki au nyama mbichi au iliyopikwa lakini haikuiva vizuri. Utajiepusha na uwezekano wa kula bakteria na vijidudu vingine hatari kwa afya ya mtoto tumboni. Mjamzito anapokula nyama, anatakiwa kuhakikisha imeiva sawasawa.

‘Soseji” na “Sandwich”
Mjamzito haruhusiwi kula ‘soseji’, ‘sandwichi’ za nyama na vyakula vingine vilivyotengenezwa kwa nyama. Inaaminika kuwa nyama zinazoandaliwa kwa ajili ya kutengenezea vyakula kama hivyo, huwa vimewekewa vihifadhi vyakula (preservatives) ambavyo vinaweza visiwe vizuri kwa afya ya mtoto.

Samaki wenye zebaki (Mercury)
Wajawazito wamekatazwa kula samaki wenye kiasi kingi cha madini ya zebaki. Ulaji wa zebaji kwa wajawazito umehusishwa na uzaaji wa watoto taahira. Mfano wa samaki hao ni pamoja na Papa, Chuchunge na dagaa wakubwa.

Mayai Mabichi
Ulaji wa mayai mabichi au vyakula vilivyochanganywa na mayai mabichi, mjamzito haruhusiwi kuvila. Kuna baadhi ya ‘Ice Cream’ na ‘mayonaizi’ hutengenezwa kwa kuchanganywa na mayai mabichi. Mjamzito amekatazwa kuvila vyakula hivyo.

Maini
Maini yana kiwango kikubwa cha madini aina ya chuma. Hata hivyo, yana kiasi kikubwa cha Vitamin A ambacho huweza kuwa na madhara kwa mtoto kikizidi.

Maziwa mabichi
Maziwa mabichi huweza kuwa na bakteria ajulikanae kama ‘Listeria’, ambaye huweza kusababisha kuharibika kwa mimba. Unapokunywa maziwa, hakikisha yamechemshwa au kama ni ya paketi hakikisha ni yale yaliyoandikwa‘Pasteurized’ na siyo ‘Unpasteurized’.

Kafeini (Caffeine)
Ingawa baadhi ya utafiti unaonesha kuwa unywaji wa kiasi kidogo cha kafeini hauna madhara, lakini kuna utafiti mwingine unaonesha kuwa unywaji wa kafeini una uhusiano na kuharibika kwa mimba. Kafeini ni aina ya kirutubisho kinachopatikana ndani ya kahawa.

Iwapo mjamzito atakunywa kahawa, basi anywe kiasi kidogo sana kisichozidi kikombe kimoja kwa siku. Kwa kawaida kahawa hukausha maji mwilini, hivyo unywaji wake husaidia kukauka maji mwilini ambayo ni muhimu sana kwa mjamzito.

Utafiti mwingine unaonesha kuwa kafeini inahusishwa pia na uharibikaji wa mimba, uzaaji wa watoto ‘njiti’ na watoto wenye uzito mdogo. Ni vizuri kunywa maji ya kutosha, maziwa na juisi na kuepuka kunywa vinywaji vyenye kahawa.

Pombe
Hakuna ushahidi unaothibitisha kuwa unywaji wa pombe kiasi kidogo wakati wa ujauzito hauna madhara, kwa maana hiyo matumizi ya pombe hayaruhusiwi kabisa wakati wa ujauzito, hata kama ni kidogo.
Unywaji wa pombe wakati wa ujauzito huweza kuathiri ukuaji mzuri wa mtoto. Kutegemeana na kiasi atakachokunywa mjamzito, pombe inaweza kumsababishia mtoto ugonjwa hatari utokanao na pombe (Fetal Alcohol Syndrome).

Vyakula gani ni muhimu sana kutumiwa na wajawazito?

Lishe bora wakati wa ujauzito ni muhimu sana, kwani lishe hii hutumika kwa mama na mtoto anaendelea kukua tumboni. kwa kawaida mahitaji ya chakula na virutubisho mwilini mwa mwanamke huongezeka wakati wa ujauzito na kadri ujauzito unavyoendelea kukua, virutubisho hivyo hutumika kujenga mwili wa mama na mtoto. hivyo maamuzi ya lishe au lishe mama anayopata huathiri pia maendeleo ya mtoto anayekua mwilini mwake. tutaona vyakula muhimu vya kuzingatia lishe bora wakati wa ujauzito na baadhi ya vitu vya kukwepa.

