Mtandao #1 kwa Afya ya Mama na Mtoto

Address:

P. O. Box 38995, Dar es Salaam, Tanzania

Zifahamu Aina Mbalimbali za Uzazi wa Mpango

Uzazi wa Mpango ni Nini?

Uzazi wa mpango ni maamuzi ya hiari ya mtu au wenza juu ya ni wakati gani waanze kuzaa, watoto wangapi wazae, wapishane kwa umri gani na lini waache kuzaa. Uzazi wa mpango unawahusu wenza wote wawili, kwahiyo ni vizuri kuliongelea hili pamoja. Hata hivyo chaguzi nyingi za uzazi wa mpango huanzia kwa mwanamke, kwahiyo ni muhimu kwa mwanamke kuamua kutumia njia ile itakayo kubaliana na mwili wake.

Uzazi wa Mpango una Faida Gani?

  • Pamoja na kumuwezesha mama na mtoto kuwa na afya njema, uzazi wa mpango una faida nyingi kwa wanawake, wanaume, watoto, familia na jamii kwa ujumla:
  • Unamsaidia mama kurudi katika hali yake ya zamani ambayo ilisumbuliwa na hali ya ujauzito, uchungu na kujifungua, mama atakuwa mwenye nguvu, afya nzuri na mchangamfu. Na pia atakuwa na muda mzuri wa kurudisha afya yake kabla ya kupata ujauzito mwingine.
  • Unamuwezesha kuhudumia familia yake vizuri na kuwa na maisha bora. Utakuwa na muda, fedha na mahitaji muhimu kwa familia yako kama chakula, mavazi, elimu, mapenzi na huduma zote muhimu. Mama anapata muda wa kutosha wakujishughulisha na mambo mengine ya kiuchumi na kimaendeleo kwa ajili ya familia na jamii kwa ujumla.
  • Mama na baba wanapata muda mzuri wa kujishughulisha zaidi na mambo na mahitaji yao binafsi.
  • Unasaidia kukuza uchumi na maendeleo ya nchi.

Nani Anapaswa Kutumia Uzazi wa Mpango?

Yoyote mwenye umri wa kuzaa au anatarajia kufikia umri huo anapaswa kufikiria kuhusu uzazi wa mpango. Uzazi wa mpango ni muhimu kwa:

  • Wanawake na wanaume
  • Watu walioa na kuolewa au ambao hawajaoa wala kuolewa
  • Watu wenye watoto au bado hawajapata watoto.

Ni Wakati Gani Mtu Atumie Uzazi wa Mpango?

Umri sahihi wa kuanza kutumia uzazi wa mpango ni kuanzia miaka ishirini (20) na thelathini na tano (35). Ujauzito ni hatari kwa mama na mtoto endapo mama atajifungua chini ya umri wa miaka ishirini (20) au zaidi ya miaka thelathini na tano (35) vilevile ni hatari kwa mama atakaejifungua zaidi ya watoto wanne au watoto wasipopishana. Wenza wanatakiwa kusubiri angalau miaka miwili kabla ya kupata mtoto mwingine pia wafikirie kutumia njia za kisasa za uzazi wa mpango wakati wote ambao hawajapanga kupata mtoto.

Njia za Uzazi wa Mpango ni Zipi?

Kuna njia nyingi za uzazi wa mpango ambazo zinaweza kutumiwa na mtu au wenza waweze kusubiri, kuchelewesha, au kupunguza idadi ya watoto watakaowazaa. Zipo njia za mda mfupi, mda mrefu na za kudumu.

Njia za muda mfupi

Hizi ni njia za kisasa za uzazi wa mpango ambazo unaweza kuzibadilisha. Unaweza kupata ujauzito pindi utakapoacha kuzitumia. Njia hizi ni nzuri kwa mama anayetaka kupata ujauzito baada ya miaka miwili baada ya kujifungua. Nazo ni:

Njia ya vichecheo-njia hizi zina vichocheo ni sawa na vichocheo vya kawaida vilivyomo kwenye mwili wa mwanamke.

Njia ya vidonge-vidonge hivi hutumiwa na wanawake kila siku. Vidonge vya uzazi wa mpango ambavyo hutumiwa na mwanamke huwa na homoni ambazo huepusha mwanamke kupata mimba kwa kuzuia yai la mwanamke kutokupevuka. Vidonge vya uzazi wa mpango havizuii maambukizi ya magonjwa ya ngono.

Njia ya sindano-mama huchoma sindano kila baada ya miezi mitatu (3). Sindano ni kama vidonge na kipandikizi huzuia yai la mwanamke kupevuka kwa kutoa homoni itakayo kukinga usipate mimba. Njia hizi hazitakuzuia kupata/ kuambukizwa magonjwa ya ngono.

Njia ya dharura ya vidonge vya uzazi wa mpango-humezwa na mama ili kuzuia kupata mimba kwa mama aliyejamiana bila kutumia kinga yeyote. Hivi vinaweza kuzuia mimba hadi siku tano baada ya kujamiana.

Njia za Kizuizi

Kondom za kike na kiume-ni muhimu kutumia ipasavyo kila unapofanya ngono. Hii ni njia pekee ya uzazi wa mpango ambayo inazuia vyote, mimba, magonjwa ya ngono ukiwemo virusi vya ukimwi. Zinazuia shahawa za mwanaume kuingia kwenye uke wa mwanamke.

