Mtandao #1 kwa Afya ya Mama na Mtoto

Address:

P. O. Box 38995, Dar es Salaam, Tanzania

Kwanini chunusi hutokea na namna ya kupambana nazo

Chunusi ni nini?

Chunusi ni ugonjwa wa ngozi unaowaathiri watu wengi katika kipindi fulani cha maisha yao. Ugonjwa huu husababisha vipele vidogo vidogo vya mafuta kwenye ngozi na wakati mwingine hufanya ngozi kuwa na maumivu au kuhisi kuungua. Viupele hivi hutokea wakati vishimo vya kupitisha jasho katika ngozi vinapozibwa kwa mafuta na seli za ngozi zilizokufa au wadudu yaani bakteria. Mara nyingi chunusi hutokea usoni, mgongoni, kifuani na shingoni. Chunusi huwaathiri takribani asilimia 80% ya watu wenye umri kati ya miaka 11-30. Ugonjwa huu hutokea zaidi wasichana kuanzia miaka 14-17 na wavulana kuanzia miaka 16-19.

Jinsi gani chunusi hutokea?

Kawaida ngozi ina vishimo vidogo vidogo vya kutolea jasho,mafuta na seli zilizozeeka kutoka ndani ya mwili. Katika ngozi pia kuna tezi ya mafuta iitwayo ‘sebacous gland’ inayotoa mafuta yaitwayo sebum. Uzalishaji wa sebum nyingi na seli za ngozi zilizokufa husababisha kuziba kwa vishimo vidogo vidogo vya ngozi vinapitisha jasho katika ngozi na kusababisha kuvimba na mara nyingine kujaa kwa usaa na kusababisha chunusi. Licha ya hayo chunusi pia huchangiwa na sababu nyinginezo kama:

  • Mabadiliko ya homoni
  • Bakteria
  • Matibabu
  • Kizazi(genetics)

Jinsi gani ya kupambana na chunusi?

Kuna njia nyingi za matibabu za kupunguza chunusi zikijumuisha kubadili hali ya maisha, taratibu na dawa. Kula kabohidrati chache na zinazomeng’enywa kwa urahisi, kama vile sukari, kunaweza kusaidia. Usijaribu kuviminya au kuvisugua kwa nguvu viupele kwasababu hufanya ngozi kuuma na kutengeneza makovu ya kudumu. Jiepushe kutumia manukato au vipodozi kwenye ngozi yenye chunusi. Tumia bidhaa za urembo zisizoziba matundu madogo madogo ya ngozi yako.

Chunusi pia huweza kutibiwa kwa matumizi ya tiba asili kama matumizi ya matunda na viungo kama vitunguu swaumu, mdalasini na vingine. Hii ni njia nzuri ya kupatia ngozi unafuu na tiba mbadala na rafiki kwa ngozi yako. Zifuatazo ni baadhi ya tiba asili za chunusi na salama kwa ngozi yako:

Mdalasini wa unga na asali.

Kwa wale ambao wanasumbuliwa sana na chunusi iwe, usoni, kifuani, mgongoni n.k wanaweza tumia mchanganyiko mzuri wa asali na mdalasini wa unga kwa kupaka angalau mara moja kwa siku. AsaliI na mdalasini  zinasaidia kuponyesha kwasababu zina tabia za ANTI-BACTERIAL (zinaua na kuzuia mazalia ya bacteria) Jinsi ya kufanya:

  1. Chukua vijiko vitatu (3) vya chai vya asali
  2. Chukua nusu kijiko cha chai cha mdalasini wa unga safi
  3. Changanya pamoja kupata uji uji mzuri
  4. Paka sehemu yenye chunusi na kisha kaa nayo kwa angalau dakika 10-30 kisha osha kwa maji ya uvuguvugu.

ANGALIZO: MDALASINI unaweza kuwasha kwenye ngozi hivyo unashauriwa ujaribu kupaka kidogo kwenye kiganja cha mkono kwanza ili kupata uhakika kua haitakusumbua.

Matango:

Unaweza kutumia tango kwa kuondoa chunusi na hata kuondoa mabaka mabaka katika ngozi na kuifanya ngozi yako kuonekana yenye afya na yenye kuvutia. Matango ni mazuri sana kwa kusafishia uso na haswa ukiwa na chunusi. Kata tango na kisha liponde ponde (unaweza kutumia blenda) kisha paka au kandika usoni. Acha likae kwa muda wa dakika 15 hadi 20 hivi, kisha suuza kwa maji baridi. Unaweza kurudia kwa siku mara mbili mpaka mara tatu hadi utakapopona.

Asali:

Matumizi ya asali kutibu chunusi huwezesha ngozi, iwe na afya na nyororo. Kwa sababu kwenye asali kuna virutubisho vingi vyenye kazi ya kuua vimelea (bacteria) na kuzuia uchafu na kusinyaa kwa ngozi. Weka asali kidogo sehemu ilio athirika na iache kwa muda mrefu kadri uwezavyo. Vilevile unaweza kupaka uso mzima au hata mwili mzima ukitaka. Sababu asali inarutubisha ngozi ya mwili na kuifanya iwe na afya na mwonekano mzuri. Ukisha ridhika na muda wa asali kwenye ngozi yako unaweza kusafisha kwa kutumia maji ya vuguvugu.

Papai:

Unaweza kushangaa, lakini matumizi ya papai yameonyesha matokeo mazuri sana katika kuondoa chunusi usoni na kusafisha sehemu zingine za mwili. Ponda ponda kiasi kidogo cha papai na upakae sehemu yenye chunusi, kisha liache kwa muda mrefu kadri uwezavyo. Ukisha ridhika na muda unaweza kujisafisha kwa kutumia maji ya kawaida. Unaweza kurudia mara kadhaa kila siku kama unataka.