Mlo kamili (balanced diet), ni muhimu kwa ajili ya maendeleo mazuri ya afya ya mjamzito na mtoto tumboni. Pamoja na mlo kamili mjamzito hupewa virutubisho ziada (supplements) kwa ajili ya kuongeza madini kama ya chuma na Foliki. Mlo kamili unajumuisha vyakula vya wanga, protini, mafuta, vitamini, madini na maji kama inavyochambuliwa hapa chini:

Nafaka na vyakula vya wanga
Vyakula hivi huupa mwili nguvu za kufanya kazi ikiwemo ukuaji wa mtoto tumboni. Vyanzo vya wanga ni kama nafaka mbalimbali(mahindi,mtama,ulezi n.k), viazi, ndizi, mihogo. Ni vizuri mjamzito awe anapata nafaka kamili(whole grains) kama mahindi, ngano na mchele usiokobolewa; cereals n.k.

Nyama, samaki na vyakula vya protini
Hivi ni muhimu kwenye kuujenga mwili, hasa kipindi cha miwezi wa 4 mpaka wa 9 ambacho viungo mbalimbali vya mtoto vinajengwa. Ni muhimu mama apate vyakula vya protini vya kutosha ili kuhakikisha ukuaji wa mtoto unaenda vizuri. Nyama za kuku, ng’ombe, mbuzi, senene, panzi na wanyama wengine ; vyanzo vya protini za mimea kama maharage, soya, njugu, njegere, karanga,korosho n.k . Samaki, maziwa, mayai ni vyanzo vingine vya protini muhimu

Vyakula vya mafuta
Hutumika kwenye kuupatia mwili nguvu pamoja na ujengaji wa seli za mwili. Mara nyingi vyakula kama nyama, karanga, ufuta, alizeti,senene, panzi, samaki na matunnda kama maparachichi huwa na mafuta. Ni vizuri kutumia mafuta yatokanayo na mimea ili kupunguza mafuta yenye lehemu(cholesterol) nyingi.

Mboga za majani na matunda
Matunda na mboga za majani ni sehemu muhimu sana ya mlo wakati wa ujauzito, kwani huupatia mwili vitamini, madini na kambakamba kwa ajili ya kulainisha chakula. Vitamini husaidia kuimarisha kinga ya mwili sambamba na ufanyaji kazi wa mwili. Madini kama ya chuma, kalsiamu, zinki, madini joto(Iodine) na magneziamu ni muhimu kwa ukuaji salama wa mtoto tumboni mwa mama.Vitamini B9 (Foliki asidi) na madini ya chuma hutolewa kama virutubisho ziada kliniki wakati wa ujauzito ili kutosheleza mahitaji ya mwili na kuzuia hatari ya upungufu wa damu kutokea.

Maji
Maji ni muhimu kwenye mmenyenyo na unyonywaji wa chakula, pia husaidia kuzuia choo kigumu, mwili kuvimba na maambukizi ya mfumo wa mkojo (UTI). Inashauriwa mjamzito anywe maji si chini ya lita 2.3 kwa siku, yanaweza kuwa katika chai, juisi, soda, au maji yenyewe. Ni vema zaidi kama akinywa maji kama maji zaidi na kupunguza vinywaji kama soda.

Mfano wa mpangilio wa mlo

Ili kuhakikisha mlo kamili mjamzito anaweza kufuata mfano wa mpangilio wa mlo ufuatao. Katika mpangilio huu inashauriwa kuchagua aina moja ya chakula kutoka katika kila herufi A mpaka E ili kuweza kuupata mlo kamili.

Mfano:

Mlo wa Asubuhi:
A – Chungwa/ Embe/ Ndizi mbivu/ Parachichi
B – Mkate/ Maandazi/ Chapati/ Vitumbua/ Uji
C – Karoti
D – Mayai
E – Maziwa/ Mtindi/ Siagi/ Maziwa ya Soya

Mlo wa Mchana:
A – Parachichi/ Papai/ Ndizi/ Embe na chungwa
B – Ugali/ Wali/ Ndizi/ Makande/ Tambi
C – Mchicha/ matembele/ Mnavu/ Kisamvu/ Spinach/ Kabeji
D – Maharage/ Samaki/ Kuku/ Njugu/ Nyama/ Dagaa
E – Maziwa/ Mtindi/ Siagi/ Maziwa ya Soya.

Mlo wa Usiku:
A – Parachichi/ Papai/ Ndizi/ Embe na Chungwa
B – Wali/ Ndizi/ Viazi/ Tambi/ Chapati
C – Mchicha/ Matembele/ Mnavu/ Kisamvu/ Spinach/ Kabeji,
D – Maharage/ Samaki/ Kuku/ Njugu/ Nyama/ Dagaa
E – Maziwa/Mtindi/Siagi/Maziwa ya Soya.

Imepitiwa: July 2017