Njia za asili

Kukosa hedhi kwa kunyonyesha mfululizo

Hii ni njia ya asili ambayo inatokea kwa mwanamke anayenyonyesha na ni ya kuaminika zaidi wakati mama huyo bado hajaanza kuona siku zake za hedhi na ili hayo yote yatokee ni lazima mama awe anamnyonyesha mwanae mara kwa mara usiku na mchana na mtoto awe na umri chini ya miezi sita (6).

Elimu ya kujua siku hatari katika uzazi

Hii inawezekana ikiwa mama anaufahamu mzunguko wake mzima wa siku zake za hedhi na kujua ni zipi siku za hatari za kushika mimba. Yeye na mwenza wanatakiwa kuacha kabisa kufanya ngono siku hizo za hatari.

Kukojoa nje

Hii inafanywa na mwanamume wakati wa tendo la ndoa ambapo humwaga shahawa zake nje ya uke.

Njia za muda mrefu

Hizi ni njia ambazo pia zinaweza kurudiwa. Unaweza kupata ujauzito mara utakapoacha kuzitumia. Hizi ni nzuri ikiwa unataka kusubiri zaidi ya miaka miwili kabla ya kupata mtoto mwingine.

Njia ya vipandikizi

Hiki ni kijiti cha plastiki (chenye urefu wa milimita nne) anachowekewa mwanamke chini ya ngozi kwenye mkono wake kinaweza kuwa kimoja au viwili. Hivi huzuia mwanamke asipate ujauzito kwa muda kati ya miaka 3 hadi 5 kutegemea na aina ya vipandikizi alivyotumia. Hutoa homoni ambazo hulizuia yai la mwanamke kupevuka na kukuepusha kupata mimba. Kipandikizi hiki kinauwezo wa kukaa kwa miaka mitatu hadi mitano lakini hakitakuzuia kupata/kuambukizwa magonjwa ya ngono.

Njia ya kitanzi

Ni kifaa kidogo chenye shaba na plastiki ambacho huwekwa kwenye mji wa mimba. Hichi hukuzuia usipate mimba mpaka miaka kumi na mbili (12), unaweza kukitoa wakati wowote utakapoamua au kuhitajia kupata mtoto.

Njia ya kudumu

Hizi ni njia huwezi kuzirudia na ukitumia huwezi kupata mtoto tena. Na hutumiwa na watu ambao hawataki kupata mtoto tena. Nazo ni;

Kufunga kizazi kwa mwanaume

Njia hii inahusisha upasuaji mdogo ambapo mirija ya uzazi ya mwanaume ukatwa au kufungwa hivyo kuzuia yai kusafiri na kukutana na shahawa. Mwanaume anaendelea kuwa na hamu ya kujamiiana na kutoa mbegu lakini mbegu zake hazitaweza kutunga mimba

Kufunga kizazi kwa mwanamke

Njia hii inahusisha upasuaji mdogo inafanyika kwa kuziba au kukata mirija ya kizazi kuzuia yai kukutana na mbegu. Mwanamke ataendelea kuwa na hamu ya kujamiiana na kuona siku zake za hedhi.

Utafahamu Vipi Kuwa Njia Gani ya Uzazi wa Mpango ni Sahihi Kwako?

Inategemea na mtu mwenyewe au wenza kuamua njia gani ni sahihi kwao. Tembelea kituo cha afya kilicho karibu nawe uonane na wahudumu wa afya wataweza kukufahamisha njia sahihi kwako.

Kumbuka sio njia hizi zote zinaweza kupatikana kila mahali, kwahiyo zungumza kuhusu njia hizi za uzazi wa mpango na muhudumu wa afya unaemwamini mahali ulipo

IMEPITIWA: OKTOBA, 2021.

Umuhimu wa Asidi ya Foliki Kipindi cha Ujauzito.

Asidi ya foliki ni shujaa katika mimba! Kumeza vitamini kabla ya kupata ujauzito kwa kiwango kinachokubalika cha mikrogramu 400mcg kabla na wakati wa ujauzito huweza kusaidia matatizo ya kuzaliwa nayo kwenye ubongo, mgongo na uti wa mgongo wa mtoto wako. Ni vyema kumeza kidonge cha asidi ya foliki kila siku kama unategemea au wewe ni mjamzito tayari.

Asidi ya foliki (Folic acid) ni nini?

Asidi ya foliki ni aina ya vitamini B inayoitwa “folate” inayotengenezwa na mwanadamu maabara (inajulikana kama vitamini B9). “Folate” inafanya kazi muhimu kwenye utengenezaji wa chembe damu nyekundu na pia husaidia katika kukinga dhidi ya kasoro katika neva za fahamu na hivyo kuepusha dosari za kimaumbile katika ubongo, mgongo na uti wa mgongo. Chakula bora chenye wingi wa asidi ya foliki ni “fortified cereals”. Folati hupatikana zaidi kwenye mbogamboga zenye rangi kijani iliyokolea na matunda jamii ya chungwa.

Ni lini uanze kutumia asidi ya foliki?

Matatizo ya kuzaliwa nayo (dosari katika neva za fahamu) huanza kutokea ndani ya wiki ya 3-4 ya ujauzito (siku 28) baada ya mimba kutungwa, kabla hata mama kujua kuwa ni mjamzito. Hivyo ni muhimu kuwa na “folate” tayari kwenye mzunguko wa mwili wako kwenye kipindi hiki muhimu cha mwanzoni ambapo ndio ubongo na uti wa mgongo wa mtoto wako unajijenga.