 

Imepitiwa: Feb 2018

Mba wa nywele na matibabu yake

Mba ni nini?

Mba katika nywele ni ugonjwa wa ngozi unaowapata watu wengi. Hali hii husababisha kuwepo kwa vipande vidogo vidogo vyeupe vya ngozi kama ukurutu, ambavyo huweza kukudhalilisha. Usiwe na shaka! Tatizo hili linaweza kutatuliwa kwa matunzo mazuri ya ngozi na kichwa.

Kisayansi, kawaida ngozi hujimenya seli za ngozi ziliyozeeka, na hizi seli hupotea bila kugundulika. Vipande vidogo vya mba vinasababishwa na ongezeko la seli za ngozi katika kichwa, ongezeko hili husababisha pia ongezeko la seli za ngozi zilizozeeka kutolewa. Seli hizi zikikutana na mafuta kwenye nywele na kichwa, pamoja zinaonekana na kufanya mba.

Utagunduaje una mba kichwani?

Kubanduka kwa ngozi ya kichwa kwa kasi ni moja ya dalili ya mba katika kichwa chako. Kubanduka huku kwa ngozi kuna ambatana na kuwashwa kwa ngozi ya kichwa, ambapo inapelekea kuwepo kwa vipande vidogo vidogo vyeupe vya ngozi(ukurutu) kwenye kichwa, nywele na mabega.

Aina za mba wa kichwani

Mba katika kichwa ni hali inayowakuta watu wengi katika jamii zetu. Kuna aina mbili za mba katika kichwa:

  • Mba wa kawaida/ wastani aina hii inaweza kutibika kwa matumizi ya shampoo, na tiba asili za kutengeneza nyumbani kama vile mafuta ya nazi na juisi ya alovera.
  • Mba mkali au uliokithiri, aina hii ya mba katika kichwa inaambatana na kuwashwa kwa kichwa, kuvimba na uwepo wa mba wenye urefu sawa na nyweleza kichwani. Mba katika hatua hii unaweza kutibika kwa dawa zilizoshauriwaa na wataalamu wa afya.

Mba kichwani unasababishwa na nini?

Hakuna chanzo maalumu kinachojulikana cha mba katika kichwa, ila zipi sababu ambazo zinatajwa na watu kuwa vyanzo vya mba kichwani. Miongoni mwa visababishi vya mba katika kichwa ni kama:

Chakula: Ulaji wa vyakula vyenye mafuta, sukari na chumvi nyingi unaweza kusababisha mba kichwani. Pia ulaji wa vyakula vyenye maziwa vinaweza kuchangia kuwepo kwa mba kichwani.

Usafi: usafi duni wa kichwa na nywele ni moja ya sababu za kuwa na mba kichwani, ni vema kusafisha kichwa na nywele mara tatu mpaka nne kwa wiki.

Vyanzo vingine vya mba kichwani vinatajwa kuwa:

  • Msongo wa mawazo
  • Mabadiliko ya homoni
  • Utumiaji wa vipodizi vya nywele sana kama vile jeli za kulaimisha nywele.
  • Kuwa na ngozi ya mafuta sana au kavu sana
  • Kurithi kutoka kwa mzazi.
  • Utumiaji wa hali ya juu wa “chlorinated swimmimg pools”.

Matibabu ya mba wa kichwani

Mba unaweza kupotea ghafla bila matibabu au unaweza kuhitaji kutunza kichwa na nywele kwa kutumia shampoo iliyo na dawa. Mara nyingine mba katika kichwa unaweza kuchukua wiki nyingi kutibika. Baadhi ya matibabu ya mba wa kichwani yanaweza kuwa ya tiba asili au tiba ya kisasa. Inashauriwa zaidi kutumia tiba ya asili kutibu mba wa kichwani, mojawapo wa tiba hizo za asili ni kama:

Matumizi ya mafuta yakupika nyumbani ya nazi na juisi ya kutengeneza ya alovera. Juisi ya alovera inaweza kutumika kama shampoo ya kuosha kichwa na nywele na mafuta ya nazi kwaajili ya kulainisha ngozi na nywele.

Matumizi ya juisi ya limao, juisi ya kimao ina asidi ya citric inayoweza kushambulia fangasi zinazosababisha ukurutu wa ngozi ya kichwa na pia inasaidia kupandisha juu ngozi zilizokufa juu na kuweza kuzisafisha kwa urahisi. Kamua limao na upate juisi ambayo itatumika kusugua kichwani kisha suuza na maji,fanya hivi kila ukitaka kuosha nywele.

Utajikinga vipi usipate mba wa kichwani

Ni vema kchukua hatua ili kuzuia mba kichwani ili usifikie hatua ya hatari zaidi, yafuatayo ni baadhi ya mambo yanayoweza kufuatwa ili kupunguza au kutokomeza kabisa mba kichwani:

  • Kula kawaida, mlo wenye afya ulio jumuisha matunda na mbogamboga kwa wingi. Punguza vyakula vyenye mafuta, sukari na chumvi kwa wingi.
  • Safisha kichwa na nywele zako walau mara tatu mpaka nne kwa wiki, na suuza kwa maji mengi.

Jaribu tiba asili kwa nywele zako kama mafuta ya kupika nyumbani ya nazi pamoja na juisi ya alovera kutibu nywele zako.

Imepitiwa: Feb 2018