Kama ulizungumza na daktari wako kipindi ulichokuwa unataka kupata ujauzito, inawezekana alishakushauri tayari kuanza kutumia vitamini na asidi ya foliki. Tafiti moja ilionesha wanawake waliotumia asidi ya foliki kwa kuanzia mwaka kabla ya kupata ujauzito walipunguza uwezekano wa kujifungua mapema kabla ya muda (kabla ya wiki 37) kwa asilimia 50 au zaidi.

Tafiti zinaonesha nusu ya mimba zote hazikuwa zimepangwa hivyo inapendekezwa kuwa mwanamke yeyote anayetarajia kupata ujauzito atumie mickrogramu 400 za vidonge vya foliki asidi kila siku, akianza kabla ya kupata ujauzito na kuendelea namna hiyo kwa wiki 12 za ujauzito. Muda huu wa wiki 12 za mwanzo wa ujauzito ndiyo muda ambao ubongo na mfumo wa neva unajengwa na kukua

Shirika la kuzuia magonjwa la Marekani (CDC) linashauri Vilevile shirika wanawake wote walio kwenye umri wa kuweza kuwa wajawazito kutumia asidi ya foliki kila siku. Hivyo hata ukiamua kuanza kutumia asidi ya foliki mapema zaidi ni vyema zaidi.

Kama utaamua kununua nyongeza ya vitamini wewe mwenyewe, ni vyema ukazungumza pia na daktari wako baada ya kupata ujauzito ili kuwa na uhakika kuwa nyongeza hiyo ya vitamini ina mjumuisho wa kila kitu unachotakiwa ukipate kwa ujauzito wako ikiwemo asidi ya foliki.

Kiasi gani cha asidi ya foliki nitumie?

Dozi inayoelekezwa kwa wanawake wote waliopo kwenye umri wa kuweza kupata ujauzito ni mikrogramu 400 au 400mcg za folati kila siku. Ikiwa wewe ni mjamzito au unajaribu kupata ujauzito unashauriwa kutumia foliki asidi mapema kadiri uwezavyo na ndani ya wiki 12 za kwanza za ujauzito. Kufanya hivi kutamsaidia mtoto kukua vizuri na kawaida.

Daktari anaweza kukushauri kutumia dozi kubwa zaidi ya foliki asidi ikiwa uko katika hatari kubwa ya kupata dosari katika neva za fahamu (neural tube defects) wakati wa ujauzito.

Huu ndio mchanganuo wa kiasi cha asidi ya foliki kinachoelekezwa kwa wanawake wajawazito kwa siku

  • Ukiwa unataka kupata ujauzito – 400mcg
  • Miezi mitatu ya kwanza ya ujauzito – 400mcg
  • Kuanzia mwezi wa 4 hadi wa 9 wa ujauzito – 600mcg
  • Ukiwa unanyonyesha – 500mcg.

Mama ambaye tayari amepata mtoto mwenye dosari katika neva za nyuroni (mfumo wa fahamu) anahitaji ajadiliane na daktari wake kama atahitaji vidonge vya foliki na dozi yake itakuwa ni ipi. Tafiti zinaonesha kwamba matumizi ya mikrogramu 4,000 kwa mwezi mmoja kabla na katika kipindi cha miezi mitatu ya mwanzo wa ujauzito zinaweza kusaidia kutatua tatizo hili. Tafadhali usitumie dawa hizi mwenyewe bila kujadiliana na daktari kwanza.

Asidi ya foliki ina faida gani?

Bila kuwa na asidi ya foliki ya kutosha, dosari katika neva za fahamu na hivyo kuepusha kasoro za kimaumbile katika ubongo, mgongo na uti wa (neural tube defects). Magonjwa haya ni kama:

  • Spina bifida: Kutokukamilika ukuaji wa uti wa mgongo au pingili za uti wa mgongo.
  • Anencephaly: Kutokukamilika kwa ukuaji wa sehemu kubwa ya ubongo.

Watoto wenye “Anencephaly” mara nyingi hawaishi muda mrefu na wale wenye “spina bifida” huwa na ulemavu maisha yao yote. Habari njema ni kwamba kutumia nyongeza ya asidi ya foliki kipindi cha ujauzito inaweza kumuepusha mtoto wako kupata magonjwa haya kwa zaidi ya asilimia 50.

Kama utatumua kabla na wakati wa ujauzito, asidi ya foliki inaweza kumkinga mtoto wako dhidi ya:

  • Mdomo sungura
  • Kuzaliwa kabla ya muda (Njiti)
  • Kuzaliwa na uzito mdogo
  • Mimba kutoka
  • Ukuaji dhaifu tumboni

Asidi ya foliki pia inahusishwa na kupunguza hatari ya kupata:

  • Matatizo kwenye ujauzito
  • Magonjwa ya moyo
  • Kiharusi
  • Aina baadhi ya saratani
  • Ugonjwa wa “Alzheimer”

Je, kuna vyanzo vingine vya folati?

Vyakula vilivyo na foliki asidi katika kiwango kiubwa ni kama:

  • Mboga za majani kama spinachi, kabichi, loshu, broccoli
  • Mimea jamii ya kunde kama maharage, mbaazi, njegere, njugu
  • Karanga, njugumawe, nazi na korosho
  • Matunda jamii ya sitrusi kama machungwa, machenza, limao n.k
  • Nafaka zisizokobolewa
  • Maini na samaki
  • Vyakula vilivyoongezwa foliki asidi.

Kumbuka

  • Kichefuchefu, kupoteza hamu ya kulan a kuvimbiwa ni madhara yanayoweza kutokea kwa mjamzito kama matokeo ya kutumia vidonge hivi. Ulaji wa chakula kidogo kidogo badala ya kula milo mikubwa mitatu kwa siku, kula na kunywa taratibu na kufanya mazoezi mepesi mara kwa mara yanaweza kusaidia dalili hizi unazoweza kupata kama matokeo ya kutumia asidi ya foliki. Ikiwa dalili hizi zinaendelea kuwa mbaya, wasiliana na daktari/mkunga anayesimamia maendeleo ya ujauzito wako mara moja.
  • Mtoto tumboni yuko katika hatari ya kupata dosari katika mfumo wa fahamu ikiwa: mama mjamzito aliwahi kupata ujauzito ulipata dosari katika mfumo wa neva za fahamu, wewe au mwezi wako ana kasoro katika neva za fahamu aliyozaliwa nayo,katika familia yako au mwezi wako kuna historia ya watu kuzaliwa na dosari katika neva za fahamu, mjamzito ana kisukari,mjamzito ana uzito mkubwa uliopitiliza na mjamzito ana ugonjwa wa siko seli.
  • Mama ambaye hakutumia foliki asidi kabla au miezi ya awali ya ujauzito ajadiliane na daktari/mkunga anayesimamia maendeleo ya ujauzito wake, wataweza kukushauri nini kifanyike na dozi kiasi gani itumike kuokoa maisha ya mtoto tumboni. Tafadhali usitumie dawa hizi mwenyewe bila kujadiliana na daktari kwanza.

IMEPITIWA: JUNI,2021.

Kuanzishiwa uchungu, sababu na faida zake

Kuanzishiwa uchungu

Kuna sababu kadhaa zinazoweza kusababisha kuanzishiwa uchungu kuwa lazima. Uchungu utatakiwa kuanzishwa iwapo:

1. Umepitiliza siku yako ya kujifungua, mara nyingi utaanzishiwa uchungu kati ya wiki ya 41 na 42
2. Chupa imevunjika lakini uchungu haujaanza
3. Una kisukari; mara nyingi huanzishiwa uchungu mara tu baada ya wiki 38
4. Umepata shinikizo la damu la mimba (pre-eclampsia)
5. Una utokaji wa damu usio wa kawaida
6. Mtoto wako ametambulika kuwa amechoka tayari
7. Mrija wa chakula wa uzazi (placenta) kushindwa kupeleka chakula na oksigeni kwa mtoto
8. Unategemea kujifungua mapacha na daktari wako ameshauri uanzishiwe uchungu

Kama unafikiria ni kwa namna gani utafanikiwa kujifungua kwa kawaida, basi kuna vidokezo kadhaa vya kuzingatia:

1. Achana kabisa na sigara, pombe na madawa yoyote kipindi chote cha ujauzito wako
2. Mara zote wasiliana na daktari wako kabla ya kutumia dawa ya aina yoyote
3. Hudhuria kliniki mara kwa mara
4. Kula mlo bora na kamili
5. Fanya mazoezi mara kwa mara
6. Muone daktari mara moja pale unapopata dalili hatarishi au usiyoielewa

Kumbuka msaada wa kitaalamu wa kukupa uchungu ukihitajika haimaanishi kwamba kuna kitu ulikosea katika ujauzito wako. Wanawake wengi wanakuwa na ujauzito wenye afya kabisa lakini wanakuja kuhitaji kuanzishiwa uchungu wakati wa kujifungua. Kwa makadirio mwanamke mmoja kati ya watatu atahitaji msaada wa kitaalamu wakati wa kujifungua.

Kuanzishiwa uchungu kunaweza kufanyika kwa njia mbali mbali, ikiwemo:

1. Kutenganisha nyavunyavu (membrane sweep): Moja ya njia maarufu za kuanzishiwa uchungu. Wakati wa tukio hili daktari au mkunga wako atatenganisha nyavunyavu nyembamba zilizozunguka kichwa cha mtoto wako kutoka kwenye mlango wa uzazi. Ni kawaida kwa kitendo hiki kurudiwa mara kwa mara.
2. Prostaglandini: Homoni hii ya kutengeneza maabara inayopatikana kama kimiminika laini au kidonge huingizwa ukeni. Homoni hii husaidia kuivisha mlango wako wa uzazi ili uweze kufunguka na kutanuka kiurahisi. Inaweza ikahitajika kuwekewa dozi kadhaa mpaka ianze kufanya kazi sawasawa.
3. AROM (Artificial rupture of membranes) – Kupasua chupa: Njia hii inahusisha kupasua chupa yako kwa kukusudia. Njia hii ilikuwa ndio njia maarufu zamani lakini kwa sasa inatumika zaidi kuharakisha uchungu kuliko kuanzisha uchungu.
4. Syntocinon: Hii ni kama homoni ya oksitosini iliyotengenezwa maabara. Husaidia kukuharakishia kupata uchungu. Hutumiwa zaidi pale njia ya kutenganisha nyavunyavu (membrane sweep) pamoja na kutumia homoni ya Prostaglandini zote zimeshindwa kufanya kazi. Dawa hii hutolewa kwa dripu.
5. Kuanzishiwa uchungu kwa njia ya kawaida: Oksitosini ni homoni ambayo inahusishwa moja kwa moja na uchungu. Homoni hii pia huwa inatolewa pale matiti yanapoguswa guswa, kunyonywa n.k. Hivyo basi kwa miaka mingi inafahamika kwamba kufanya mapenzi pia ni njia ya kawaida kabisa inayoweza kukuanzishia uchungu.

Kama taratibu za kukuanzishia uchungu zote hazitafanikiwa, basi itabidi ujifungue kwa upasuaji kadiri itakavyoonekana ni muhimu kiafya. Lakini, wanawake wengi wameanzishiwa uchungu na wakaweza kupata uchungu na kujifungua kawaida.

Imepitiwa: Dec 2017

Dalili hatari kipindi cha ujauzito ambazo si za kupuuzia

Hata kama umesoma sana na kuongea na wazazi mbalimbali kuhusu dalili mbali mbali kipindi cha ujauzito, bado itatokea baadhi ya wakati ambapo utakuwa huna uhakika kama unavyojisikia ni kawaida au la.
Dalili zifuatazo ni muhimu kuzipa uzito wake na kuzifuatilia kwa makini. Kama ukizipata dalili hizi ni vyema kuwasiliana na mkunga, daktari wako au kituo cha kliniki ya wajawazito haraka iwezekanavyo.

Nina maumivu tumbo la kati

Maumivu makali au vichomi katikati au juu kidogo ya tumbo, ikiambatana na kchefuchefu na kutapika, inaweza kumaanisha kitu kimoja kati ya vifuatavyo. Unaweza ukawa na:

  • Kuvimbiwa kulikopitiliza
  • Kiungulia
  • Tumbo kuchafuka

Kama upo kwenye miezi mitatu hadi sita ya ujauzitowako, hii inawezza kumaanisha presha mimba ya awali. Hii ni dalili hatari na itahitaji matibabu ya haraka.

Nina maumivu ya tumbo ka chini

Maumivu makali upande mmoja au pande zote kwenye tumbo lako la chini yanahitaji uchunguzi kugundua kama sio kitu cha kushtua.

Kwa kiwango cha chini kabisa inaweza pia ikawa ni dalili za:

  • Mimba nje ya mji wa mimba
  • Mimba kutoka
  • Uchungu uliowahi
  • Uvimbe kwenye kizazi – uliovunjika na kuanza kuvuja damu kwa ndani yake.
  • Kuachia kwa kondo la nyuma (placenta)

Nina homa

Kama una homa na una jotoridi zaidi ya digrii 37.5c, na bila dalili za mafua, ni vyema kumuona daktari ndani ya siku hiyo hiyo.

Kama jotoridi ni zaidi ya nyuzi joto 39c wasiliana au fika kwa daktari wakati huo huo bila kusubiri. Inawezekana umepata maambukizi. Daktari wako atakuandikia dawa za kupambana na bakteria na kushauri upate mapumziko. Kama nyuzi joto za mwili wako zitapanda zaidi ya nyuzi joto 39 kwa muda mrefu itamuathiri mtoto wako tumboni.

Ninaona maruerue (mbili mbili) na nyota nyota

Muone daktari haraka kama, katika miiezi mitatu hadi sita ya ujauzito wako, kuona kwako kunapata shida ya:

  • Kuona mbili mbili
  • Kuona ukungu
  • Kuona giza
  •  Kuona nyota nyota

Matatizo haya kwenye mfumo wa kuona yanaweza yakawa ni dalili za presha mimba ya awali (Pre-eclampsia)

Mikono na miguu yangu imevimba

Kuvimba au kuumuka (oedema) kwenye mikono, uso, macho ni kawaida mwishoni mwa ujauzito. Mara nyingi sio kitu cha kuleta wasiwasi. Lakini kama kuvimba huku ni kukubwa na kumetokea ghafla, kukiambatana na kichwa kuuma na matatizo ya kuona kwako, inawezekana ukawa na presha mimba ya awali (pre-eclampsia). Kama utaona dalili yoyote kati ya hizi wasiliana na daktari bila kuchelewa.

Nina maumivu makali ya kichwa yasiyopungua

Kama maumivu makali ya kichwa yanaendelea kwa masaa mawili hadi matatu, na pia una matatizo ya kuona kwako na kuvimba sana kwa mwili wako, inawezekana ukawa na presha mimba ya awali (pre-eclampsia). Kama presha mimba ya awali ikitokea, mara nyingi huwa ni katika nusu ya mwisho ya ujauzito wako au punde tu baada ya kujifungua.

Ninavuja damu ukeni

Matone au kutokwa na damu kidogo bila maumivu ni kawaida kipindi cha mwanzo cha ujauzito. Inawezekana ni kuvuja kwa damu kunakosababishwa na zile homoni zinazouongoza mzunguko wako wa hedhi ziliendelea kutolewa kwa nguvu ya ziada na kusababisha kuvuja kwa damu kidogo.
Usiwe na wasiwasi kuhusu aina hii ya kutokwa damu, kwani hali hii huondoka yenyewe na si rahisi kumdhuru mtoto wako.
Pamoja na hilo, ni vyema kuwasiliana na mkunga au daktari wako kama utapata kutokwa na damu ukeni katika hatua yoyote ya ujauzito wako. Inaweza ikawa inamaanisha kuna tatizo kubwa kwenye ujauzito wako kama:

  • Kutoka damu tofauti na ilivyo kawaida kwa hedhi yako, inaweza ikawa nyepesi zaidi na nyeusi zaidi kuliko kawaida. Hili pamoja na maumivu makali ya muda mrefu upande mmoja wat umbo lako inaweza ikawa ni dalili ya mimba nje ya mji wa mimba.
  • Kutokwa kwa damu kwingi, ikiungana na maumivu ya muda mrefu ya mgongo au tumbo la chini inaweza kuwa ni dalili ya kutoka kwa mimba.
  • Kutoka kwa damu kwa ghafla kusiko ambatana na maumivu yoyote.

Imepitiwa: April 2017

Vifahamu vyakula bora na vile vinavyokatazwa kipindi cha ujauzito

Ni vyakula gani vya kuepuka kutumiwa na wajawazito?

Ili mtoto azaliwe akiwa na afya njema pamoja na akili timamu, akiwa tumboni lazima alishwe lishe bora na mlo sahihi. Mwenye jukumu la kutoa lishe bora na sahihi kwa kiumbe kilichomo tumboni ni mama. Anatakiwa kujua aina ya vyakula anavyopaswa kula. Vivyo hivyo, anatakiwa kujua aina ya vyakula vya kuviepuka.

Katika makala ya leo, tunaangalia orodha ya vyakula vilivyokatazwa. Mama mja mzito haruhusiwi kuvila vyakula vifuatavyo kwa faida ya kiumbe kilichomo tumboni na kwa faida yake mwenyewe:

Nyama mbichi

Epuka kula samaki au nyama mbichi au iliyopikwa lakini haikuiva vizuri. Utajiepusha na uwezekano wa kula bakteria na vijidudu vingine hatari kwa afya ya mtoto tumboni. Mjamzito anapokula nyama, anatakiwa kuhakikisha imeiva sawasawa.

‘Soseji” na “Sandwich”
Mjamzito haruhusiwi kula ‘soseji’, ‘sandwichi’ za nyama na vyakula vingine vilivyotengenezwa kwa nyama. Inaaminika kuwa nyama zinazoandaliwa kwa ajili ya kutengenezea vyakula kama hivyo, huwa vimewekewa vihifadhi vyakula (preservatives) ambavyo vinaweza visiwe vizuri kwa afya ya mtoto.

Samaki wenye zebaki (Mercury)
Wajawazito wamekatazwa kula samaki wenye kiasi kingi cha madini ya zebaki. Ulaji wa zebaji kwa wajawazito umehusishwa na uzaaji wa watoto taahira. Mfano wa samaki hao ni pamoja na Papa, Chuchunge na dagaa wakubwa.

Mayai Mabichi
Ulaji wa mayai mabichi au vyakula vilivyochanganywa na mayai mabichi, mjamzito haruhusiwi kuvila. Kuna baadhi ya ‘Ice Cream’ na ‘mayonaizi’ hutengenezwa kwa kuchanganywa na mayai mabichi. Mjamzito amekatazwa kuvila vyakula hivyo.

Maini
Maini yana kiwango kikubwa cha madini aina ya chuma. Hata hivyo, yana kiasi kikubwa cha Vitamin A ambacho huweza kuwa na madhara kwa mtoto kikizidi.

Maziwa mabichi
Maziwa mabichi huweza kuwa na bakteria ajulikanae kama ‘Listeria’, ambaye huweza kusababisha kuharibika kwa mimba. Unapokunywa maziwa, hakikisha yamechemshwa au kama ni ya paketi hakikisha ni yale yaliyoandikwa‘Pasteurized’ na siyo ‘Unpasteurized’.

Kafeini (Caffeine)
Ingawa baadhi ya utafiti unaonesha kuwa unywaji wa kiasi kidogo cha kafeini hauna madhara, lakini kuna utafiti mwingine unaonesha kuwa unywaji wa kafeini una uhusiano na kuharibika kwa mimba. Kafeini ni aina ya kirutubisho kinachopatikana ndani ya kahawa.

Iwapo mjamzito atakunywa kahawa, basi anywe kiasi kidogo sana kisichozidi kikombe kimoja kwa siku. Kwa kawaida kahawa hukausha maji mwilini, hivyo unywaji wake husaidia kukauka maji mwilini ambayo ni muhimu sana kwa mjamzito.

Utafiti mwingine unaonesha kuwa kafeini inahusishwa pia na uharibikaji wa mimba, uzaaji wa watoto ‘njiti’ na watoto wenye uzito mdogo. Ni vizuri kunywa maji ya kutosha, maziwa na juisi na kuepuka kunywa vinywaji vyenye kahawa.

Pombe
Hakuna ushahidi unaothibitisha kuwa unywaji wa pombe kiasi kidogo wakati wa ujauzito hauna madhara, kwa maana hiyo matumizi ya pombe hayaruhusiwi kabisa wakati wa ujauzito, hata kama ni kidogo.
Unywaji wa pombe wakati wa ujauzito huweza kuathiri ukuaji mzuri wa mtoto. Kutegemeana na kiasi atakachokunywa mjamzito, pombe inaweza kumsababishia mtoto ugonjwa hatari utokanao na pombe (Fetal Alcohol Syndrome).

Vyakula gani ni muhimu sana kutumiwa na wajawazito?

Lishe bora wakati wa ujauzito ni muhimu sana, kwani lishe hii hutumika kwa mama na mtoto anaendelea kukua tumboni. kwa kawaida mahitaji ya chakula na virutubisho mwilini mwa mwanamke huongezeka wakati wa ujauzito na kadri ujauzito unavyoendelea kukua, virutubisho hivyo hutumika kujenga mwili wa mama na mtoto. hivyo maamuzi ya lishe au lishe mama anayopata huathiri pia maendeleo ya mtoto anayekua mwilini mwake. tutaona vyakula muhimu vya kuzingatia lishe bora wakati wa ujauzito na baadhi ya vitu vya kukwepa.

Mlo kamili (balanced diet), ni muhimu kwa ajili ya maendeleo mazuri ya afya ya mjamzito na mtoto tumboni. Pamoja na mlo kamili mjamzito hupewa virutubisho ziada (supplements) kwa ajili ya kuongeza madini kama ya chuma na Foliki. Mlo kamili unajumuisha vyakula vya wanga, protini, mafuta, vitamini, madini na maji kama inavyochambuliwa hapa chini:

Nafaka na vyakula vya wanga
Vyakula hivi huupa mwili nguvu za kufanya kazi ikiwemo ukuaji wa mtoto tumboni. Vyanzo vya wanga ni kama nafaka mbalimbali(mahindi,mtama,ulezi n.k), viazi, ndizi, mihogo. Ni vizuri mjamzito awe anapata nafaka kamili(whole grains) kama mahindi, ngano na mchele usiokobolewa; cereals n.k.

Nyama, samaki na vyakula vya protini
Hivi ni muhimu kwenye kuujenga mwili, hasa kipindi cha miwezi wa 4 mpaka wa 9 ambacho viungo mbalimbali vya mtoto vinajengwa. Ni muhimu mama apate vyakula vya protini vya kutosha ili kuhakikisha ukuaji wa mtoto unaenda vizuri. Nyama za kuku, ng’ombe, mbuzi, senene, panzi na wanyama wengine ; vyanzo vya protini za mimea kama maharage, soya, njugu, njegere, karanga,korosho n.k . Samaki, maziwa, mayai ni vyanzo vingine vya protini muhimu

Vyakula vya mafuta
Hutumika kwenye kuupatia mwili nguvu pamoja na ujengaji wa seli za mwili. Mara nyingi vyakula kama nyama, karanga, ufuta, alizeti,senene, panzi, samaki na matunnda kama maparachichi huwa na mafuta. Ni vizuri kutumia mafuta yatokanayo na mimea ili kupunguza mafuta yenye lehemu(cholesterol) nyingi.

Mboga za majani na matunda
Matunda na mboga za majani ni sehemu muhimu sana ya mlo wakati wa ujauzito, kwani huupatia mwili vitamini, madini na kambakamba kwa ajili ya kulainisha chakula. Vitamini husaidia kuimarisha kinga ya mwili sambamba na ufanyaji kazi wa mwili. Madini kama ya chuma, kalsiamu, zinki, madini joto(Iodine) na magneziamu ni muhimu kwa ukuaji salama wa mtoto tumboni mwa mama.Vitamini B9 (Foliki asidi) na madini ya chuma hutolewa kama virutubisho ziada kliniki wakati wa ujauzito ili kutosheleza mahitaji ya mwili na kuzuia hatari ya upungufu wa damu kutokea.

Maji
Maji ni muhimu kwenye mmenyenyo na unyonywaji wa chakula, pia husaidia kuzuia choo kigumu, mwili kuvimba na maambukizi ya mfumo wa mkojo (UTI). Inashauriwa mjamzito anywe maji si chini ya lita 2.3 kwa siku, yanaweza kuwa katika chai, juisi, soda, au maji yenyewe. Ni vema zaidi kama akinywa maji kama maji zaidi na kupunguza vinywaji kama soda.

Mfano wa mpangilio wa mlo

Ili kuhakikisha mlo kamili mjamzito anaweza kufuata mfano wa mpangilio wa mlo ufuatao. Katika mpangilio huu inashauriwa kuchagua aina moja ya chakula kutoka katika kila herufi A mpaka E ili kuweza kuupata mlo kamili.

Mfano:

Mlo wa Asubuhi:
A – Chungwa/ Embe/ Ndizi mbivu/ Parachichi
B – Mkate/ Maandazi/ Chapati/ Vitumbua/ Uji
C – Karoti
D – Mayai
E – Maziwa/ Mtindi/ Siagi/ Maziwa ya Soya

Mlo wa Mchana:
A – Parachichi/ Papai/ Ndizi/ Embe na chungwa
B – Ugali/ Wali/ Ndizi/ Makande/ Tambi
C – Mchicha/ matembele/ Mnavu/ Kisamvu/ Spinach/ Kabeji
D – Maharage/ Samaki/ Kuku/ Njugu/ Nyama/ Dagaa
E – Maziwa/ Mtindi/ Siagi/ Maziwa ya Soya.

Mlo wa Usiku:
A – Parachichi/ Papai/ Ndizi/ Embe na Chungwa
B – Wali/ Ndizi/ Viazi/ Tambi/ Chapati
C – Mchicha/ Matembele/ Mnavu/ Kisamvu/ Spinach/ Kabeji,
D – Maharage/ Samaki/ Kuku/ Njugu/ Nyama/ Dagaa
E – Maziwa/Mtindi/Siagi/Maziwa ya Soya.

Imepitiwa: July 2017

Mazoezi Mepesi Kipindi cha Ujauzito

Mazoezi kipindi cha ujauzito.
Je ni salama?

Kufanya mazoezi ni jambo ambalo binadamu wengi hulifanya mara kwa mara ikiwa ni mpango wa kimaisha au hulifanya mara moja moja. Mazoezi ni kitendo cha kuushughulisha mwili kwa njia mbalimbali. Mazoezi yaliyojipatia umaarufu ni kama kutembea, kukimbia, kushiriki michezo mbalimbali na hata watu hutumia vifaa maalumu vya mazoezi kuishughulisha miili yao. Hivi karibuni vituo vingi vya mazoezi ambavyo vilikuwa maarufu kwenye nchi zilizoendelea vinaanza pia kuonekana barani Afrika.

Mazoezi ni mazuri kwa afya ya mwili na akili. Pia mazoezi ni njia nzuri kupata afya bora. Ikiwa ni kawaida kabisa watu wa umri wowote ule kushiriki katika mazoezi, huwa inazua mjadala mara kwa mara ni kwa namna gani wajawazito wafanye mazoezi. Kwanza kabisa je wanaruhusiwa kisayansi kufanya mazoezi?
Waandishi wa Idhaa ya Kiswahili ya DW waliwahi kuyasema haya kuhusu mabadiliko ya mtazamo wa kisayansi kuhusu kufanya mazoezi wakati wa ujauzito

Nukuu

Miaka 20 iliyopita, madaktari wangemuambia mama mjamzito kupumzika kadiri awezavyo, kwa kuhofia kuathiri ukuaji wa kiumbe aliye tumboni, na kusababisha uchungu wa mapema au hata mimba kutoka. Hata hivyo chuo cha wakunga na madaktari wa wanawake cha nchini Marekani ACOG, kinasema kujishughulisha kimwili kuna hatari ndogo sana na kunawasaidia wanawake wengi zaidi.
Miongozo ya hivi karibuni ya chuo cha ACOG, kuanzia mwishoni mwa mwaka 2015, ambayo inatazamwa kama alama teule duniani kote, inabainisha kuwa wasiwasi kuhusu uzazi wa njiti, kutoka kwa mimba au kudumaa kwa kijusi kutokana na mazoezi haujathibitishwa. Kwa mujibu wa ACOG, wanawake wanatakiwa kuhimizwa kushiriki katika mazoezi ya viungo na kuimarisha misuli kabla na baada ya ujauzito.

Nicole Goebel/Iddi Ssessanga – DW

Aina za Mazoezi Kipindi cha Ujauzito

Mazoezi ya dakika kati ya 20 hadi 30 yanapendekezwa kwa siku nyingi za wiki kwa mwenye ujauzito usio na matatizo yoyote – wakiwemo wale walio na uzito uliopitiliza au wasio na shughuli za kutosha. Haijalishi pia wewe ni mtu wa umri gani. Inapendekeza baadhi ya michezo, kama vile kuogelea au kutembea, ambayo ni rahisi kwa viungo.

Faida za Mazoezi

Mazoezi yanaweza kukusaidia kuwa mwenye afya na kukuepushia kisukari cha ujauzito, ambacho kinaweza kukidhuru kiumbe tumboni na kinachohitaji mlo makhsusi, na katika wakati mwingine sindano za insulini hata kama kwa kawaida hauna ugonjwa wa kisukari. Kulingana na ACOG, mazoezi yanaweza pia kupunguza hatari ya tatizo linalosababishwa na kupanda kwa shinikizo la damu na vilevile kujifungua kwa njia ya upasuaji.

Wakati watafiti wakiendelea kutafuta njia za kuzuia uzito uliopitiliza hasa miongoni mwa watoto wadogo, faida za mazoezi wakati wa ujauzito zimevutia usikivu wa wanasayansi. Wakati hakuna ushahidi kuonyesha kuwa mtoto wako atakuwa na umbo la kimichezo kwa sababu umekuwa ukifanya mazoezi wakati wa ujauzito, mazoezi yanaweza kuathiri ukuaji wa viungo vya mtoto huyo, na hivyo kuwa na faida katika utoto wake na kuendelea.
Ikiwa mazoezi laini ni jambo usilotegemea kufanya, mazoezi yalioboreshwa ya yoga yanaweza kukusaidia kubakia mnyumbufu na kukusaidia pia dhidi ya maumivu ya mgongo – ambayo ni tatizo la kawaida wakati wa ujauzito, kwa sababu kina mama wanakuwa na kawaida ya kuumwa mgongo kutokana na uzito ulioongezeka.

Hivyo hakuna kisingizio cha kutokufanya mazoezi- lakini unapaswa kuchagua mazoezi yako kwa umakini. Michezo ya kugusana kama vile soka, ndondi, mpira wa kikapu/pete haishauriwi. Pia jiepushe na michezo ya kujitupa majini, kupanda, kupanda juu ya zaidi ya mita 2,000, na jambo lolote linaloweza kukuweka katika hatari ya kuanguka. Pia jihadhari sana wakati wa joto kali, vilevile pumzike ukiwa na dalili zozote za mafua, maumivu ya kichwa au kizunguzungu.

IMEPITIWA: OKTOBA,2021.